Kufuatilia waathiriwa wa Ebola ni changamoto, juhudi zinaendelea kuimarika - WHO
Shirika la Afya Duniani (WHO) limetangaza Jumatano kwamba juhudi za kukabiliana na mlipuko wa Ebola katika Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo zinaendelea kuimarika, huku visa 344 vikithibitishwa na vifo 60 kuripotiwa.
Hata hivyo, changamoto zinaendelea, hasa katika kuongeza uwezo wa kupima na kufuatilia waathiriwa.
Mlipuko huo unaosababishwa na ugonjwa wa Bundibugyo, umeenea pia katika nchi jirani ya Uganda, ambapo maambukizi 15 yamethibitishwa, ikiwa ni pamoja na kifo kimoja.
Mkurugenzi Mkuu wa WHO Tedros Adhanom Ghebreyesus alisisitiza kwamba wakati hatua inapigwa, mengi zaidi yanahitajika kufanywa, huku asilimia 45 tu ya mawasiliano ya wale waliokutana na waathiriwa ndiyo yanayofuatiliwa kwa sasa.
Wakati huo huo, Dkt. Tedros Ghebreyesus, ameonya dhidi ya kuwekwa kwa vikwazo vya jumla vya usafiri na baadhi ya nchi kutokana na mlipuko wa unaoendelea wa virusi vya Ebola.
Marufuku ya kusafiri yaliyowekwa na zaidi ya nchi kumi na mbili yanaathiri uwezo wa Shirika la Afya Ulimwenguni kukabiliana vilivyo na mlipuko wa Ebola katika Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo.
Marufuku hiyo ya kusafiri "inatatiza usambazaji na kuzuia mwitikio wa kukabiliana na Ebola," Mkurugenzi Mkuu wa WHO Tedros Adhanom Ghebreyesus aliambia mkutano wa waandishi wa habari.
Wito wa Dkt. Tedros unakuja baada ya Idara ya Uhamiaji, Wakimbizi na Uraia ya Canada kurejelea tena uamuzi wake wa kusitisha utoaji wa stakabadhi za uhamiaji kwa wakazi wa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo, Uganda na Sudan Kusini kwa muda wa siku 90.
Marekani, Bahrain, Mexico na nchi zingine zimeweka vizuizi vya kusafiri, wakati Canada inatekeleza karantini ya siku 21 kwa wasafiri wote wanaofika kutoka Congo.
Kando na hayo, WHO imesema inahitaji angalau dola milioni 115 katika kipindi cha miezi mitatu ijayo ili kukabiliana na dharura hiyo ya kiafya.
Shirika hilo limeeleza kuwa hadi sasa limefanikiwa kupata takribani asilimia 35 ya fedha zinazohitajika.
Soma zaidi: