Mapigano makali Yemen: Pakistan yasema "itafanya kila iwezalo" kuilinda Saudi Arabia

Msemaji wa jeshi la Pakistan amesema nchi yake "itafanya kila iwezalo" kuilinda Saudi Arabia.

Muhtasari

Moja kwa moja

Abdalla Seif Dzungu

  1. Mapigano makali Yemen: Pakistan yasema "itafanya kila iwezalo" kuilinda Saudi Arabia

    Maandamano yamezuka katika jiji la Karachi nchini Pakistan kufuatia taarifa za shambulio dhidi ya Mecca tarehe 18 Septemba 2026.

    Chanzo cha picha, AFP via Getty Images

    Msemaji wa jeshi la Pakistan amesema nchi yake "itafanya kila iwezalo" kuilinda Saudi Arabia, wakati ufalme huo ukikabiliwa na ongezeko la mashambulizi kutoka kwa kundi la Ansar Allah la Houthi nchini Yemen.

    Houthi wamesema wiki hii kwamba maeneo wanayodhibiti nchini Yemen yameshambuliwa tena kwa ndege za kivita za Saudi Arabia, huku Riyadh ikiwatuhumu kwa kujaribu kulenga mji mtakatifu wa Mecca kwa kutumia droni.

    Msemaji wa jeshi la Pakistan, Ahmed Sharif Chaudhry, alisema katika mahojiano na Arab News yaliyochapishwa Alhamisi: "Tutakwenda mbali zaidi katika kuhakikisha usalama wa Misikiti Miwili Mitakatifu na Ufalme wa Saudi Arabia."

    Chaudhry aliongeza: "Pakistan iko imara upande wa Saudi Arabia, kidiplomasia na kijeshi."

    Mwezi uliopita, Pakistan, Saudi Arabia na Uturuki zilitia saini makubaliano yanayojulikana kama "Mkataba wa Mecca wa Ulinzi wa Pamoja", ambao unazitaka nchi hizo tatu kuzingatia kanuni ya ulinzi wa pamoja endapo moja kati yao itashambuliwa.

    Hata hivyo, makubaliano hayo hayamaanishi kwamba nchi yoyote kati ya hizo tatu itaingia moja kwa moja katika vita vyovyote vitakavyoanzishwa na mojawapo ya nchi wanachama.

    Unaweza kusoma;

  2. Mashambulizi ya mseto ya Urusi dhidi ya Ulaya yanaongezeka, asema Macron

    Emmanuel Macron

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron ameonya kwamba tishio la mashambulizi ya mseto kutoka kwa Urusi dhidi ya Ulaya na Ufaransa limeongezeka.

    Katika mkutano na waandishi wa habari katika Ikulu ya Élysée, Macron amesema ameitaka serikali ya Ufaransa kuandaa mpango wa kulinda miundombinu muhimu na maeneo ya sekta ya ulinzi dhidi ya tishio hilo.

    Amesema Ufaransa imekuwa ikilengwa na mashambulizi ya mseto ya Urusi katika wiki za hivi karibuni, ambayo hayataachwa "bila jibu".

    Idadi inayoongezeka ya viongozi wa Ulaya imeonya kwamba huenda Urusi inajiandaa kufanya mashambulizi ili kupima dhamira yao ya kuendelea kuunga mkono Ukraine.

    Rais huyo wa Ufaransa alikuwa akizungumza na waandishi wa habari baada ya kukutana na viongozi wa vyama vya kisiasa kujadili athari za kiusalama za vita vinavyoendelea Mashariki ya Kati na Ukraine.

    "Katika wiki za hivi karibuni, tishio la mashambulizi ya mseto kutoka Urusi dhidi ya Wazungu na dhidi ya Ufaransa limeongezeka," alisema.

    "Lengo ni kututisha na kuvuruga juhudi zetu za kuendelea kuiunga mkono Ukraine. Matokeo yatakuwa kinyume kabisa. Hatujatishwa kwa sababu tunajua kwamba usalama wetu wa leo na kesho uko hatarini nchini Ukraine."

  3. Othman Masoud Othman ateuliwa kuwa Makamu wa kwanza wa rais wa Zanzibar

    Othman Masoud Othman

    Chanzo cha picha, ACT

    Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Mwinyi amemteua tena Othman Masoud Othman kuwa Makamu wa kwanza wa rais wa Zanzibar.

    Makamu wa Kwanza wa rais ataapishwa siku ya Jumanne tarehe 22 September.

    Othman Masoud ni mwanasheria mwenye taaluma ya juu na uzoefu mpana serikalini. Kabla ya kuingia rasmi katika siasa za upinzani, aliwahi kuwa Mkurugenzi mkuu wa mashtaka (2002–2011) na baadaye mwanasheria mkuu wa Serikali wa Zanzibar.

    Hapo awali hakujitokeza sana kwenye medani ya urais kutokana na kivuli kikubwa cha kisiasa cha Maalim Seif, alama kuu ya upinzani Zanzibar kwa zaidi ya robo karne. Lakini baada ya kifo cha Maalim Seif mwaka 2021, ACT-Wazalendo ilimteua Masoud kuziba nafasi yake na kuwa makamu wa kwanza wa rais katika serikali ya umoja wa kitaifa

  4. Watu watatu wauawa na wengine wanane kujeruhiwa katika ufyatuaji risasi shuleni Ufilipino

    wahudumu wa dharura

    Chanzo cha picha, Philippine Red Cross/Facebook

    Mtu aliyekuwa na silaha mwenye umri wa miaka 16 amewapiga risasi na kuwaua wanafunzi wawili na kuwajeruhi wengine wanane katika shule ya sekondari nchini Ufilipino, kabla ya kuripotiwa kujitoa uhai.

    Waathiriwa wawili waliofariki walikuwa wanafunzi wenye umri wa miaka 14 katika shule iliyoko Banga, katika mkoa wa kusini wa Mindanao, meya wa eneo hilo ameiambia BBC.

    Albert Palencia amesema wanne kati ya waliojeruhiwa wako katika hali mahututi.

    Idara ya Elimu imesema katika taarifa kwamba "imehuzunishwa sana" na tukio hilo lililoripotiwa kutokea Ijumaa alasiri katika Shule ya Sekondari ya Kitaifa ya Banga.

    Hili ni tukio la tatu la ufyatuaji risasi shuleni nchini Ufilipino lililosababisha vifo tangu Juni mwaka huu.

    "Jambo letu la kwanza ni kuhakikisha usalama na ustawi wa wanafunzi, walimu na wafanyakazi wa shule," Idara ya Elimu ilisema, na kuongeza kuwa inashirikiana na mamlaka kuthibitisha tukio hilo na kutoa msaada unaohitajika.

    "Tunawahimiza wote kubaki watulivu na kujiepusha na kusambaza taarifa ambazo hazijathibitishwa huku mamlaka zikiendelea na uchunguzi."

    Palencia aliliambia shirika la habari la Reuters kwamba wakati wa mazungumzo ya chakula cha mchana Ijumaa, mshambuliaji huyo aliwahimiza marafiki zake waende nyumbani "kwa sababu baada ya chakula cha mchana, angekuwa akitekeleza mpango wake".

  5. Muogeleaji auawa katika shambulio la papa Australia

    Msako wa polisi unaendelea kumtafuta mtu aliyepotea katika ufukwe wa Sorrento mjini Perth baada ya shambulio linalodhaniwa kufanywa na papa.

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Polisi wamesema muogeleaji ameuawa katika shambulio la papa kwenye ufukwe mjini Perth, pwani ya magharibi ya Australia.

    Huduma za dharura ziliitwa katika eneo la "tukio linalohusisha papa" katika ufukwe wa Sorrento Beach saa 10:15 hivi kwa saa za eneo siku ya Ijumaa.

