Rais wa zamani wa Kosovo ahukumiwa miaka 25 jela

Thaçi mwenye umri wa miaka 58 alikutwa na hatia ya kuhusika na mauaji ya wapinzani 96 wa kisiasa, pamoja na kutesa mamia ya watu waliotuhumiwa kushirikiana na Waserbia.

Ruka Video uendelee
  • xx
  • Besigye
  • .
  • xx
  • xx
  • xx
  • Lungu
  • xx
  • xx
  • d
  • s
  • a
  • Sonko
  • xx
  • xx
  • xx
  • xx
  • xx
  • Dangote

Moja kwa moja

Na Ambia Hirsi & Abdalla Seif Dzungu

  1. Rais wa zamani wa Kosovo ahukumiwa miaka 25 jela

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Maelezo ya picha, Aliyekuwa Rais wa Kosovo, Hashim Thaci (kushoto), ameketi mahakamani karibu na aliyekuwa kiongozi wa KLA, Rexhep Selimi (nyuma), huku akihudhuria kwenye kesi yake akikabiliwa na mashtaka ya uhalifu wa kivita mbele ya Mahakama Maalum ya Kosovo mjini The Hague

    Aliyekuwa Rais wa Kosovo Hashim Thaçi amehukumiwa kifungo cha miaka 25 jela kwa uhalifu wa kivita.

    Thaçi aliongoza Jeshi la Ukombozi wa Kosovo (KLA) wakati wa harakati za Kosovo za kujitenga na Serbia.

    Mahakama hiyo pia ilimhukumu Yakup Krasniqi, aliyekuwa kiongozi wa KLA aliyeshtakiwa pamoja na Thaçi, kifungo cha miaka 25 jela.

    Kadri Veseli amehukumiwa miaka 18, huku Recep Selimi akihukumiwa miaka 13 jela.

    Mahakama Maalum ya Kosovo mjini The Hague imesema Thaçi, ambaye upande wa mashtaka uliomba ahukumiwe kifungo cha miaka 45, anawajibika kwa uhalifu wa kivita uliofanyika Kosovo katika miaka ya 1990, ukiwemo mauaji, mateso na kuwazuilia watu kinyume cha sheria.

    Mahakama hiyo imeamua kumhukumu miaka 25 jela.

    Thaçi mwenye umri wa miaka 58 alikutwa na hatia ya kuhusika na mauaji ya wapinzani 96 wa kisiasa, pamoja na mateso na kutendewa vibaya kwa mamia ya watu waliotuhumiwa kushirikiana na Waserbia.

    Thaçi alisikiliza hukumu hiyo akiwa amesimama. Hapo awali alikuwa amekanusha mashtaka dhidi yake.

    Kabla ya kusomwa kwa hukumu hiyo mjini The Hague, Uholanzi, idadi kubwa ya Waalbania wa Kosovo waliandamana kuonyesha kumuunga mkono Thaçi na wenzake.

    Wafuasi wake walionekana kusikitishwa na hukumu hiyo.

  2. Houthis wazungumzia kwa mara ya kwanza kuhusu kuishambulia Makka

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Saudi Arabia imesema imeidungua droni ya waasi wa Houthi wa Yemen kabla haijaingia eneo la Makka, na kuzuia shambulio. Msemaji wa muungano unaoongozwa na Saudi Arabia amesema hii ni mara ya pili kwa Houthis kuishambulia Makka, baada ya shambulio la kombora mwaka 2017.

    Hata hivyo, msemaji wa kijeshi wa Houthis, Yahya Saree, amekanusha kuishambulia Makka au maeneo mengine matakatifu ya Waislamu, akisema mashambulizi yao yalilenga vituo vya gesi na kambi za kijeshi.

    Wakati huo huo, Houthis wamedai kuidungua ndege ya kivita ya Saudi Arabia aina ya F-15 katika eneo la Ma'rib, Yemen. BBC haijaweza kuthibitisha kwa uhuru madai hayo wala uhalisia wa video zinazosambaa mitandaoni kuhusu tukio la Makka.

    Mamlaka za Saudi Arabia ziliwaonya wakazi wa Makka, Jeddah na Taif kuwa makini kutokana na tishio la mashambulizi, na kuwaelekeza kufuata maelekezo ya usalama na kukaa ndani iwapo kutatolewa tahadhari.

    Baadaye, Mamlaka ya Ulinzi wa Raia ya Saudi Arabia ilisema hakuna tena hatari, huku ikiwataka wananchi kufuata taarifa kutoka vyanzo rasmi.

  3. Muigizaji nguli wa Nigeria Olu Jacobs afariki dunia akiwa na umri wa miaka 84

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Olu Jacobs, mmoja wa waigizaji maarufu zaidi nchini Nigeria, ambaye taaluma yake ilidumu kwa miongo kadhaa katika nyanja za ukumbi wa michezo, televisheni na filamu, amefariki dunia akiwa na umri wa miaka 84.

