'Kutoka kuwa watawa hadi wapenzi wa jinsia moja'

    • Author, Ian Alves
    • Nafasi, BBC News Brasil
  • Iliyochapishwa
  • Muda wa kusoma: Dakika 6

Haikuwa upendo mara tu tulipokutana. Wakati Luiza Silvério alipokutana kwa mara ya kwanza na mwanamke ambaye baadaye angekuwa mke wake, katika nyumba ya watawa walikoingia wakiwa na umri wa miaka 19 kama wanafunzi wa utawa, walichukiana.

Sasa wakiwa wameoana na wenye furaha, mke wake, Francília Costa, anaendelea kuzungumzia simulizi hiyo akiiambia BBC News Brazil: "Nilikuwa nikimfikiria vivyo hivyo. Jamani, inawezekanaje msichana awe na majivuno kiasi hicho?"

Francília alikuwa tayari ameishi katika nyumba hiyo ya watawa kwa miaka mitano wakati Luiza alipojiunga nao, miaka sita iliyopita. Na alikuwa ameweka nadhiri zake za milele kama kukataa umiliki wa kibinafsi wa bidhaa aina zote ikiwa ni pamoja na urithi, ahadi iliyotolewa kwa Mungu ndani ya Kanisa Katoliki na utiifu, na alikuwa akisomea shahada ya teolojia.

Akiwa amelelewa na babu na bibi yake waliokuwa waumini wa dini wenye msimamo mkali, katika eneo lenye ukame la Piaui, kaskazini-mashariki mwa Brazil, alihisi kwamba maisha ya utawa yalikuwa wito wa asili kwake.

Kisha Luiza akawasili. Akiwa hajaridhishwa na "upweke" aliouhisi katika miaka ya ujana wake huko Minas Gerais, kusini-mashariki mwa Brazil, naye pia alihisi kuwa na wito wa kujitolea kikamilifu katika maisha yake yote kwa huduma ya kidini.

"Tuliingia katika nyumba ya watawa tukiwa na lengo moja —kumtumikia Mungu," Francília anasema.

Taratibu, katika kipindi cha miaka miwili iliyofuata, lengo hilo liliwakutanisha na kuwafanya hawa wawili, mtawa na mwanafunzi wa utawa, kuwa karibu zaidi. Wakawa marafiki, na pole pole, chuki yao ya awali ilibadilika na kuwa heshima na kila mmoja kuanza kuvutiwa na mweziwe.

Lakini wakati tu urafiki wao ulipoanza kuchanua, kujitolea kwao kwa maisha ya utawa ukaanza kuyumba.

Janga la COVID-19 lilimwacha Francília akiwa na matatizo ya kupata mshutuko. Mara nyingi alikumbwa na hofu ya kuambukiza wengine virusi hivyo. Wakati wa vikao vyake vya tiba ya kisaikolojia, alianza kutafakari upya maamuzi yake ya maisha.

"Maisha ya kidini ni maisha mazuri sana — lakini unahitaji kuwa na afya njema ya mwili na akili. Haitoshi kujua tu jinsi ya kusali," anasema.

Wakati huo huo, Luiza, aliyekuwa akiomboleza kifo cha bibi yake, naye alianza kukumbwa na hofu, na baadaye akapatwa na mfadhaiko. Tiba yake ya kisaikolojia ilimsaidia kutambua kwamba alihitaji kutanguliza afya yake ya akili na kuachana na ndoto yake ya kuweka nadhiri za utawa na kuishi katika nyumba ya watawa maisha yake yote.

"Luiza pia alihitaji kutunza afya yake ya akili," Francília anasema. "Na alipoamua kuondoka, nilishtuka sana. Nilijiambia, 'Mungu wangu! Msichana wa umri huo ana ujasiri wa kufikiria kuanza maisha upya popote pale. Mimi mwenyewe siwezi hata kufikiria kuanza upya, ingawa nimeishi muda mrefu zaidi nje ya nyumba hii ya watawa nikilinganisha na muda ambao nimekuwa ndani.'"

Akihamasishwa na ujasiri wa rafiki yake huyo mdogo, Francília naye, kwa upande wake, alifikia hitimisho lile lile. Aliamua pia kuondoka katika nyumba ya watawa—ingawa kuondoka kuligeuka kuwa jambo gumu zaidi kuliko walivyotarajia wote wawili.

"Maisha huku nje si rahisi," Luiza anasema. "Ni magumu sana.

'Hujui kama utaweza kuendelea na masomo ya chuo kikuu, au kama utaweza kupata kazi.'"

Francília naye alihisi vivyo hivyo. "Hebu fikiria ukienda kwenye usaili wa kazi, halafu unaulizwa, 'Ulisomea nini?' Unajibu, 'Teolojia.' Ni kazi ya aina gani nitakayopata?" anasema.

Kufikia wakati alipoamua kuondoka, baada ya kuishi katika nyumba ya watawa kwa miaka saba, Francília alilazimika kununua mavazi mapya kabisa ili aanze maisha yake mapya, kwa sababu hangeendelea tena kuvaa vazi la kitawa.

Hata hivyo, changamoto kubwa zaidi ya kifedha ilikuwa kulipa kodi ya nyumba. Kwa hiyo, ili kupunguza gharama, marafiki hao wawili walikubaliana kupanga na kuishi pamoja katika chumba kimoja.