    Polisi wamesema msako mkubwa ulifanywa katika eneo hilo na mamlaka kwa kutumia helikopta na boti, lakini hawakusema ikiwa mwili wa mwathiriwa umepatikana.

    Shahidi mmoja alieleza kuona mwanaume akivutwa chini ya maji na papa, umbali wa takribani mita 50 kutoka ufukweni, huku mwingine akisema aliona "dimbwi la damu" majini, kwa mujibu wa vyombo vya habari vya eneo hilo.

    Shuhuda mmoja aliiambia WAtoday kwamba alimwona mwanaume huyo "akishambuliwa vikali" huku papa huyo "akimrusha huku na huko kama samaki".

    "Mimi ni muuguzi, kwa hiyo bila shaka huwa naona mambo mengi ya kutisha, lakini kumuona mtu akiuawa kwa kushambuliwa vikali majini mbele yangu ni jambo ambalo ni vigumu sana kulishuhudia," aliiambia WAtoday.

    "Ninaishi umbali mfupi tu kutoka hapa, na mimi huogelea kila siku. Kwa kweli, hakuna namna nitakavyoweza kuingia tena majini."

    Shahidi mwingine alisema alikuwa akitembea ufukweni na rafiki yake wakati shambulio hilo lilipotokea.

  6. Rais wa Korea Kusini: Hatutaingilia vita na Iran

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Maelezo ya picha, Rais wa Kosea Kusini

    Rais wa Korea Kusini, Lee Jae-myung, amesema hatawahi kamwe kuamuru kutumwa kwa vikosi vya jeshi la nchi yake kushiriki katika mzozo wa kigeni.

    Wiki iliyopita, Seoul ilikanusha ripoti kwamba jeshi lake la majini lilikuwa likijiandaa kushiriki katika operesheni za kulinda uhuru wa usafiri wa meli za kibiashara katika Ghuba ya Uajemi na Lango la Hormuz.

    Kauli hii inaweza pia kuwa imetolewa katika muktadha wa msimamo wake kuhusu uwezekano wa mzozo kati ya China na Taiwan na nafasi ya Korea Kusini katika hali hiyo.

    Katika mahojiano mwishoni mwa mwezi uliopita, Donald Trump alilalamika kuwa amepata "msaada mdogo sana" kutoka kwa nchi nyingine akitoa mfano wa Korea Kusini kama mmoja wa washirika wakuu wa Marekani barani Asia.

    Wiki mbili zilizopita, msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran, Esmail Baghaei, aliionya Korea Kusini akisema, "Ushiriki wowote wa kiutendaji au uwepo wa kijeshi wa pande nyingine katika Ghuba ya Uajemi na Lango la Hormuz ni sawa na kuunga mkono moja kwa moja upande unaoanzisha uchokozi, na hatua hiyo itakuwa na matokeo mabaya."

    Katika sehemu nyingine ya hotuba yake, Rais wa Korea Kusini alisema, "Ni wazi kuwa Trump anataka mazungumzo, na mimi pia namtaka Rais Trump kuanzisha mazungumzo."

    Hivi karibuni, kupunguzwa kwa ukubwa wa mazoezi ya kijeshi ya kila mwaka kati ya Marekani na Korea Kusini, pamoja na juhudi za Donald Trump za kurejesha mazungumzo na Pyongyang, kumezua wasiwasi kuhusu uwezekano wa Seoul kuachwa nje ya mazungumzo yanayohusu mpango wa nyuklia wa Korea Kaskazini.

    Donald Trump ameyataja mazoezi hayo ya kijeshi ya kila mwaka kati ya Marekani na Korea Kusini kuwa ya gharama kubwa, akiongeza kuwa yanaathiri vibaya "uhusiano wake mzuri sana" na kiongozi wa Korea Kaskazini, Kim Jong-un.

  7. Charles 'alionekana mwenye furaha iliyopitiliza' baada ya Diana kufariki, Earl Spencer adai

    .