    Mkewe, mwigizaji mkongwe Joke Silva, alitangaza kifo chake na kuomba faragha wakati familia ikiwa katika kipindi cha maombolezo.

    Silva alitangaza kifo hicho katika taarifa iliyomwelezea mwigizaji huyo mashuhuri kama "Simba wa Lufodo" na kusema kuwa aliishi maisha yenye mafanikio na mapambano ya dhati.

    Baadhi ya filamu zake mashuhuri ni pamoja na*My Kingdom, Covert Operation* na One Fine Day.

    Alichukuliwa kuwa mmoja wa waanzilishi na nguzo muhimu za Nollywood kama tasnia ya filamu ya Nigeria inavyojulikana na alijipatia heshima na pongezi kubwa kote nchini.

    "Tunawaomba wanablogu wote na watu wenye ushawishi kwenye mitandao ya kijamii kuheshimu faragha ya familia yetu katika kipindi hiki," Silva alisema katika taarifa hiyo.

    Jacobs, aliyezaliwa tarehe 11 Julai 1942, alipata mafunzo katika chuo cha Royal Academy of Dramatic Art jijini London kabla ya kuanza taaluma iliyojumuisha kushiriki katika vipindi vya televisheni vya Uingereza na filamu za kimataifa.

    Baadaye, alikuja kuwa mmoja wa watu muhimu waliojenga tasnia ya filamu ya Nigeria, akishiriki katika kazi nyingi za ndani na kujipatia sifa kutokana na uwezo wake mkubwa wa kuigiza na uhodari wa kuigiza aina mbalimbali za wahusika.

  4. Afrika Kusini inasema Marekani ilipotosha kuhusu sera zake kufuatia vikwazo vya visa

    Wizara ya Mambo ya Nje ya Afrika Kusini ilisema siku ya Jumatano kuwa imebaini kwa wasiwasi vikwazo vya visa vya Marekani dhidi ya baadhi ya raia wa Afrika Kusini, vilivyotangazwa na Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, Marco Rubio, siku moja kabla.

    Wizara hiyo iliongeza katika taarifa yake kuwa tangazo hilo la Marekani linaendana na "upotoshaji wa sera za ndani za Afrika Kusini unaofanywa na makundi yenye misimamo mikali".

    "Tunasisitiza kuwa changamoto katika uhusiano wetu wa pande mbili na Marekani zinaweza kutatuliwa tu kupitia mazungumzo yenye tija kati ya maafisa wa serikali kutoka

  5. Tuko tayari kulinda haki halali za Iran - China

    .

    Chanzo cha picha, S_A_ARAGHACHI

    Waziri wa Mambo ya Nje wa China, Wang Yi, alisema siku ya Jumatano katika mazungumzo na mwenzake wa Iran, Abbas Araqchi, kwamba nchi yake iko tayari "kulinda" haki za Iran.

    Katika mkutano na Abbas Araqchi, ambaye anafanya ziara nchini China, Bw. Wang alisema mjini Beijing kuwa China "iko tayari kuimarisha mazungumzo na ushirikiano na Iran, na kulinda haki na maslahi halali ya Iran."

    Aliongeza: "Tunahimiza Iran na Marekani kutumia busara na kujizuia."

    Rais wa China, Xi Jinping, anatarajiwa kusafiri hadi Washington wiki ijayo kukutana na Rais wa Marekani, Donald Trump.

    Kwa mujibu wa shirika la habari la AFP, China ambayo ni mmoja wa washirika wakuu wa kiuchumi wa Iran imekuwa ikijitahidi kwa muda mrefu kupunguza mvutano wa mzozo wa Mashariki ya Kati unaoendelea kwa miezi kadhaa sasa; mzozo ambao pia umeenea hadi katika nchi jirani na Iran.

    "Hatutaki kuona mivutano ya kikanda ikienea hadi Yemen na Bahari Nyekundu," alisema Bw. Wang.

    Wiki hii, China ilikanusha taarifa katika vyombo vya habari vya Marekani zilizodai kuwa taasisi za China "zilipatia Jamhuri ya Kiislamu" picha za satelaiti za kambi ya kijeshi ambapo vikosi vya Marekani vimewekwa nchini Jordan.

    Wanajeshi watatu wa Marekani waliuawa katika shambulio hilo.

  6. 20 wafariki baada ya jengo la Gaza, lililokuwa limeharibiwa na vita, kuporomoka

    .

    Chanzo cha picha, Reuters

    Maelezo ya picha, Jengo la gaza lililoporomoka

    Takriban watu 20 wameuawa, wakiwemo watoto, na wengine kadhaa hawajulikani walipo baada ya jengo lililoharibiwa na vita kuporomoka katika Ukanda wa Gaza, kulingana na timu za uokoaji za eneo hilo.

    Picha za video zinaonyesha shughuli za kutafuta miili na manusura zikiendelea kwenye vifusi vya jengo hilo la ghorofa nyingi katika eneo la Tal al-Hawa jijini Gaza, ambapo sakafu zake zilikuwa zimebonyeana na kuangukiana.

