Maandalizi ya mwisho wa dunia: Je, uko tayari?

.

Chanzo cha picha, Getty Images

Iliyochapishwa
Muda wa kusoma: Dakika 10

Je, unapaswa kujiunga na watu wanaojiandaa kwa mwisho wa dunia? Na ikiwa ndivyo, uanzeje?

Mnamo Februari 2025, wanasayansi wa Chuo Kikuu cha Chicago walisogeza Saa ya Mwisho wa Dunia (Doomsday Clock) hadi sekunde 89 kabla ya saa sita usiku. Saa hiyo ni ishara inayotumika kuonyesha kiwango cha hatari ya binadamu kutoweka kabisa, na huu ndio muda ambao imewahi kuwa karibu zaidi na "dakika ya mwisho".

Lakini kutokana na hali ya dunia ilivyo, ni nani angeweza kuwalaumu wanasayansi hao kwa kujaribu kutabiri hatari zinazoweza kutukabili?

Wanasayansi wa tabianchi wanaonya kuwa tuko nyuma katika kutimiza malengo ya kuzuia mabadiliko hatari ya tabianchi. Akili bandia (AI) inaendelea kusonga mbele licha ya tahadhari kutoka kwa wataalamu kadhaa na hata maonyo yanayoonyeshwa katika filamu za Hollywood. Hata homa ya ndege inaonekana kujaribu kurejea.

Kwa hiyo, huenda si jambo la kushangaza kwamba idadi inayoongezeka ya watu haingoji kuona ni aina gani ya janga litakalotokea kwanza.

Raia wenye wasiwasi pamoja na serikali wanawekeza katika makazi ya chini ya ardhi, yaliyoundwa ili kuwezesha watu kuendelea kuishi endapo dunia itakumbwa na janga kubwa.

Miongoni mwa watu mashuhuri wanaohusishwa na harakati hizi za kujenga makazi ya chini ya ardhi ni mwanzilishi wa Facebook, Mark Zuckerberg, ambaye anaripotiwa kujenga makazi makubwa ya kujikinga chini ya ardhi katika eneo lake la Hawaii, yakiwa na mifumo yake ya chakula na nishati. Aliyekuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Microsoft, Bill Gates, pia anaripotiwa kuwa na makazi makubwa ya chini ya ardhi chini ya nyumba zake huko California na Washington.

Lakini si matajiri wakubwa pekee wanaovutiwa na bunkers. Hata mataifa yamekuwa yakichunguza wazo hilo.

Hauhitaji Whatsapp
BBC Swahili sasa kwenye WhatsApp

Pata habari za kina kutoka BBC News Swahili, moja kwa moja kupitia WhatsApp.

Bonyeza hapa kujiunga

Mwisho wa Whatsapp

Mwisho wa mwaka 2024, Uswisi ilitangaza mipango ya kuboresha mtandao wake mkubwa wa makazi 360,000 ya chini ya ardhi yaliyojengwa wakati wa Vita Baridi – ambayo yanaweza kuhifadhi zaidi ya watu milioni tisa. Nchini Uswisi, kila raia ana haki ya kupata makazi ya chini ya ardhi kutokana na sheria iliyopitishwa mwaka 1963.

Wakati huohuo, nchini Finland, jiji la Helsinki mara nyingi hutajwa kama mfano bora wa mipango ya ulinzi wa raia chini ya ardhi. Lina maeneo makubwa yaliyotengenezwa si kwa ajili ya dharura pekee, bali pia yanatumika katika maisha ya kawaida, yakiwa na mabwawa ya kuogelea na migahawa.

Uingereza ina idadi ya bunkers zilizojengwa wakati wa Vita Baridi, lakini wataalamu wanasema nyingi hazifai tena kwa matumizi ya sasa. Serikali haionekani kuwa na mpango wa kujenga makazi mapya, hivyo baadhi ya watu wanashirikiana na kampuni maalumu kujenga maeneo yao ya kuishi chini ya ardhi.