    Chanzo cha picha, PA Media

    Maelezo ya picha, Bintimfalme Diana

    Earl Spencer, kaka yake Diana, Bintimfalme wa Wales, amedai kuwa Mfalme Charles "alisikika akiwa na furaha iliyopitiliza" alipompigia simu baada ya kifo chake mwaka 1997.

    Katika kitabu chenye utata kuhusu Diana, alidai kuwa Prince Charles wa wakati huo alisikika kama "mshindi wa bahati nasibu" baada ya kupata habari hizo.

    Jumba la Buckingham lilikana vikali siku ya Jumatano uhalali wa kitabu hicho baada ya dondoo ya awali kudai kuwa Charles alinukuliwa akisema kuhusu Diana: "Tutamsahau hivi karibuni."

    Msemaji alisema: "Ingawa kwa kawaida hatutoi maoni kuhusu vitabu, Mfalme anatambua kuwa uchungu wa kuondokewa na ndugu unaweza kutia ukungu katika mantiki, kuathiri maamuzi na kubadilisha jinsi matukio yanavyokumbukwa kwa namna ambazo wengine hawawezi kuzielewa, hata miaka mingi baada ya kupoteza mtu wa namna hiyo."

    Madai hayo ya hivi karibuni tena yanajikita katika mashambulizi ya kibinafsi dhidi ya Mfalme Charles na familia ya kifalme, yakitafsiri nia zao kwa mtazamo mkali sana.

    Ushahidi uliopo ni kumbukumbu binafsi ya Earl Spencer kuhusu mazungumzo yaliyofanyika katika kipindi hicho cha hisia nzito kufuatia kifo cha dada yake, takriban miaka 30 iliyopita.

    Kinachosubiriwa kuonekana ni jinsi umma utakavyopokea madai hayo; iwapo wataunga mkono kitabu hiki kama mtazamo mpya na tofauti kutoka kwa Spencer, au iwapo wataona kuwa si jambo sahihi kuweka wazi migogoro ya aina hiyo ya kibinafsi.

    Wawakilishi wa Prince Harry wamesema hawataki kutoa maoni kuhusu kitabu hicho, na kasri la Buckingham limerejelea majibu yake ya siku ya Jumatano, ambapo lilikanusha maelezo hayo kuhusu Prince Charles kufuatia kifo cha Diana jijini Paris.

  8. Kila Mnigeria sasa ni tajiri wa mafuta

    .

    Chanzo cha picha, Bloomberg via Getty Images

    Maelezo ya picha, Bilionea wa Nigeria Aliko Dangote

    Angalau hivyo ndivyo picha na jumbe za vichekesho (memes) kwenye mitandao ya kijamii zinavyotaka uamini, huku hamu ya kuwekeza ikishika kasi nchini humo.

    Wanigeria wamekuwa na shauku kubwa ya kumiliki sehemu ya biashara ya nishati iliyoanzishwa na mtu tajiri zaidi nchini humo – na barani Afrika – Aliko Dangote.

    Zaidi ya hisa bilioni nne za kiwanda chake kikubwa cha kusafisha mafuta zinazowakilisha zaidi ya asilimia 3 ya kampuni hiyo ziliingizwa sokoni siku ya Jumatatu katika mauzo makubwa zaidi ya aina yake kuwahi kushuhudiwa barani Afrika.

    Kiwango cha chini cha ununuzi kilikuwa hisa 10 kwa takriban dola 4 (pauni 3), na ingawa hii inawakilisha sehemu ndogo sana ya kampuni, wengi sasa wanasherehekea na kufanya mzaha kuhusu hadhi yao mpya ya kuwa wamiliki (wa sehemu) ya kampuni hiyo.

    Video moja maarufu kwenye mitandao ya kijamii inamuonyesha Mnigeria akisimulia jinsi alivyomsimamisha dereva wa lori la kampuni ya Dangote aliyekuwa akiendesha kwa kasi, na kumwonya dhidi ya kutumia mali ya kampuni hiyo bila uangalifu.