    Wakazi walisema familia 10 zilikuwa zikiishi katika vyumba hivyo licha ya maonyo kwamba jengo hilo halikuwa salama.

    Wafanyakazi wa huduma ya uokoaji ya Ulinzi wa Raia inayoendeshwa na Hamas walisema kuwa mwanzoni walikuwa wakifanya kazi "bila zana zozote" kutokana na vikwazo vikali vya Israel dhidi ya vifaa vinavyoruhusiwa kuingizwa Gaza.

    Hata hivyo, baadaye waliweza kukopa mitambo mizito.

    Siku ya Jumanne, mashambulizi ya anga ya Israel huko Gaza yaliua angalau Wapalestina watano, wakiwemo watoto wawili na kamanda wa Hamas, kulingana na maafisa wa afya na vyanzo vya Hamas.

    Jeshi la Israel lilisema liliua kamanda wa Hamas kusini mwa Gaza na mpiganaji mwingine kaskazini. Katika matukio yote mawili, mtoto mmoja pia aliripotiwa kuuawa.

    Kando na hayo, shirika la hisani la Uingereza la Medical Aid for Palestinians lilisema kuwa mgonjwa mmoja aliuawa na ndege isiyo na rubani ya Israel katika kituo cha afya kinachosaidiwa na shirika hilo huko Jabalia, kaskazini mwa Gaza.

  7. J.D Vance: Mgogoro wa Marekani na Iran utaingia katika mkondo mpya katika miezi ijayo

    .

    Chanzo cha picha, EPA

    Maelezo ya picha, J.D Vance

    J.D. Vance, makamu wa rais wa Donald Trump, alisema katika mahojiano ya kipekee na gazeti la New York Post kwamba vita vya Marekani na Iran vitaingia katika "hatua tofauti sana" katika miezi ijayo.

    Bw. Vance anaunga mkono kauli za Donald Trump kwamba vita hivyo vitakwisha mara tu baada ya uchaguzi wa katikati ya muhula nchini Marekani.

    Katika mazungumzo yaliyofanyika ndani ya ndege siku ya Jumatatu, alisema kuwa Jamhuri ya Kiislamu bado "itapoteza udhibiti wa Lango la Hormuz" kufikia wakati wa uchaguzi.

    "Hatuwezi kutabiri wakati ujao, lakini nadhani rais yuko sahihi kwamba hali itakuwa tofauti sana katika miezi michache ijayo," alisema Bw. Vance.

    "Yeye (Donald Trump) pia ndiye Amiri Jeshi Mkuu; kwa hivyo yeye ndiye anayeamua... ni lini migogoro inapoanza na lini inapoisha."

    Makamu wa Rais wa Marekani pia aliongeza: "Ninaelewa vyema kwamba wananchi wa Marekani wanaanza kukosa subira, lakini kinachoendelea kwa sasa ni kwamba Marekani haijajihusisha na operesheni za mashambulizi; kwa kweli hatufanyi hivyo."

    Pia alisema: "Lakini kinachotokea ni kwamba wakati mwingine Wairani hufyatulia risasi meli za kibiashara, ingawa kwa kawaida hawafanikiwi."

    Rais wa Marekani Donald Trump amesema mara kadhaa kwamba vita na Iran vitakwisha baada ya uchaguzi wa katikati ya muhula nchini Marekani mwezi Novemba.

  8. Wahouthi: Tumetungua ndege ya kivita ya Saudia aina ya F-15

    .

    Chanzo cha picha, Dalibor Ankovic / DA Photography

    Maelezo ya picha, Ndege aina ya F-15

    Wahouthi wa Yemen wanadai kuwa wametungua ndege ya kivita ya Saudi Arabia; pia walisema walitumia silaha "zilizotengenezwa nchini humo" kuilenga ndege hiyo.

    Yahya Saree, msemaji wa jeshi la Wahouthi, aliandika kwenye mitandao ya kijamii kwamba vikosi vya jeshi la Yemen "vilifanikiwa kutungua ndege ya kivita ya Saudi Arabia aina ya F-15 wakati ikifanya operesheni za uhasama kusaidia harakati za kijeshi katika anga ya mkoa wa Marib."

    Yahya Saree amesema ndege hiyo ya kivita ililengwa "kwa kutumia kombora la angani-kwa-angani lililotengenezwa nchini humo."

    Msemaji huyo pia alikanusha madai ya Saudi Arabia kwamba Wahouthi walilenga mji wa Makka wiki hii.

    "Operesheni zetu hulenga miundombinu ya mafuta na kambi za kijeshi," alisema.

    Masaa machache yaliyopita, mifumo ya ulinzi wa anga ya Saudi Arabia ilisema kuwa ilizuia na kuharibu ndege isiyo na rubani (drone) iliyorushwa na Wahouthi wa Yemen kabla haijaingia katika anga iliyopigwa marufuku ya mji wa Makka.