"Biashara yangu nyingi ilikuwa kujenga vyumba vya kujikinga, vyumba salama, milango na madirisha ya usalama ili kutengeneza eneo salama ndani ya nyumba iwapo kungetokea uvamizi. Sasa ningesema ni nusu kwa nusu kati ya hilo na makazi ya chini ya ardhi," anasema Paul Weldon, anayeendesha kampuni ya The Panic Room Company.

.

Chanzo cha picha, Getty Images

Anasema mabadiliko hayo yalianza baada ya kuzuka kwa vita nchini Ukraine, na sasa anajenga bunkers maalumu nchini Uingereza na nje ya nchi. Lakini si matajiri pekee wanaofanya hivyo.

"Imeshuka hadi kwa watu wa kawaida," anasema Weldon. "Kwa mfano, tunapata maombi kutoka kwa watu ambao tayari wana basement na wanataka kuifanya iwe salama. Hapo unazungumzia karibu pauni 100,000, badala ya kiwango cha chini cha nusu milioni kwa bunker maalumu ya chini ya ardhi."

Weldon anaamini kwamba majira ya baridi ya nyuklia kwa kiwango kikubwa si hatari inayowezekana zaidi. Badala yake, anasema makazi mengi hujengwa kama sehemu ya kujisitiri kwa muda mfupi iwapo kutatokea mafuriko, machafuko makubwa ya kijamii au hata shambulio la bomu chafu.

Kwa hiyo, je, unapaswa kuanza kuchimba bustani yako? Ikiwa ndivyo, unapaswa kuijengaje? Unapaswa kuhifadhi nini? Na utawezaje kupata hewa safi, maji na nishati?

Usiwe na hofu – au labda uwe na hofu zaidi ikiwa tayari una wasiwasi – kwa sababu tunaingia kwa kina katika suala hili na kukuletea ushauri wa kujenga bunker yako mwenyewe ya chini ya ardhi.

Uhandisi

Makazi ya kawaida ya kujikinga dhidi ya mabomu hayajengwi kustahimili shambulio la moja kwa moja. Ungekuwa na bahati mbaya sana iwapo kichwa cha kombora kingedondoka moja kwa moja juu yako.

"Sababu ya kuyaweka chini ya ardhi ni kwamba iwapo mlipuko utatokea umbali wa kilomita kadhaa, nguvu iliyotolewa husafiri zaidi kwa mlalo na kupita juu ya bunker," anasema Weldon.

Kwa familia ya watu watano, anapendekeza makazi yenye ukubwa wa takriban mita 8 kwa 4. Hii ingewapa nafasi ya kuishi kwa starehe kiasi na kuwa na faragha ya kibinafsi.

Makazi mengi hujengwa kwa zege.

"Unaweza kutumia risasi, lakini ni ghali sana," anasema Weldon.

"Ikiwa unajenga, kwa mfano, maegesho ya magari chini ya ardhi, hakuna tofauti kubwa. Kadiri zege linavyokuwa nene, ndivyo ulinzi dhidi ya milipuko na mionzi unavyoongezeka. Kwa bunker yenye kiwango cha NATO, huenda ukahitaji zege lenye unene wa mita 2 hadi 3 na mita kadhaa za zege juu yake."

.

Chanzo cha picha, Getty Images

Wanasayansi wamefanya hesabu kuhusu kiwango cha ulinzi kinachohitajika katika tukio la kuvuja kwa mionzi ya nyuklia kwa kiwango kikubwa.

"Katika hali mbaya zaidi, kiwango cha ulinzi kinachotolewa na vifaa vya kuzuia mionzi, kama vile zege yenye msongamano mkubwa, huamuliwa na uwezo wake wa kupunguza kwa ufanisi mionzi ya neutroni na gamma," anasema Profesa Patrick Tang wa Chuo Kikuu cha Newcastle, Australia.

Mwaka 2024, Tang alikuwa mmoja wa waandishi wa mapitio kuhusu zege linalotumika kuzuia mionzi. Anapendekeza zege nzito yenye msongamano wa zaidi ya kilo 3,200 kwa kila mita ya ujazo. Zege hilo hutoa kiwango cha ulinzi kinachozuia mionzi kutoka kwenye mabomu ya mgawanyiko wa nyuklia kupenya kwenye makazi.

