Rais wa FIFA anavyoishi maisha ya kifahari

    • Author, Dale Johnson
    • Nafasi, Periodista de fútbol, BBC Sport
  • Iliyochapishwa
  • Muda wa kusoma: Dakika 7

Gianni Infantino alishuka kutoka kwenye ndege huko Cali na kupokelewa kwenye uwanja wa ndege na Rais wa Shirikisho la Soka la Colombia.

Rais wa Shirikisho la soka la Colombia Ramón Jesurún, ambaye ni mshirika wa karibu wa Infantino, aliona hiyo kama fursa ya kuonyesha kumuunga mkono, huku viongozi hao wawili wakitabasamu katika picha iliyowekwa kwenye akaunti ya Instagram ya shirikisho hilo.

Infantino hakusafiri kwenda Colombia kushiriki katika mikutano yoyote ya kawaida iliyokuwa imepangwa kwa Ijumaa. Bali alihudhuria uzinduzi wa Rais mpya wa nchi hiyo, Abelardo de la Espriella.

Infantino aliandamana na Alejandro Domínguez, Rais wa Shirikisho la Soka la Amerika Kusini, Conmebol, ambaye alisifu rekodi ya Infantino pamoja na Kombe la Dunia la 2026 aliloliita "lenye mafanikio makubwa", na pia akaonyesha kumuunga mkono.

Haya ndiyo maisha ya Rais wa FIFA

Maisha ya Rais wa FIFA yanajumuisha kujenga uhusiano na baadhi ya watu wenye nguvu zaidi duniani, kama inavyoonekana katika uhusiano wa Infantino na Rais wa Marekani Donald Trump.

Kabla ya kashfa kubwa zaidi kuwahi kuikumba mihula yake, yaani mpango uliofeli wa FIFA Forward Enterprise (FFE), Infantino alikuwa mtu mwenye nguvu kubwa ambaye alionekana kana kwamba asingeweza kuyumbishwa.

Sasa, baada ya kuomba msamaha na kueleza nia yake ya kuvumilia upinzani dhidi ya mpango wake wa kuiuzia kampuni za uwekezaji binafsi sehemu ya Kombe la Dunia la wanaume, Infantino anaonekana kujaribu kurejea katika hali ya kawaida.

Lakini huenda hilo lisiwe rahisi.

Tishio la UEFA kususia mashindano ya FIFA bado lipo. Hilo litajaribiwa katika Kombe la Dunia la Under-20, litakaloanza nchini Poland katika kipindi kisichozidi mwezi mmoja.

Huenda akitiwa moyo na uungwaji mkono alioupata nje ya Ulaya katika siku za hivi karibuni, Infantino hatajisalimisha kwa urahisi.

Lakini je, jukumu la rais wa FIFA ni lipi haswa?

Safari za kidiplomasia za kusimamia soka duniani

Msafara wa magari ya Mercedes yenye vioo vya giza, ukiambatana na magari ya polisi, ulifika katika makao makuu ya FIFA mjini Rabat, Morocco, mapema wiki hii.

Infantino alikuwa amewaita baadhi ya wajumbe wa bodi ya wakurugenzi ya FIFA kujadili mpango wake wa kuipa kampuni ya uwekezaji binafsi asilimia 21 ya biashara na pia biashara ya mfumo wa tiketi.

Hivi ndivyo raia huyo mwenye uraia wa Uswisi na Italia anavyosafiri: kati ya safari za ndege kwenye ndege ya Qatar Airways ya kifahari iliyowekwa kwa ajili yake.

Ndege hiyo ilimwezesha kufanya hadi safari tatu kwa siku na, kutokana na hilo, kuhudhuria mechi mbili wakati wa Kombe la Dunia la 2026.

Aina hiyo ya mapokezi na usafiri inaonekana kama ya rais wa nchi, na si sana kama ya kiongozi wa taasisi ya michezo.

Hii inamwezesha kusafiri duniani kote kutembelea ofisi rasmi za FIFA, kama ile ya Rabat, ambako alikuwa akifanya kazi wiki iliyopita wakati mjadala kuhusu FFE ukiendelea.

Katika nafasi yake, Infantino anatarajiwa kutembelea nchi zote 211 wanachama wa FIFA ili kuona miradi ya ngazi ya chini ya soka ambayo FIFA imefadhili.

Sehemu ya dhamira yake ni kuiunganisha soka, jambo ambalo haliwezi kufikiwa akiwa tu katika makao makuu ya FIFA mjini Zurich.

Safari za kimataifa ni muhimu ili kuhudhuria mikutano ya mashirikisho ya soka na mashindano ya kimataifa yanayoandaliwa na FIFA. Infantino anahitaji kujenga uhusiano na viongozi wa soka na wanasiasa.