    Wahouthi wamekuwa wakipambana tena na vikosi vya serikali ya Yemen, vinavyoungwa mkono na Saudi Arabia, tangu vita vya wenyewe kwa wenyewe nchini Yemen vilipoanza upya mwezi Julai.

    Kundi hilo pia limetangaza kuzuia usafiri wa majini kuelekea Saudi Arabia na kulenga meli za nchi hiyo katika Bahari Nyekundu.

  9. Vita vya Iran vimesababisha uhaba wa zana za kivita Marekani - Mkaguzi wa Pentagon

    .

    Chanzo cha picha, Martin Lockheed

    Maelezo ya picha, Mfumo wa anga wa Marekani wa Thaad

    Mkaguzi mkuu wa idara ya ulinzi ya Marekani anasema vita na Iran vimesababisha "uhaba" wa silaha na kikwazo katika usambazaji mpya, kinyume na Rais Donald Trump ambaye amekataa mara kwa mara kwamba Marekani inakabiliwa na uhaba.

    Trump amedai kuwa vifaa vya silaha vya Marekani "havina kikomo" na kusema kuripoti vinginevyo ni "habari za uwongo".

    Lakini mlinzi huru alisema Marekani ilitumia zaidi ya dola bilioni 22 kwa risasi kuanzia Februari hadi Juni, na kusababisha "uhaba wa kimkakati wa hesabu".

    Ilipoulizwa kuhusu ripoti ya mlinzi huyo, Ikulu ya White House ilisema Marekani ilikuwa na risasi "zaidi na za kutosha".

    Ripoti hiyo inatoa taswira ya kwanza ya aina yake, huru kuhusu akiba ya silaha za Marekani, data ambayo kwa kawaida huainishwa.

    Makadirio ya awali yameonyesha picha mbaya ya uhaba wa Marekani.

    Katika kipindi cha vita, vikosi vya Marekani vimetumia kiasi kikubwa cha mifumo ya mashambulizi ya ardhini ya masafa marefu na ulinzi wa anga na makombora unaotumika kuzuia mashambulizi yanayokuja ya Iran.

    Makadirio ya mwishoni mwa Julai kutoka Kituo cha Mafunzo ya Kimkakati na Kimataifa, au CSIS, yaligundua kuwa akiba ya baadhi ya vizuizi - kama vile kombora la Patriot na mfumo wa ulinzi wa anga THAAD - ilipungua kwa kiasi kikubwa, katika baadhi ya matukio kwa zaidi ya nusu.

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Maelezo ya picha, Mfumo wa anga wa Marekani wa Patriot
  10. Raia wa Uingereza atekwa nchini Malawi

    Police have offered a reward for details that could help find Nusrat Osman

    Chanzo cha picha, Handout

    Maelezo ya picha, Police have offered a reward for details that could help find Nusrat Osman

    Polisi nchini Malawi wanaendelea na uchunguzi wa tukio la kutekwa nyara kwa raia wa Uingereza katika mji wa Blantyre, kitovu cha biashara cha nchi hiyo.

    Kwa mujibu wa taarifa ya polisi, Nusrat Osman, mwenye umri wa miaka 47, alitekwa na watu wanne majira ya mchana siku ya Ijumaa. Inadaiwa kuwa watekaji hao walikuwa wakitumia gari la rangi ya kijivu aina ya Nissan Dualis.

    Mamlaka zimeahidi kutoa zawadi ya zaidi ya dola 17,000 za Marekani (takriban pauni 12,600) kwa mtu yeyote atakayetoa taarifa za kuaminika zitakazosaidia kupatikana kwa Osman na kuwafikisha wahusika wa tukio hilo mbele ya sheria.

    Osman, ambaye ni mama wa watoto wawili wadogo, anaripotiwa kufanya kazi katika kampuni ya ukaguzi wa hesabu nchini Malawi.

    Vyombo vya habari vya nchini humo vimeripoti kuwa mume wake ameeleza hofu na majonzi makubwa kufuatia kutoweka kwake.

    "Sijui alipo wala hali yake ikoje. Mke wangu ni mkaguzi wa hesabu na sina ugomvi na mtu yeyote," alinukuliwa akisema na gazeti la Nyasa Times.

    Polisi wamesema hadi sasa chanzo cha utekaji huo hakijafahamika. Pia wameeleza kuwa watekaji bado hawajawasiliana na familia ya Osman wala mamlaka za serikali.

    Wakati huo huo, Wizara ya Mambo ya Nje ya Uingereza imesema inafahamu taarifa za kutekwa kwa raia wake nchini Malawi na inaendelea kushirikiana kwa karibu na mamlaka za Malawi katika kufuatilia tukio hilo.

  11. Marekani yabana viza za maafisa wa Afrika Kusini kwa madai ya ubaguzi dhidi ya wazungu

    Marco Rubio

    Chanzo cha picha, Reuters

    Maelezo ya picha, Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, Marco Rubio

    Marekani imetangaza vikwazo vya usafiri dhidi ya watu wanaotuhumiwa kuwabagua wazungu walio wachache nchini Afrika Kusini, katika hatua mpya ambayo huenda ikachangia kuongezeka kwa mvutano wa kidiplomasia kati ya nchi hizo mbili.

