Moja kwa moja, Zelensky apendekeza mazungumzo ya ana kwa ana na Putin ili kumaliza vita vya Ukraine

Kupitia barua ya wazi aliyomwandikia Putin, Zelensky alisema kuwa ni muhimu viongozi hao wawili kukutana moja kwa moja ili kujadili njia za kurejesha amani kati ya Urusi na Ukraine.

Moja kwa moja

Na Asha Juma

  1. Wananchi washambulia timu ya mazishi DRC, hofu ya Ebola kuenea yaongezeka

    s

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Mamlaka za afya nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), zimeeleza wasiwasi mkubwa baada ya wakazi wa eneo la Katana katika jimbo la Kivu Kusini kushambulia timu maalum ya mazishi ya waathirika wa Ebola.

    Tukio hilo lilitokea Jumatatu na kulazimisha wahudumu wa afya kuacha jeneza walilokuwa wakilisafirisha kutokana vurugu hizo.

    Kwa mujibu wa taarifa za wizara ya afya, mwili wa marehemu uliendelea kushughulikiwa na wananchi wa kawaida baada ya timu hiyo kuondoka. Hatua hiyo inatajwa kuwa hatari kubwa kwa sababu miili ya waathirika wa Ebola inaweza kuendelea kusambaza maambukizi ikiwa haitashughulikiwa kwa kufuata taratibu maalum za afya.

    Tukio hilo limeongeza changamoto katika juhudi za kudhibiti mlipuko wa aina ya Bundibugyo ya Ebola, huku kukiwa na taarifa za mashambulizi mengine dhidi ya wahudumu wa afya na timu za mazishi katika maeneo tofauti. Katika mji wa Bunia, jimbo la Ituri, watu kadhaa walijeruhiwa baada ya wakazi kushambulia timu ya wahudumu wa afya kwenye makaburi.

    Wataalamu wa afya wanaeleza kuwa ukosefu wa imani kutoka kwa baadhi ya wananchi na upinzani dhidi ya hatua za kudhibiti ugonjwa huo vinaendelea kuathiri mapambano dhidi ya Ebola. Baadhi ya familia zimekuwa zikipinga taarifa rasmi za sababu za vifo vya ndugu zao, jambo linalochochea migogoro na wahudumu wa afya.

    Tangu mlipuko huu wa 17 wa Ebola nchini DRC kutangazwa Mei 15, jumla ya wagonjwa 363 wamethibitishwa kuambukizwa huku watu 62 wakifariki dunia. Maambukizi yameendelea kuongezeka katika majimbo ya Ituri, Kivu Kaskazini na Kivu Kusini, hali inayoongeza hofu ya kuenea zaidi kwa ugonjwa huo ikiwa hatua za kudhibiti maambukizi hazitaheshimiwa kikamilifu.

  2. Tetesi za soka: Diomande, Kroupi wazigonganisha Arsenal, PSG na Liverpool

    s

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Arsenal wanakabiliwa na ushindani kutoka kwa Mabingwa wa Ulaya, Paris Saint-Germain, (PSG) katika harakati za kumsajili mshambuliaji Mfaransa Eli Junior Kroupi kutoka Bournemouth, pamoja na mshambuliaji wa Argentina Julian Alvarez anayechezea katika Atletico Madrid. (Independent)

    Liverpool inamtaka winga wa Ivory Coast, Yan Diomande, baada ya kuwasiliana na klabu ya RB Leipzig. Hata hivyo, klabu hiyo ya Ujerumani ina msimamo wa kutomuuza mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 19. (Athletic)

    PSG pia wanamfuatilia Diomande. Inadaiwa kuwa mchezaji huyo mwenyewe angependa zaidi kuhamia PSG kuliko sehemu nyingine yoyote. (Telefoot, via Mirror)