    Picha nyingine za vichekesho zinawaonyesha wawekezaji wakijaribu kumpigia simu Dangote ili kujadili masuala ya kibiashara.

    Na neno "Yangote" neno la kuchezea lugha ya Kihausa lenye maana ya "sote tuna hisa sasa" limekuwa likivuma sana kwenye mitandao ya kijamii.

  9. Watu 2 wafariki dunia baada ya lori la mafuta kulipuka kwenye barabara kuu ya Eldoret-Webuye Kenya

    .

    Chanzo cha picha, Liberia National Red Cross Society/Facebook

    Watu wawili wamethibitishwa kufariki dunia huku wengine 14 wakijeruhiwa kufuatia mlipuko wa lori la kubeba mafuta kwenye barabara ya Eldoret-Turbo, nchini Kenya karibu na Shule ya Sekondari ya Paul Boit, usiku wa Alhamisi.

    Wawili hao wanahisiwa kufariki walipojaribu kuchota mafuta kutoka kwenye lori hilo baada ya ajali kutokea.

    Shirika la Msalaba Mwekundu la Kenya lilisema Alhamisi kuwa tukio hilo lilihitaji mwitikio wa kushughulikia majeruhi wengi eneo hilo.

    "Shirika la Red Cross Kenya lipo eneo la tukio likitoa huduma kwa kushirikiana na Polisi wa Kenya pamoja na wazima-moto," shirika hilo lilisema katika ujumbe kwenye mtandao wa X mwendo wa saa nne na nusu usiku.

  10. Muungano wa kulinda katiba DRC wataka serikali kuwaachilia wafuasi wake waliokamatwa wakati wa maandamano

    Muungano wa Kulinda Utaratibu wa Kikatiba (C64) umesifu kile ulichokitaja kuwa ni mwitikio mkubwa wa wananchi katika maandamano yaliyofanyika kote Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo mnamo tarehe 15 Septemba, ukisema maandamano hayo yalionyesha kuungwa mkono kwa utawala wa kikatiba, demokrasia na uhuru wa raia.

    Katika taarifa iliyotolewa tarehe 17 Septemba, C64 ililaani kifo cha mwanachama wa ADDCONGO, Manassé Lomboto Bomengola, wakati wa maandamano hayo jijini Kinshasa.

    Muungano huo ulidai kuwa makundi yanayounga mkono serikali na baadhi ya maafisa wa vyombo vya usalama walihusika.

    Pia uliripoti majeraha, ukamataji wa watu na uharibifu wa mali wakati wa maandamano hayo, na kutaka kufanyika kwa uchunguzi huru ili kubaini waliohusika.

    Muungano huo wa upinzani ulidai kuachiwa huru kwa watu waliokamatwa wakati wa maandamano na kuzitaka mamlaka kuwafikisha mahakamani waliohusika na madai ya ukiukwaji wa haki za binadamu.

    Pia ulisisitiza tena wito wa kuvunjwa kwa kundi la vijana linalojulikana kama Force du Progrès.

    C64 ilikosoa zaidi kile ilichokiita vikwazo dhidi ya uhuru wa kukusanyika katika miji kadhaa.

    Huku ukisisitiza upinzani wake dhidi ya marekebisho yoyote ya katiba, muungano huo ulirudia kaulimbiu zake za "Hapana kwa kubadilisha Katiba" na "Hapana kwa muhula wa tatu", ukisisitiza kuwa kanuni ya kidemokrasia ya kubadilishana madaraka lazima iheshimiwe kabla ya uchaguzi wa mwaka 2028.

    C64 ilisema itaendeleza kampeni yake ya kulinda utaratibu wa kikatiba na uhuru wa wananchi.

    Hata hivyo, mamlaka za mkoa zilitoa maelezo tofauti kuhusu matukio hayo.