    Utawala wa Rais Donald Trump umeendelea kuikosoa Afrika Kusini kuhusu sera zake za kushughulikia ukosefu wa usawa wa rangi, ukidai kuwa baadhi ya hatua hizo zinawabagua Waafrikaans, ambao wengi wao ni wazao wa walowezi wa Uholanzi na Ufaransa.

    Hata hivyo, serikali ya Afrika Kusini imekuwa ikikanusha mara kwa mara tuhuma hizo.

    Katika taarifa iliyotolewa Jumanne, Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, Marco Rubio, alisema serikali ya Afrika Kusini haijatoa majibu ya kuridhisha kuhusu wasiwasi uliowasilishwa hapo awali na Washington.

    Uhusiano kati ya Marekani na Afrika Kusini umeendelea kudorora tangu Donald Trump alipoingia tena madarakani mapema mwaka jana.

    Utawala wake umepunguza baadhi ya misaada kwa Afrika Kusini, kumfukuza balozi wa nchi hiyo nchini Marekani, na kutangaza kuwa utawapa hifadhi baadhi ya wazungu wa Afrika Kusini wanaodai kukabiliwa na mateso nchini mwao.

    Hata hivyo, serikali ya Afrika Kusini imeendelea kupinga madai kuwa inawalenga au kuwatesa raia weupe, pamoja na tuhuma za kunyang'anya ardhi yao.

    Imeeleza kuwa madai ya kuwepo kwa kile kinachoitwa "mauaji ya kimbari dhidi ya wazungu" nchini humo yamepuuzwa na wataalamu na hayana msingi wowote.

    Hata hivyo, takwimu za hivi karibuni za uhalifu nchini Afrika Kusini hazioneshi kuwa wazungu wanakabiliwa na tishio kubwa la kuvamiwa ikilinganishwa na makundi mengine ya wananchi nchini humo.

    Pia unaweza kusoma:

  12. Zaidi ya Wajapani 100,000 wafikisha umri wa miaka 100

    Wakati rekodi zilipoanza kuwekwa mwaka 1963, Japan ilikuwa na watu 153 pekee wenye umri wa miaka 100 au zaidi, lakini sasa idadi hiyo imeongezeka hadi 107,677.

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Maelezo ya picha, Wakati rekodi zilipoanza kuwekwa mwaka 1963, Japan ilikuwa na watu 153 pekee wenye umri wa miaka 100 au zaidi, lakini sasa idadi hiyo imeongezeka hadi 107,677.

    Idadi ya watu walio na umri wa miaka 100 au zaidi nchini Japan imevuka watu 100,000 kwa mara ya kwanza katika historia ya nchi hiyo, kwa mujibu wa Wizara ya Afya.

    Takwimu zinaonyesha kuwa Japan sasa ina watu 107,677 waliofikisha umri wa miaka 100 au zaidi, idadi kubwa zaidi duniani. Kati yao, asilimia 88 ni wanawake.

    Mwanamke mwenye umri mkubwa zaidi nchini humo ni Kishimoto Fuyo mwenye miaka 114 kutoka mji wa Kyoto, huku mwanaume mwenye umri mkubwa zaidi akiwa Kato Hikaru, mwenye miaka 112 kutoka Kumamoto.

    Waziri wa Afya, Kenichiro Ueno, alisema anafurahishwa na ukweli kwamba watu wengi zaidi wanaishi maisha marefu, yenye afya njema na yenye shughuli za kujenga jamii. Alieleza kuwa maendeleo katika sekta za tiba na teknolojia yamechangia ongezeko hilo.

    Hata hivyo, alionya kuwa kuongezeka kwa idadi ya wazee kunaleta changamoto kwa mfumo wa hifadhi ya jamii na huduma za ustawi wa wananchi.

    Wataalamu wanasema maisha marefu ya Wajapani yanachangiwa na sababu kadhaa, ikiwemo lishe bora na mtindo wa maisha unaohusisha shughuli za mwili. Mlo wa kawaida nchini humo unajumuisha samaki, mboga na wali, huku ukiwa na kiwango kidogo cha mafuta ikilinganishwa na nchi nyingi za Magharibi.

    Aidha, watu wengi wazee nchini Japan huendelea kutembea kwa miguu, kutumia usafiri wa umma, kuendesha baiskeli na kufanya mazoezi mepesi ya kujinyoosha.

    Japan imekuwa ikikabiliwa na ongezeko la idadi ya wazee kwa miaka mingi. Katika ishara ya mabadiliko hayo ya demografia, mauzo ya nepi za watu wazima yamekuwa yakizidi yale ya nepi za watoto kwa zaidi ya muongo mmoja.