    Beki wa Chelsea, Marc Cucurella, anaangalia uwezekano wa kuondoka Stamford Bridge, huku Atletico Madrid ikijiandaa kutoa ofa yake ya kwanza kwa ajili ya nyota huyo wa Hispania. (Teamtalk)

    s

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Brentford wamepeleka dau la £43m kwa ajili ya kumsajili winga wa Mjerumani Said El Mala kutoka FC Cologne. (Bild) Hata hivyo, El Mala hana nia ya kuhamia klabu hiyo ya Ligi Kuu England. (Sky Sports Germany)

    Juventus wanahitaji angalau £26m ili kumuachia beki wa pembeni wa Italia Andrea Cambiaso, ambaye anahusishwa pia na vilabu vya Chelsea na Barcelona. (Calciomercato)

    Mshambuliaji wa Serbia, Dusan Vlahovic ataondoka Juventus mwishoni mwa mwezi Juni baada ya kuamua kutosaini mkataba mpya na klabu hiyo ya Italia. (Football Italia)

    Juventus wameonyesha tena nia kumsajili mshambuliaji wa Crystal Palace na timu ya taifa ya Ufaransa, Jean-Philippe Mateta. (Gazzetta dello Sport)

  3. Zelensky apendekeza mazungumzo ya ana kwa ana na Putin ili kumaliza vita vya Ukraine

    Z

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Rais wa Ukraine, Volodymyr Zelensky, ametoa wito wa kufanyika kwa mazungumzo ya ana kwa ana kati yake na Rais wa Urusi, Vladimir Putin, katika juhudi mpya za kutafuta suluhisho la kumaliza vita vinavyoendelea kati ya nchi hizo mbili.

    Kupitia barua ya wazi aliyomwandikia Putin, Zelensky alisema kuwa ni muhimu viongozi hao wawili kukutana moja kwa moja ili kujadili njia za kurejesha amani.

    Katika barua hiyo yenye zaidi ya maneno 1,800, Zelensky alisisitiza kwamba amani ya kudumu inaweza kupatikana tu kupitia mazungumzo ya moja kwa moja kati ya Ukraine na Urusi. Aliongeza kuwa haitakuwa sahihi kusubiri hadi Marekani irejee kuipa kipaumbele vita vya Ulaya baada ya kuelekeza nguvu zake kwenye migogoro mingine ya kimataifa, ikiwemo suala la Iran.

    Zelensky pia alipendekeza kusitishwa kwa mapigano kwa kipindi chote cha mazungumzo hayo ili kutoa mazingira mazuri ya kufikia makubaliano. Hata hivyo, Putin awali alikataa wazo la kusitisha mapigano kwa muda, akisisitiza kuwa bado kuna masuala muhimu yanayohitaji kujadiliwa kabla ya kufikiwa kwa makubaliano yoyote.

    Serikali ya Urusi imethibitisha kupokea barua hiyo na kusema kwamba rais wa Urusi atapewa taarifa kamili kuhusu yaliyomo kabla ya kutoa msimamo rasmi.

    Rais wa Marekani, Donald Trump, pia alitoa maoni yake kuhusu pendekezo hilo, akisema kuwa itakuwa jambo jema ikiwa viongozi hao wawili watakutana uso kwa uso. Wakati huo huo, Zelensky alipendekeza kwamba mazungumzo hayo yaweze kufanyika katika nchi isiyoegemea upande wowote kama Switzerland au Turkey.

    Vita kati ya Urusi na Ukraine vilianza kwa uvamizi mkubwa wa Urusi mwezi Februari mwaka 2022 na vimesababisha maelfu ya vifo pamoja na uharibifu mkubwa wa miundombinu. Licha ya majaribio kadhaa ya mazungumzo yaliyofanyika katika maeneo mbalimbali, juhudi za kufikia usitishaji wa mapigano zimekuwa zikikwama. Pendekezo hili jipya la Zelensky linaonekana kuwa hatua nyingine muhimu katika kutafuta njia ya kumaliza mzozo huo wa muda mrefu.

  4. Karibu katika habari zetu za moja kwa moja leo Juni 5, 2026