Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Marekani yatishia benki kubwa za Iran, Hormuz yageuka uwanja mpya wa mvutano
Mvutano mpya wa kijeshi kati ya Iran na Marekani umeanza tena baada ya kusitishwa kwa karibu mwezi mmoja, kufuatia shambulio dhidi ya virushia makombora ambavyo Marekani ilisema vilikuwa vinaandaliwa kutumiwa kuweka mabomu ya baharini kwa njia isiyo ya kawaida, kwa kurusha roketi zilizobeba mabomu hayo kuelekea Mlango bahari wa Hormuz.
Kamandi Kuu ya Marekani (CENTCOM) ilitangaza tarehe 30 Agosti kwamba ilikuwa imelenga virushia makombora viwili vya Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran (IRGC) katika Kisiwa cha Lark, karibu na njia za meli za Mlango wa Hormuz.
Msemaji wa CENTCOM, Tim Hawkins, alisema kuwa vikosi vya IRGC vilionekana vikiandaa kurusha "roketi zilizobeba mabomu ya baharini" kuelekea kwenye mlango huo.
Kufuatia shambulio hilo, Iran ililenga kituo cha kijeshi cha Marekani nchini Jordan kwa makombora, na hivyo kurejesha mashambulizi ya kulipizana kati ya pande hizo mbili.
Kwa mujibu wa maelezo ya Marekani, virushia makombora vilivyokuwa Lark vilikusudiwa kuwezesha mabomu ya baharini kutumbukizwa kwenye mlango huo kutoka nchi kavu, bila kuhitaji matumizi ya boti au meli maalumu za kuweka mabomu hayo.
IRGC ilikuwa imewahi kuonesha mfano wa mfumo kama huo katika zoezi la kijeshi. Hata hivyo, shambulio la Lark lilikuwa mara ya kwanza kwa mfumo wa kuweka mabomu ya baharini kwa kutumia roketi kuwa sehemu kuu ya mzozo wa moja kwa moja kati ya nchi hizo mbili.
Shambulio hilo lilitokea siku mbili tu baada ya Kamandi Kuu ya Marekani kutangaza kwamba mabomu ya baharini yaliyowekwa katika njia za kimataifa za meli kwenye Mlango wa Hormuz yalikuwa yameondolewa.
Gazeti la Financial Times liliripoti hivi karibuni kwamba operesheni hiyo ilichukua miezi minne na ilifanywa hasa nyakati za usiku, kwa kutumia wapiga mbizi wa Jeshi la Wanamaji la Marekani, pamoja na boti za roboti na magari yasiyokuwa na waendeshaji yaliyokuwa yakifanya kazi chini ya maji.
Marekani imechukua mfululizo wa hatua za kiuchumi dhidi ya Iran tangu mzozo huo ulipoanza mwezi Februari, ikilenga mauzo ya mafuta, mitandao ya usafirishaji wa meli, njia za ununuzi wa silaha, masuala ya kifedha, mali za kidigitali na usafiri wa anga.
Utawala wa Trump ulizidisha kampeni yake mwezi uliopita kupitia kile ambacho Bisent alikiita "Operesheni ya Kutenga Kiuchumi" (Operation Economic Exclusion).
Operesheni hiyo iliweka vikwazo dhidi ya taasisi, watu binafsi na meli karibu 60, pamoja na kupanua vikwazo vya sekondari kwa wale wanaofanya biashara na Iran katika sekta zikiwemo usafirishaji wa meli, usafiri wa anga, teknolojia, dhahabu na mali za kidigitali.
Wizara ya Hazina ya Marekani ilitangaza Alhamisi kwamba imeweka vikwazo dhidi ya taasisi na watu binafsi nchini Lebanon, Iraq na Uturuki, ambao ilisema wanaunga mkono Hezbollah ya Lebanon na Brigedi za Hezbollah ya Iraq.