    Soma zaidi:

  13. Lissu apendekezwa kuwania Tuzo ya Haki za Binadamu ya Umoja wa Ulaya

    Lissu Mahakamani

    Kundi la Chama cha Watu wa Ulaya (EPP) katika Bunge la Ulaya limemteua mwanasheria, mwanaharakati wa haki za binadamu na mwanasiasa wa Tanzania, Tundu Lissu, kuwa miongoni mwa wanaowania Tuzo ya Sakharov ya Uhuru wa Mawazo.

    Katika taarifa yake, EPP ilisema uteuzi wa Lissu unatambua mchango wake katika kutetea demokrasia, utawala wa sheria na haki za msingi za raia, licha ya changamoto mbalimbali za kisiasa na binafsi alizokumbana nazo kwa miaka kadhaa.

    Kundi hilo lilikumbusha kuwa Lissu alinusurika jaribio la mauaji mwaka 2017 kabla ya kurejea Tanzania kuendelea na kampeni za kudai mageuzi ya kidemokrasia. EPP ilieleza kuwa baadaye alikabiliwa na kukamatwa, mashtaka ya uhaini na kuzuiwa kushiriki uchaguzi wa urais wa mwaka 2025, huku chama chake kikiondolewa kwenye mchakato wa uchaguzi.

    Kwa mujibu wa EPP, matukio hayo yanaibua maswali kuhusu hali ya ushindani wa kisiasa na demokrasia ya mfumo wa vyama vingi nchini Tanzania.

    Kundi hilo lilisema Lissu anaashiria ujasiri, msimamo wa kidemokrasia na dhamira ya kutetea uhuru wa kisiasa, likiongeza kuwa uteuzi wake unaonyesha mshikamano wa Ulaya na watu wanaopigania demokrasia ya kikatiba na uhuru wa kisiasa barani Afrika pamoja na nchi washirika wa Umoja wa Ulaya.

    Tuzo ya Sakharov ya Uhuru wa Mawazo ndiyo tuzo ya juu zaidi inayotolewa na Umoja wa Ulaya (EU) kwa watu au makundi yaliyotoa mchango mkubwa katika utetezi wa haki za binadamu na uhuru wa msingi duniani.

    Maelezo zaidi:

  14. Edward Rukidi kutawazwa Mfalme wa Tooro Septemba 29

    Mwanamfalme Edward Rukidi Kijanangoma

    Chanzo cha picha, UBC

    Mwanamfalme Edward Rukidi Kijanangoma, ambaye hivi karibuni alitangazwa kuwa mfalme mpya wa Ufalme wa Tooro magharibi mwa Uganda, anatarajiwa kutawazwa rasmi Septemba 29, 2026.

    Hatua hiyo inafuatia kuidhinishwa kwake na Baraza Kuu la Kifalme la Tooro baada ya kutambulishwa kama mrithi wa marehemu Mfalme Oyo Nyimba Kabamba Iguru Rukidi IV.

    Hata hivyo, uteuzi wake umeibua mvutano ndani ya familia ya kifalme kuhusu suala la urithi wa kiti cha enzi. Baadhi ya wanafamilia wa karibu wa marehemu mfalme, akiwemo mama yake na dada yake, wamepinga uamuzi huo.

    Wanaopinga uteuzi huo wanadai kuwa mtoto wa marehemu mfalme ndiye anayestahili kurithi ufalme huo kwa mujibu wa wosia wa marehemu. Hata hivyo, mtoto huyo anayehusishwa na madai hayo hajawahi kutambulishwa rasmi mbele ya taasisi za ufalme.

    Mvutano huo umeendelea hata baada ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Uganda kuripotiwa kuishauri serikali kuzingatia matakwa ya wosia wa marehemu mfalme katika mchakato wa kumpata mrithi. Lakini viongozi wa ukoo wa kifalme walikataa msimamo huo, wakisisitiza kuwa masuala ya urithi wa ufalme yanapaswa kuamuliwa kwa kuzingatia taratibu na mila za ufalme, si kwa maelekezo ya serikali.

    Licha ya upinzani huo, viongozi wa ukoo wa kifalme wameendelea na maandalizi ya sherehe ya kutawazwa kwa Prince Edward kama ilivyopangwa.

    Wakati huohuo, Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi ya Uganda (UPDF), Jenerali Muhoozi Kainerugaba, ambaye ni mtoto wa Rais Yoweri Museveni, amemuunga mkono hadharani Prince Edward Rukidi Kijanangoma, akimtaja kuwa mrithi halali wa marehemu Mfalme Oyo.

  15. Tetesi za Soka Ulaya Jumatano: Barcelona yawanyatia Kane & Haaland

    Halaand & Kane

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Barcelona inaendelea kutathmini chaguo mbalimbali ili kuimarisha safu yao ya mashambulizi, huku majina ya Harry Kane wa Bayern Munich na Erling Haaland wa Manchester City yakitajwa kama mbadala endapo mpango wa kumsajili Julian Alvarez wa Atletico Madrid hautafanikiwa.