Mwezi Aprili, kabla ya Mkutano wa FIFA mjini Vancouver, mamlaka za eneo hilo zilikataa ombi la kutumia msafara wa usalama wa kiwango cha nne, ambao kwa kawaida hutengwa kwa wakuu wa nchi au Papa.

Polisi wa New Zealand walisema walikataa ombi kama hilo pia wakati wa Kombe la Dunia la Wanawake la 2023.

Pamoja na msafara huo na safari za ndege za kukodi, huja mshahara mkubwa: mara tatu ya kiasi alichokuwa akipokea alipochaguliwa mwaka 2016.

Infantino, aliyekuwa akipata takribani dola milioni 1.7 za Marekani miaka 10 iliyopita, sasa anapata karibu dola milioni 5: mshahara wa msingi wa dola milioni 2.9 pamoja na bonasi iliyothibitishwa ya dola milioni 2.4.

Mtangulizi wake, Sepp Blatter, alipokea kifurushi cha malipo cha dola milioni 3.5 katika mwaka wake wa mwisho akiwa rais wa FIFA.

Infantino pia hupokea posho ya kila siku (per diem) kwa ajili ya kugharamia maisha na gharama nyingine, yenye thamani ya dola 27,600 kwa mwaka, mbali na mshahara wake.

Akiwa kiongozi wa mchezo maarufu zaidi duniani, mtu angeweza kutarajia alipwe mshahara unaolingana na nafasi hiyo.

Infantino pengine anaweza kusema kuwa, kwa kuzalisha mapato yaliyoweka rekodi na fedha za kufadhili vyama wanachama, amethibitisha kuwa anastahili mshahara huo.

Jinsi Infantino na Trump walivyozidi kuwa karibu

Uswahiba wa Infantino na Trump ulionekana kuongeza zaidi hadhi yake.

Watu wengi katika ulimwengu wa soka waliona kuwa ukaribu huo ulianza kumfanya apuuze majukumu yake katika soka.

Mwezi Mei 2025, Infantino alifanya ziara ya kidiplomasia katika Mashariki ya Kati pamoja na Trump na akawasili saa mbili baada ya muda uliopangwa kwenye Mkutano wa FIFA nchini Paraguay.

UEFA ilimtuhumu Infantino kwa kuweka "maslahi yake binafsi ya kisiasa" mbele, na wajumbe wake wakaondoka ukumbini kuonyesha kutoridhishwa kwao.

Jambo lingine lilikuwa Tuzo ya Amani ya FIFA, iliyotolewa kwa Trump wiki chache kabla ya Marekani kuivamia Venezuela ili kumuondoa madarakani Rais Nicolás Maduro na kuanzisha mashambulizi ya anga dhidi ya Iran.

Licha ya ukosoaji huo, kamati ya maadili ya FIFA haikujibu malalamiko kuhusu msimamo wa Infantino wa kutokuwa na upendeleo kisiasa kuhusiana na tuzo hiyo.

Mapema mwaka huu, Infantino alijitokeza kwa kushtukiza katika mkutano wa kwanza wa Bodi ya Amani ya Trump, iliyoundwa kusimamia ujenzi mpya wa Gaza.

Kamati ya Kimataifa ya Olimpiki, ambayo Infantino ni mwanachama aliyealikwa, ilisema kuwa kanuni zake za kutokuwa na upendeleo kisiasa hazikukiukwa.

Hata hivyo, wengi waliona kuwa Infantino alikuwa amejiweka karibu sana na Rais wa Marekani.

Hali hiyo ilizidi kuwa mbaya wakati mshambuliaji wa Marekani, Folarin Balogun, alipoepuka adhabu baada ya kuonyeshwa kadi nyekundu kwenye Kombe la Dunia.

Ulikuwa uamuzi ambao haujawahi kutokea wa kamati ya nidhamu ya FIFA. Trump mwenyewe alisema kwamba alimpigia simu Infantino binafsi na kuomba kadi hiyo ipitiwe upya.

Infantino alisisitiza kuwa huo ulikuwa uamuzi wa chombo huru ambacho hakuna mtu angeweza kukishawishi.

Katika wikendi ya mwisho ya Kombe la Dunia, Trump na Infantino walionekana pamoja katika Trump Tower mjini New York. Rais wa Marekani alisema alikuwa amempigia simu Rais wa FIFA, ambaye "alifanya uamuzi mwingine mzuri".

Kisha, kilele cha uhusiano wa karibu kati ya Infantino na Trump kikawa FIFA Forward Enterprise.

Mwekezaji huyo binafsi alikuwa kampuni inayohusishwa na kaka wa mkwe wa Trump, Jared Kushner.

Infantino mara chache hujibu maswali ya waandishi wa habari

Maswali huru kuhusu mbinu na maamuzi ya Infantino ni machache kwa sababu Infantino huzungumza mara chache na vyombo vya habari.