Wizara hiyo iliongeza kuwa imeanza kukataa idadi kubwa ya maombi ambayo bado hayajashughulikiwa ya leseni zinazohusiana na miamala na Iran, huku ikiweka kikomo cha kutoa vibali katika mazingira ya kipekee pekee.
Licha ya kuongezeka kwa shinikizo dhidi ya Iran, Rais Trump alitabiri Jumatano kwamba vita hivyo havitaisha hadi baada ya uchaguzi wa katikati ya muhula nchini Marekani, uliopangwa kufanyika mwezi Novemba.
Mvutano unaendelea kuongezeka katika njia za usafirishaji wa baharini, huku Iran ikisema Jumatano kwamba ilishambulia meli 20 zilizojaribu kuvuka Mlango bahari wa Hormuz na kutangaza kupanua "eneo la kutoruhusiwa kuingia" nje ya mlango huo. Wakati huo huo, vyanzo vya serikali ya Yemen viliripoti kwamba waasi wa Houthi walikuwa wamefika katika Visiwa vya Hanish, vilivyoko katika Bahari ya Shamu, hali iliyozua wasiwasi kuhusu usalama wa usafiri wa meli karibu na Mlango wa Bab al-Mandab.
Shirika la Uingereza la Uendeshaji wa Biashara za Baharini (UKMTO) lilisema Alhamisi kwamba makombora manne yasiyotambuliwa yalipiga meli mbili, umbali wa maili nne za baharini magharibi mwa Khasab, nchini Oman. Shambulio hilo lilisababisha moto kwenye mojawapo ya meli hizo, huku hali ya meli nyingine ikiwa haijulikani.
Shirika hilo liliongeza kuwa nahodha wa meli nyingine aliripoti kuona makombora hayo yakizipiga meli hizo mbili, takriban maili sita za baharini kaskazini mwa alikokuwa.
Akirejelea Tehran, Trump alisema Jumatano:
"Nadhani vita vitaisha mara tu uchaguzi utakapokamilika, kwa sababu hawataweza kuendelea kuvumilia kwa muda mrefu zaidi."
Alitoa matamshi hayo akiwa njiani kuelekea Texas kuhudhuria mkutano wa kwanza wa Chama cha Republican kuelekea uchaguzi wa katikati ya muhula. Alirudia matamshi hayo wakati wa mkutano huo, akisema kwamba kuvumilia matatizo ya kiuchumi ya muda mfupi kulikuwa na umuhimu ili kuzuia Tehran kutengeneza silaha za nyuklia.
Trump anakabiliwa na kushuka kwa umaarufu wake katika kura za maoni, pamoja na shinikizo kutoka ndani ya Chama cha Republican la kutaka kumaliza vita na Iran.
Trump aliwaambia waandishi wa habari:
"Mara tu baada ya uchaguzi, bei ya mafuta itashuka kwa kiasi kikubwa."
Aliongeza:
"Nadhani itachukua muda mrefu zaidi, hadi baada ya uchaguzi wa katikati ya muhula."
Alidai pia kwamba Iran:
"Inajitahidi sana kushawishi uchaguzi, ili kundi zuri lakini dhaifu lichukue madaraka", akionekana kurejelea chama cha Democrats "na kuwaacha peke yao na kuwaruhusu kupata silaha yao ya nyuklia."
Rais huyo wa Marekani hakutoa ushahidi wowote kuunga mkono madai yake kuhusu uchaguzi. Wakati huo huo, Tehran imeendelea kukana kwamba inatafuta kutengeneza silaha za nyuklia.
Wakati wa mkutano huo huko Texas, Trump alirudia baadhi ya kauli hizo, akisema kuwa bei ya mafuta itashuka kwa kiasi kikubwa "mara tu tutakaposhinda vita na Iran."
