Tshisekedi adokeza kuongeza muhula wa tatu wa urais DRC

Chanzo cha picha, Getty Images
Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), Félix Tshisekedi, amesema anaweza kuwania muhula wa tatu wa urais baada ya muda wake wa sasa kumalizika mwaka 2028 ikiwa wananchi wataridhia kupitia kura ya maoni. Katiba ya nchi hiyo kwa sasa inaruhusu mihula miwili pekee ya urais.
Akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari mjini Kinshasa, Tshisekedi alisema hajataka muhula wa tatu moja kwa moja, lakini yuko tayari kuendelea kuongoza ikiwa wananchi watamhitaji. Kauli hiyo imezua mjadala mkubwa nchini humo huku upinzani ukihofia jaribio la kubadili katiba ili kuongeza muda wa utawala wake.
Rais huyo pia amesema uchaguzi mkuu wa mwaka 2028 unaweza usifanyike kwa wakati kutokana na hali mbaya ya usalama mashariki mwa nchi. Waasi wa M23 wameendelea kudhibiti maeneo makubwa ya Kivu Kaskazini na Kivu Kusini, yakiwemo miji muhimu ya Goma na Bukavu.
Tshisekedi ameilaumu Rwanda kwa kuchelewesha juhudi za amani na kunufaika na rasilimali za madini kutoka DR Congo. Rwanda imeendelea kukanusha kuunga mkono waasi wa M23 licha ya madai na ushahidi kutoka mataifa mbalimbali.
Kauli za Tshisekedi zimekuja wakati muswada wa kuruhusu kura ya maoni kuhusu marekebisho ya katiba ukiendelea kujadiliwa bungeni. Upinzani umeonya kuwa jaribio lolote la kubadili ukomo wa mihula ya urais litakuwa “mapinduzi ya kikatiba” yenye lengo la kumweka madarakani Tshisekedi kwa muda mrefu zaidi.