Kisha, jioni moja, baada ya kutazama pamoja filamu ya vichekesho vya mapenzi 'Love in Verona', ambayo wahusika wakuu wanaanza kwa kuchukiana na baadaye kupendana, Francília alimweleza Luiza kwamba hisia zake kwake zilikuwa zimefuata mkondo huo.

Walipokuwa vijana, wote wawili walijitambua kama mtu ambaye anavutiwa kimapenzi, kihisia, au mvuto wa kimapenzi kwa zaidi ya jinsia moja.

Hata hivyo, jambo hilo halikuathiri hamu yao ya kuwa watawa wala uamuzi wao wa kujiunga na nyumba ya watawa.

"Hilo halikutufanya tumwogope Mungu wala kuogopa kuwa huko," Luiza anasema. "Sikutaka kuwa katika uhusiano wa kimapenzi na mtu yeyote. Nilitaka kwa dhati kuishi maisha ya useja, kufuata dini yangu na Kanisa langu. Sikuwahi kufikiria uwezekano wa kutoka na kuanzisha uhusiano wa kimapenzi na mtu."

Francília anakubaliana na hilo. "Hakukuwa na muda wa kufikiria jambo lingine lolote," anasema. "Kuingia katika nyumba ya watawa kulikuwa rahisi sana, lakini kutoka lilikuwa jambo gumu zaidi nililowahi kupitia maishani mwangu."

Kwa sasa, wakiwa wanaishi pamoja kama wanandoa, changamoto yao kubwa ilikuwa jinsi ya kuendelea kuishi na kuifuata imani yao.

Mwaka mmoja baada ya kuondoka katika nyumba ya watawa, na miaka miwili kabla ya harusi yao, mnamo Oktoba 2025, Papa Francisko, aliyekuwa kiongozi wa kwanza wa Kanisa Katoliki la Roma kutoka Amerika ya Kusini, aliruhusu mapadri kuwabariki wanandoa wa jinsia moja na wanandoa waliokuwa katika hali ambazo Kanisa halikutambua kikamilifu kama ndoa halali, chini ya masharti fulani.

Hata hivyo, alisisitiza kwamba Kanisa bado lilizingatia mahusiano ya jinsia moja kuwa "dhambi kwa mtazamo wa mafundisho ya Kanisa," na halikuyatambua kama ndoa halali za Kanisa.

"Hili ni jambo ambalo mimi na Fran hulizungumzia sana nyumbani," Luiza anasema. "Huwezi kumtenganisha Yesu kama mwanadamu na Yesu wa utakatifu. Yeye ni mmoja. Na ujinsia wetu na imani yetu havipaswi kutenganishwa, kwa sababu viko ndani yetu. Sisi ni wanandoa wenye imani — hakuna namna tunaweza kuvigawanya."

Wawili hao bado wanaendelea kuwasiliana na watawa na mapadri waliokuwa nao katika maisha ya nyumba ya watawa — lakini hakuna mtu kutoka Kanisa aliyehudhuria harusi yao. Hata hivyo, Luiza anasema: "Tulipokea upendo mwingi, jumbe na maombi yaliyotolewa kwa ajili yetu, siku yetu ya harusi."

"Labda hatuna picha ya madhabahuni mwa kanisa — lakini tuna picha pamoja na Mama Yetu wa Aparecida [sanamu ya Bikira Maria, mama wa Yesu, anayeheshimiwa sana nchini Brazili]. Kwetu sisi, yeye anawakilisha shukrani, maombezi na kuwekwa wakfu kwa familia yetu kwa Mungu."

Wala hawajaacha ile hisia ya wito na dhamira iliyowafanya waingie katika nyumba ya watawa walipokuwa vijana.

Baada ya kushirikisha simulizi yao kwenye mitandao ya kijamii, wanandoa hao walianza kupokea idadi kubwa ya ujumbe kutoka kwa Wakristo waliokuwa na maswali kuhusu ujinsia wao wenyewe, pamoja na watu wanaoshiriki mapenzi ya jinsia moja, wanaovutiwa kimapenzi na zaidi ya jinsia moja au watu waliobadili jinsia waliokuwa na maswali kuhusu imani.

"Hili lilianza kuimarisha zaidi hamu yetu ya kuzungumza kuhusu simulizi yetu kwa uwazi, kuhusu ujinsia wetu na imani yetu," Luiza anasema. "Lilikuwa jambo lenye maana kabisa, na linawasaidia watu wengi.

"Fursa hii inaimarisha zaidi safari yetu ya imani kama watu binafsi na wanandoa. Kila nafasi tunayopata ya kushirikisha wengine simulizi yetu — kwetu sisi, hiyo ni njia ya kuonyesha kuendelea kwa dhamira yetu."

Francília anasema: "Dhamira yetu kuwa hapa ili kusikiliza simulizi za watu na kuwasaidia. Mojawapo ya changamoto kubwa unapotekeleza unachotaka kupitia mitandao ya kijamii ni kujua jinsi ya kusikiliza na kujua jinsi ya kuzungumza.

"Kwa sababu hili ni jambo nililokuwa nikisema kila mara, 'Kama siku moja nitapaswa kuwa na familia, Mungu ataniletea mfano wa familia ambayo Yeye anataka niwe nayo.' Kwa hiyo… tuko hapa.

"Ingawa linaweza kuonekana kuwa jambo la kushangaza sana, kama kuna mungu wa mapenzi duniani, basi wetu alikuwa Mungu."