Awali, Rais huyo wa Marekani alitarajia vita hivyo, ambavyo vilikuwa vimeingia mwezi wake wa saba, vingedumu kwa wiki chache pekee. Mzozo huo na athari zake kwa bei za bidhaa mbalimbali, kuanzia mafuta ya petroli hadi chakula, zilisababisha kushuka kwa kiasi kikubwa kwa kiwango cha kumuunga mkono, pamoja na shinikizo kutoka ndani ya chama chake, likiwemo kutoka kwa wafuasi wake waaminifu, la kutaka vita hivyo vikome haraka.
Uchaguzi wa katikati ya muhula utafanyika Novemba 3, huku Republican wakikabiliwa na hatari ya kupoteza udhibiti wa Bunge la Marekani.
Kupanua eneo la "kutoruhusiwa kuingia"
Gazeti la Financial Times liliripoti Ijumaa kwamba mawaziri wa mambo ya nje wa nchi za Ghuba wanatarajia kukutana na mwenzake wa Iran, katika juhudi zinazoongozwa na Oman na Iran za kupata idhini ya makubaliano ya muda ya kusimamia usafiri wa meli kupitia Mlango wa Hormuz.
Gazeti hilo lilinukuu vyanzo viwili vyenye ufahamu wa suala hilo vikisema kuwa mkutano huo umepangwa kufanyika Jumatatu katika mji wa Salalah, ulioko kwenye pwani ya Oman.
Katika hatua ambayo huenda ikazua changamoto zaidi kwa usafiri wa baharini, IRGC walitangaza kupanua "eneo lililowekewa vikwazo", ambalo meli zimepigwa marufuku kuingia bila kuratibu na Tehran.
Msemaji wa Walinzi hao, Hossein Mohebi, alisema:
"Linaanzia takriban eneo la Chabahar, kusini mwa Iran, na linajumuisha sehemu ya Bahari ya Oman pamoja na sehemu nyingine ya Bahari ya Arabia, kando ya njia inayoelekea kwenye Mlango wa Hormuz."
Alifafanua:
"Meli ikiingia katika eneo hilo bila kuratibu, itachukuliwa hatua za adhabu. Hii ina maana kwamba, kwa mfano, ikiwa baadaye itataka kutumia Mlango wa Hormuz au kupata huduma katika eneo fulani, kama vile bima au huduma nyingine zinazohusiana, tutakataa kutoa huduma hizo."
Msemaji wa jeshi la Iran, Hossein Mohebi, alisema Jumatano kwamba madai ya Tehran ya kumaliza vita yanajumuisha kuondolewa kwa vikosi vya Israel kutoka kusini mwa Lebanon na kuachiliwa kwa takriban dola bilioni 24 za mali za Iran zilizozuiwa.
Katika hatua nyingine, Reuters ilinukuu Wall Street Journal Alhamisi ikisema kwamba Iran imeanza tena uzalishaji wa makombora ya balestiki katika vituo vya chini ya ardhi, kwa mujibu wa taarifa kutoka kwa maafisa wa Marekani na Mashariki ya Kati.
Kwa mujibu wa gazeti hilo, Tehran inategemea zaidi kuunganisha makombora kwa kutumia vipengele vilivyohifadhiwa awali, huku ikizalisha kwa kiwango kidogo kuliko ilivyokuwa kabla ya vita.
Mashambulizi ya mabomu kusini mwa Lebanon
Kusini mwa Lebanon, Israel ilitangaza Alhamisi kwamba imeharibu handaki ambazo ilisema zilitengenezwa na Hezbollah chini ya maeneo ya juu ya Ali Taher, katika mkoa wa Nabatieh, kwa ufadhili na mipango kutoka Iran.
Shirika la Habari la Taifa la Lebanon liliripoti "mlipuko mkubwa" katika maeneo hayo ya miinuko, uliosababisha mtikisiko na sauti kubwa ya mlipuko.
Waandishi wa habari wa AFP waliokuwa eneo hilo pia waliripoti kusikia milipuko mikubwa.