    Katika taarifa iliyochapishwa na shirika la habari la serikali la ACP, Waziri wa Mambo ya Ndani wa Mkoa wa Kinshasa, Jeannot Canon La Rose, alisema takwimu za awali zilionyesha kuwa hakuna vifo vilivyorekodiwa.

    "Takwimu za awali katika hatua hii zinaonyesha hakuna vifo, majeraha machache kwa pande zote mbili — akiwemo Kamishna wa Polisi wa Mkoa — na takriban watu ishirini waliokamatwa kuhusiana na maandamano hayo," alisema Bw. Canon.

    Maelezo hayo yanayotofautiana yanaangazia migogoro kati ya upinzani na mamlaka kuhusu jinsi maandamano hayo yalivyoendeshwa na matokeo yake.

  11. Tetesi: Arsenal inamtaka kinda wa Bournemouth Eli Junior Kroupi

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Maelezo ya picha, Eli Junior Kroupi

    Arsenal ina nia kubwa ya kumsajili mshambuliaji wa Bournemouth na timu ya taifa ya Ufaransa ya vijana chini ya umri wa miaka 21, Eli Junior Kroupi (20), lakini klabu hiyo ya Bournemouth (inayofahamika kama 'Cherries') inatarajia ada kubwa. (Football London)

    Real Madrid inafikiria uwezekano wa kumsajili beki wa England mwenye umri wa miaka 24 wa Everton, Jarrad Branthwaite, ambaye pia anafuatiliwa na klabu kadhaa za Ligi Kuu ya England. (Goal)

    Chelsea ina nia ya kuchunguza dili la pauni milioni 69 kwa ajili ya winga wa Uhispania na Athletic Bilbao, Nico Williams (24). (Fichajes – In Spanish)

    Arsenal haina mpango wowote wa kumuuza kiungo wa Uhispania mwenye umri wa miaka 27, Martin Zubimendi, mwezi Januari. (Football Insider)

    Real Madrid na Barcelona zimefanya uchunguzi mpya kuhusu kinda wa Marekani Cavan Sullivan (16), ambaye anatarajiwa kujiunga na Manchester City akitokea Philadelphia Union atakapofikisha umri wa miaka 18. (Teamtalk)

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Maelezo ya picha, Rayan

    Liverpool italazimika kulipa ada kamili ya kuvunja mkataba ya pauni milioni 130 ili kumsajili mchezaji wa Brazil mwenye umri wa miaka 20, Rayan, kutoka Bournemouth, licha ya uhusiano wa meneja Andoni Iraola na kiungo huyo tangu alipokuwa kocha wa Bournemouth. (ESPN Brazil via Caught Offside)

    Kiungo wa Atletico Madrid na Argentina, Julian Alvarez (26) - ambaye anawaniwa na klabu kama Arsenal na Barcelona - anafikiria kuachana na wakala wake wa muda mrefu kufuatia kipindi cha majira ya joto kilichojaa tetesi za uhamisho. (Mundo Deportivo)

    Everton ina uwezekano mdogo wa kumfuatilia mshambuliaji wa Tottenham na Brazil, Richarlison, licha ya mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 29 kuhusishwa na uwezekano wa kurejea Everton wakati wa majira ya joto. (Football Insider)

  12. Polisi wa Nigeria wanachunguza vifo vya watu 37 waliokuwa wakishikiliwa kwa tuhuma za uchimbaji haramu wa madini

    .

    Chanzo cha picha, AFP via Getty Images

    Watu thelathini na saba walioshutumiwa kwa uchimbaji madini haramu kaskazini-magharibi mwa Nigeria wamefariki wakiwa kizuizini, maafisa wa eneo hilo wanasema.

    Polisi wameanzisha uchunguzi kuhusu vifo hivyo, ambavyo Kikosi cha Usalama na Ulinzi wa Raia cha Nigeria (NSCDC) kililaumu mlipuko wa ugonjwa.