Katika kipindi cha miaka minne iliyopita, amefanya mikutano miwili tu na waandishi wa habari, yote ikiwa ya saa moja na kufanyika kabla ya kuanza kwa Kombe la Dunia.

Mbali na hilo, Infantino mara nyingi huonekana katika mahojiano yanayotayarishwa na FIFA na kuchapishwa kupitia njia zake rasmi.

Kabla ya Kombe la Dunia la 2026, alijaribu kuelezea kuhusu bei kubwa za tiketi na visa kwa mashabiki.

Hata hivyo, katika mkutano na waandishi wa habari kabla ya Kombe la Dunia, jibu lake la "mnajua, tulieni" alipoulizwa kuhusu mwamuzi wa Somalia, Omar Artan, ambaye alizuiwa kuingia Marekani katika uwanja wa ndege wa Miami, lilizua wasiwasi.

Kwa kutoa taarifa kupitia njia za FIFA, Infantino anaweza kujaribu kuelekeza simulizi kuhusu masuala yanayomhusu.

Taarifa ya FIFA iliyotolewa Jumatano ilionesha kujutia baadhi ya mambo. Lakini pia ilikuwa na onyo.

Taarifa hiyo ilimpa Infantino nafasi ya kujibu, ikisema FIFA "haitavumilia tena mashambulizi dhidi ya uadilifu wake, utawala bora na mchakato wa haki".

Wakosoaji wanasema hoja dhidi yake ni vigumu kupuuzwa

Mvuto wa nafasi hiyo ni mkubwa sana, jambo linaloonekana kutokana na ukweli kwamba kumekuwa na marais wanne tu wa kudumu wa FIFA tangu Stanley Rous alipochaguliwa mwaka 1961.

Nje ya Ulaya, mapato makubwa yaliyopatikana wakati wa uongozi wa Infantino yamefadhili shughuli za soka katika nchi nyingi. Hilo limejenga uaminifu, na ni mfumo unaoonekana kuleta mafanikio.

Hata hivyo, kwa UEFA na baadhi ya vyama vingine vya kitaifa, rekodi hiyo sasa imekuwa ndefu mno.

Wakosoaji wake, wengi wao wakiwa ndani ya soka la Ulaya, wanasema FIFA haiwezi tena kuendeshwa kama mradi wa mtu mmoja mwenye mamlaka yasiyodhibitiwa.

Kupanua Kombe la Dunia kulikuwa sehemu ya ilani ya uchaguzi ya Infantino, lakini ongezeko la timu hadi 64 mwaka 2030 linaonekana kuwa na uwezekano mkubwa ikiwa atapata muhula wa nne.

Kulikuwa pia na upanuzi wa Kombe la Dunia la Klabu msimu huu wa joto. Kombe hilo limechorwa maneno ya heshima binafsi: "Imehamasishwa na Rais wa FIFA Gianni Infantino."

Ugawaji wa Kombe la Dunia la wanaume la miaka miwili ijayo ulisaidia kuhakikisha kuwa Saudi Arabia, mshirika mwingine wa karibu wa Infantino, itakuwa mwenyeji wa mashindano ya mwaka 2034.

Droo ya Kombe la Dunia la mwaka huu ilikuwa tukio refu, la kifahari na la gharama kubwa. Trump alikuwa mstari wa mbele, pamoja na Infantino.

Mashabiki wengi walihisi kuwa bei za tiketi zilikuwa juu sana, huku baadhi ya waliokuwa tayari kulipia tiketi wakinyimwa visa.

FIFA iliamua kutumia soko la pili la tiketi lenye bei zisizo na ukomo na kuchukua asilimia 30 ya kila tiketi iliyouzwa.

Wakosoaji walieleza kuwa faida ilikuwa imepewa umuhimu zaidi kuliko uzoefu wa mashabiki, na mawakili wakuu wa majimbo ya New York na New Jersey waliitaka FIFA kujibu maswali kuhusu taratibu zake za uuzaji wa tiketi.

Licha ya mabishano hayo yote, Infantino alitarajiwa kuchaguliwa tena, kutokana na kiwango kikubwa cha uungwaji mkono alichokuwa nacho kutoka kwa vyama wanachama duniani kote.

Kwa hakika, kabla ya Kombe la Dunia, vyama 111 tayari vilikuwa vimempigia kura ya kumuunga mkono: idadi hiyo ilitosha kumhakikishia ushindi katika uchaguzi wa Urais.

Sasa hali hiyo haijulikani kutokana na mpango wa uwekezaji binafsi wa FIFA ulioshindikana.

UEFA inaona wakati huu kama fursa ya kumlazimisha kujiuzulu.

Lakini, kama inavyoonyesha uwepo wake katika ghafla ya kuapishwa kwa Rais wa Colombia, kumwondoa madarakani kunaweza kuwa jambo gumu sana.