    Bayern Munich inatajwa kumfuatilia mshambuliaji wa kimataifa wa Ujerumani Nick Woltemade, anayemilikiwa na Newcastle United lakini anayekipiga kwa mkopo Juventus. Mabingwa hao wa Bundesliga wanamwona kama chaguo la baadaye la kuziba nafasi ya Kane.

    Nchini England, Manchester United wamefufua nia yao ya kumsajili beki wa Everton Jarrad Branthwaite, baada ya mchezaji huyo kurejea uwanjani kufuatia kipindi cha majeraha.

    Kwa upande wa vijana, Arsenal wameonyesha kuvutiwa na winga chipukizi wa Liverpool Rio Ngumoha, mwenye umri wa miaka 18. Hata hivyo, Liverpool wanaripotiwa kufanya kila juhudi kuhakikisha wanamfunga kwa mkataba mpya wa muda mrefu.

    Tottenham Hotspur nao bado hawajakata tamaa katika harakati za kumsajili kiungo wa Nottingham Forest Morgan Gibbs-White. Spurs walijaribu kumpata mwaka 2025, lakini Forest wameweka wazi kuwa hawana mpango wa kuuza nyota huyo.

    Naye mshambuliaji wa Real Madrid Endrick anaweza kuwa mmoja wa majina makubwa yatakayopatikana katika dirisha la usajili la Januari. Manchester United ni miongoni mwa klabu zinazofuatilia kwa karibu maendeleo ya Mbrazil huyo mwenye umri wa miaka 20.

    Kwingineko, kiungo wa Hispania Rodri amefichua kuwa alimwasiliana na kocha wa Real Madrid Jose Mourinho kumshukuru kwa hamu yake ya kutaka kumsajili, kabla ya yeye kuamua kujiunga na Barcelona akitokea Manchester City majira ya joto yaliyopita.

    Barcelona pia wanaendelea na mipango ya kuhifadhi nyota wao muhimu, huku mkurugenzi wa michezo Deco akifanya mazungumzo na mshambuliaji wa Brazil Raphinha kuhusu kuongeza muda wa mkataba wake, ambao kwa sasa unamalizika mwaka 2028.

    Nchini Italia, AC Milan wana nafasi ya kugeuza uhamisho wa mkopo wa mshambuliaji wa England Omari Hutchinson kutoka Nottingham Forest kuwa wa kudumu, kwa ada inayokadiriwa kufikia euro milioni 50.

    Pia unaweza kusoma:

  16. Wasanii wasusia tamasha la Ed Sheeran kupinga kuondolewa kwa Macklemore.

    .

    Chanzo cha picha, Getty

    Wasanii wote waliokuwa wamepangwa kutumbuiza katika tamasha la Ed Sheeran nchini Marekani wamejiondoa, wakipinga uamuzi wa kuondolewa kwa rapa Macklemore kufuatia kauli zake za kuunga mkono Palestina alizotoa jukwaani.

    Miongoni mwa waliojiondoa ni Finneas, kaka wa mwimbaji nyota Billie Eilish, ambaye alisema wasanii hawapaswi kuzuiwa au kunyamazishwa wanapotumia majukwaa yao kuzungumzia mateso ya watu wanaokandamizwa.

    Pia waliojitenga na ziara hiyo ni mwimbaji na mtunzi wa nyimbo kutoka Ireland Aaron Rowe, bendi ya Denmark Lukas Graham, pamoja na bendi ya muziki wa folk ya Ireland Beoga, ambayo imekuwa ikitumbuiza pamoja na Sheeran katika maonesho ya ziara hiyo.

    Hatua ya wasanii hao ilikuja saa chache baada ya Sheeran kueleza hadharani kuwa hatahusika katika mjadala kuhusu vita vya Gaza. Mwimbaji huyo alisisitiza kuwa hakuwa na nafasi yoyote katika uamuzi wa kumuondoa Macklemore.

    Kupitia ujumbe aliouchapisha kwenye Instagram, Sheeran alisema kuondolewa kwa Macklemore kulikuwa uamuzi wa waandaaji wa ziara, na si wake binafsi.

    Aliongeza kuwa hangeweza kufuta au kuondoka kwenye ziara hiyo kwa sababu ya wajibu wake kwa mashabiki, wafanyakazi na wanamuziki wanaotegemea maonesho hayo kwa ajira na kipato.

    Mapema mwezi huu, Macklemore, ambaye jina lake halisi ni Benjamin Haggerty, alitoa wito wa "Palestina Huru" na kuonyesha picha za uharibifu wa Gaza wakati wa maonesho mawili ya muziki yaliyofanyika New Jersey.

    Kauli hizo zilisababisha ukosoaji kutoka kwa baadhi ya makundi ya Wayahudi. Baada ya hapo, baadhi ya kumbi za maonesho ziliripotiwa kuweka shinikizo kwa waandaaji wa ziara hiyo, wakitaka rapa huyo aondolewe kwenye orodha ya watumbuizaji.