    Hata hivyo, ripoti ya kijasusi iliyoshirikiwa na shirika la habari la AFP ilionyesha kuwa kundi hilo lilifariki kutokana na msongamano na uingizaji hewa hafifu ndani ya kituo cha kizuizi katika jimbo la Niger la Nigeria.

    Gavana wa jimbo hilo Mohammed Umaru Bago aliviita vifo hivyo "vya kusikitisha" wakati wa mkutano na waandishi wa habari siku ya Alhamisi.

    Kamanda wa NSCDC amekamatwa kufuatia vifo hivyo, Bago pia alisema.

    Alitangaza siku tatu za maombolezo na kuahirisha kuanza kwa kampeni za uchaguzi zilizopangwa kufanyika Januari.

    Maafisa walikuwa wamelikamata kundi hilo la vijana siku ya Jumanne kwa tuhuma za uchimbaji madini haramu karibu na Borgu, katika jimbo lenye utajiri wa madini la Niger. Eneo hilo linajulikana kwa uchimbaji mdogo wa dhahabu.

    Siku mbili baadaye, watu thelathini na saba waliokamatwa kama sehemu ya operesheni inayoshukiwa kuwa haramu walipatikana wamekufa ndani ya kituo cha kizuizi kinachoendeshwa na NSCDC.

  13. Axios: Trump kufanya uamuzi mkubwa wa kuingia vitani na Iran

    .

    Chanzo cha picha, REU

    Maelezo ya picha, Trump

    Jarida la Axios limemnukuu mwandishi wake, Barack Ravid, akisema kuwa Rais wa Marekani Donald Trump anasema yuko karibu kufanya uamuzi mzito kuhusu kuanzisha upya mashambulizi makubwa dhidi ya Iran.

    Kulingana na Axios, Donald Trump alisema katika mazungumzo ya simu na Bw. Ravid: "Nina uamuzi mkubwa mbele yangu. Je, nichukue hatua na kuwaangamiza [serikali ya Iran] au la? Ni uamuzi mkubwa. Chaguzi zote zipo mezani."

    Kauli hizi zinakuja wakati Rais wa Marekani akitarajiwa kukutana na viongozi wa Saudi Arabia, Falme za Kiarabu (UAE), Qatar, Bahrain, Kuwait, na Oman siku ya Jumanne, pembezoni mwa Mkutano Mkuu wa Umoja wa Mataifa jijini New York; mkutano unaotarajiwa kujikita katika mustakabali wa mzozo na Iran.

    Bw. Trump anasema ana mpango wa kutumia mkutano huo kutathmini misimamo ya mataifa ya Ghuba kabla ya kuamua hatua zake zinazofuata.

    Alimwambia Barak Ravid: "Nataka kujua hali yao (nchi za Ghuba) ikoje. Siku zote tumekuwa tukiwaunga mkono na kuwalinda."

    Wakati huo huo, ripoti zinaonyesha kuwa Waziri wa Ulinzi wa Marekani, Pete Hegseth, ameviagiza vikosi vya Marekani katika Mashariki ya Kati kujiandaa kikamilifu kwa uwezekano wa kurejea kwenye mapigano makali kabla ya mwisho wa mwaka.

    Alipoulizwa ikiwa ana mpango wa kukutana na Waziri Mkuu wa Israel, Benjamin Netanyahu, jijini New York wiki ijayo, Bw. Trump alisema: "Huenda."

  14. Mshauri wa Mojtaba: Mlango-bahari wa Hormuz hautafunguliwa hadi Trump atakapoondolewa madarakani

    ..

    Chanzo cha picha, Reuters

    Maelezo ya picha, Vita nchini Yemen na kusonga mbele kwa Wahouthi katika maeneo ya pwani yanayotawala Mlango-bahari wa Bab al-Mandab vimebadilisha sura ya mzozo katika Ghuba ya Uajemi

    Mohammad Baqer Zolghadr, mshauri wa kisiasa wa Mojtaba Khamenei, kiongozi mpya wa Jamhuri ya Kiislamu, amesema kuwa nchi yake haina nia ya kufungua Mlango-bahari wa Hormuz mradi tu Donald Trump aendelee kuwa madarakani.

    Katika taarifa iliyochapishwa na mashirika ya habari nchini Iran siku ya Alhamisi, Bw. Zolqadr alisema: "Taifa hili limeazimia kuvunja pembe ya adui mchokozi na kuvunja migongo ya wenye kiburi."

    Aliendelea kusema kuwa Mlango-bahari wa Hormuz hautafunguliwa hadi pale Donald Trump na Benjamin Netanyahu watakapong'olewa kutoka "kiti cha madaraka," na kwamba hii ni "hatua ya kwanza ya kulipiza kisasi kwa taifa la Iran."

    Sambamba na kauli nyingi na wakati mwingine zinazokinzana za Donald Trump kuhusu vita au mazungumzo na Iran, kuna mgawanyiko mkubwa wa maoni ndani ya nchi hiyo kuhusu iwapo waendelee na makabiliano ya kijeshi au wafanye mazungumzo na Marekani.

    Wakati kundi la maafisa wa ngazi ya juu wa kisiasa nchini humo, kama vile Massoud Pezhikian na Mohammad Bagher Qalibaf, likitaka Marekani irejee kwenye masharti ya Mkataba wa Maelewano wa Islamabad na kuliona hilo kama sharti la kusitisha vita, watu wenye msimamo mkali akiwemo makamanda wa Walinzi wa Mapinduzi wanazungumzia kuendeleza vita na kuuweka Mlango-bahari wa Hormuz ukiwa umefungwa kama suluhisho madhubuti zaidi la kukabiliana na Marekani na Israel.

    Wakati huo huo, kupanda kwa kasi kwa mfumuko wa bei, vikwazo vya kiuchumi, na kuzingirwa kwa bandari za kusini mwa Iran kwa njia ya maji kumeifanya hali ya maisha ya kila siku kwa raia wa nchi hiyo kuwa ngumu zaidi, huku kushuka kwa thamani ya sarafu ya Rial dhidi ya sarafu za kimataifa kukiongeza shinikizo zaidi kwenye hali ya maisha ya kila siku.

  15. UN yasema kuna ushahidi kuwa Marekani ilifanya uhalifu wa kivita katika mashambulizi dhidi ya Iran

    .

    Chanzo cha picha, WANA via Reuters

    Wataalamu wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa wanasema kuna sababu nzuri za kuamini kwamba Marekani ilitenda uhalifu wa kivita katika mashambulizi mawili nchini Iran yaliyoua raia wasiopungua 177.

    Ripoti mpya ya Ujumbe Huru wa Kimataifa wa Kutafuta Ukweli kuhusu Iran ilisema mashambulizi ya kombora ya Februari kwenye shule ya msingi huko Minab na uwanja wa michezo huko Lamerd yalikuwa mashambulizi yasiyo ya kuchagua na kusababisha vifo vya raia na uharibifu wa miundombinu ya raia.

    Hapo awali Marekani ilikanusha kushambulia Lamerd na kusema ilikuwa ikichunguza kilichotokea Minab. Afisa wa Wizara ya Mambo ya Nje alisema Marekani haikutoa uaminifu kwa matokeo katika ripoti hiyo.

    Wataalamu hao pia waligundua kuwa mamlaka ya Iran ilifanya uhalifu dhidi ya binadamu wakati wa msako dhidi ya maandamano makubwa ya kupinga serikali mwezi Januari.

    Walisema mauaji yaliyofanywa na vikosi vya usalama yalitokea kwa "kiwango cha kushangaza na kisicho cha kawaida" katika majimbo yote 31.

    Iran pia haijatoa maoni kuhusu matokeo hayo, lakini hapo awali imekataa madai ya ukiukwaji wa kimfumo wa haki za binadamu.

  16. Natumahi hujambo na karibu katika habari zetu za moja kwa moja