  17. Saudi Arabia yazuiwa droni ya Wahouthi karibu na Makka

    Makka

    Chanzo cha picha, Reuters

    Vikosi vya ulinzi wa anga vya Saudi Arabia vimesema viliizuia na kuiangamiza droni iliyokuwa imerushwa na waasi wa Wahouthi kutoka Yemen kabla haijaingia katika eneo la anga lililowekewa marufuku ya kuruka ndege karibu na mji mtakatifu wa Makka.

    Kwa mujibu wa muungano unaoongozwa na Saudi Arabia katika vita vya Yemen, tukio hilo limetokea wakati wa ongezeko la mashambulizi ya makombora na droni yanayolenga maeneo mbalimbali ndani ya ufalme huo.

    Msemaji wa muungano huo, Turki al-Maliki, amesema katika taarifa kwamba hii ni mara ya pili kwa Wahouthi kujaribu kushambulia Makka. Alisema jaribio la kwanza lilitokea Julai 2017, wakati kombora la masafa marefu lilirushwa kuelekea eneo hilo.

    Wakati huohuo, tahadhari ya kiusalama ilitolewa kwa muda mfupi Jumanne, tarehe 15 Septemba, katika miji ya Makka, Jeddah na Taif. Hata hivyo, mamlaka za ulinzi wa raia baadaye zilitangaza kuwa hali ilikuwa salama na kwamba "hatari imedhibitiwa".

    Tahadhari hiyo iliyotolewa mjini Makka imezua taharuki, kwani mji huo haujawahi kushuhudia tukio la aina hiyo katika kipindi cha hivi karibuni cha mvutano na mashambulizi kati ya Wahouthi na Saudi Arabia.

    Siku moja kabla, mashambulizi ya makombora na droni yaliyotekelezwa na Wahouthi dhidi ya miji mitatu nchini Saudi Arabia yaliwajeruhi raia 13, kwa mujibu wa muungano huo. Muungano huo pia ulisema nyumba saba na magari mawili yaliharibiwa katika mashambulizi hayo.

    Wahouthi hawajatoa kauli yoyote kuhusiana na madai hayo ya muungano unaoongozwa na Saudi Arabia.

    Soma zaidi:

  18. CBS yachapisha picha za uharibifu katika kambi za Marekani

    ,

    Chanzo cha picha, CBS

    Mtandao wa habari wa Marekani, CBS, ambao ni mshirika wa BBC nchini humo, umechapisha kwa mara ya kwanza picha mpya zinazoonyesha kile unachosema ni uharibifu mkubwa uliosababishwa na mashambulizi ya Iran dhidi ya kambi za kijeshi za Marekani Mashariki ya Kati.

    Kwa mujibu wa CBS, picha hizo za kipekee zinaonyesha uharibifu mkubwa katika baadhi ya kambi za kijeshi za Marekani, ambapo majengo, magari ya kijeshi na miundombinu mingine iliharibiwa katika mashambulizi ya makombora na ndege zisizo na rubani.

    Mmoja wa wanajeshi walioko katika kambi hizo alinukuliwa na CBS akisema kuwa ukubwa wa uharibifu uliosababishwa na mashambulizi hayo haujawekwa wazi kikamilifu kwa umma wa Marekani.

    "Hii ni hasara kubwa kwa kambi zetu ambayo wananchi wa Marekani hawajafahamishwa kikamilifu. Tumekuwa tukikabili mashambulizi mfululizo huku tukionekana kutokuwa na uwezo wa kujibu kwa ufanisi," alisema.

    Miongoni mwa picha zilizosambazwa ni moja inayodaiwa kupigwa katika Kambi ya Jeshi la Anga ya Prince Sultan nchini Saudi Arabia. Picha hiyo inaonyesha kile kinachodaiwa kuwa athari ya shambulio la moja kwa moja kwenye sehemu ya nyuma ya ndege ya kijeshi ya Boeing A-3 Sentry yenye injini nne.

    Katika picha hiyo, mkia wa ndege unaonekana kuwa umetenganishwa na sehemu kuu ya mwili wa ndege, huku mabaki yake yakionyesha dalili za kuungua. Uharibifu pia unaonekana kuathiri sehemu iliyobeba mfumo wa rada unaozunguka, unaotumiwa kufuatilia na kukusanya taarifa kuhusu shughuli za angani.

    Maelezo zaidi:

    Banda lililoharibiwa katika Kambi ya Bowering, Kuwait

    Chanzo cha picha, CBS

    Maelezo ya picha, Banda lililoharibiwa katika Kambi ya Bowering, Kuwait
    Uharibifu mkubwa katika jengo moja kwenye kambi ya kijeshi ya Arifjan nchini Kuwait.

    Chanzo cha picha, CBS

    Maelezo ya picha, Picha zinaonyesha uharibifu mkubwa katika jengo moja lililopo ndani ya Kambi ya Kijeshi ya Arifjan nchini Kuwait.
  19. Natumai hujambo.