"Unene huo unahakikisha kwamba kiwango cha mionzi kinachopita kwenye kinga kinabaki katika kiwango cha sievert 0.0001 au chini yake, ambacho kinachukuliwa kuwa salama kwa binadamu," anasema.

Pia utahitaji milango maalumu ya kuzuia mlipuko. Milango hiyo inaweza kukulinda dhidi ya milipuko na mafuriko.

"Mlango unaweza kuwekwa ndani ya ukuta wa zege, kisha ukaweka zege ndani ya mlango wenyewe," anasema Weldon. "Vinginevyo, unaweza kutumia chuma. Aina tunayotumia ina unene wa takriban milimita 20, ikiwa na tabaka la chuma lililowekwa ndani ya zege. Huo ndio mlango wa kwanza, lakini tunaweka mwingine pia."

Baada ya yote, huu ni mwisho wa dunia – huwezi kuwa mwangalifu kupita kiasi.

Huduma muhimu

Hewa safi. Umeme. Na ikiwezekana Wi-Fi. Hivi ni baadhi ya vitu vya msingi ambavyo tungependa kuwa navyo katika makazi ya kujikinga wakati wa mwisho wa dunia. Vingi kati yake ni rahisi kiasi kuvifunga.

Umeme unaweza kutoka kwenye mfumo wa kawaida wa umeme, jenereta ya dharura au chanzo cha nishati kinachojitosheleza, kama vile paneli za sola zilizowekwa juu ya ardhi.

.

Chanzo cha picha, Getty Images

Iwapo unataka kuwasiliana na watu walio nje, Weldon anasema intaneti na simu za satelaiti pia hutumika kwa kawaida, huku antena za nje zikiunganishwa na bunker.

"Kadiri muda unavyokwenda, tunaweka pia Starlink zaidi," anasema, akirejea mtandao mkubwa wa satelaiti unaotoa huduma ya intaneti karibu kila mahali duniani.

Kuhakikisha kuwa kuna hewa safi katika eneo lililofungwa pia ni muhimu, anasema Antonia Cornaro wa International Tunnelling and Underground Space Association, yenye makao yake Uswisi.

"Makazi mengi hutumia vichujio vya hewa vya ufanisi wa juu (HEPA) au mifumo ya shinikizo la juu ndani ili kuzuia uchafuzi kuingia."

Vichujio vya HEPA vimeundwa kuondoa asilimia 99 ya chembechembe kutoka angani, huku mifumo ya shinikizo la juu ikiwa ya kawaida katika majengo yaliyoundwa kujikinga dhidi ya vitisho vya kemikali, kibayolojia, mionzi na nyuklia.

Mfumo huo huweka shinikizo la hewa ndani ya bunker kuwa kubwa kuliko nje, hivyo kuzuia hewa iliyochafuliwa kuingia.

Chakula

Mnamo Februari 2025, National Preparedness Commission ya Uingereza ilichapisha ripoti iitwayo "Just In Case", iliyochunguza uwezo wa nchi hiyo kukabiliana na dharura zinazoweza kuathiri upatikanaji wa chakula. Ripoti hiyo ina mambo ya kutisha.

Inasema Uingereza kwa sasa haina "mkakati madhubuti wa usalama wa chakula na ustahimilivu unaolingana na changamoto za siasa za dunia katika karne ya 21."

Mwandishi wa ripoti hiyo, Profesa Timothy Lang, alichunguza maandalizi ya nchi mbalimbali kukabiliana na kile kinachoitwa misukosuko ya upatikanaji wa chakula.

"Uswisi huhifadhi akiba ya miezi mitatu ya bidhaa muhimu, na mwaka mmoja uliopita walipitisha kanuni kwamba wataongeza akiba hiyo hadi miezi 12," anasema.

"Ujerumani inatoa ushauri wa kina kabisa rasmi, hata kwa walaji wa mboga na wasiokula mboga na kadhalika."

.

Chanzo cha picha, Alamy

Mamlaka za Ujerumani zinawashauri raia kuhifadhi chakula cha siku 10 kwa kila mtu, kwa kuzingatia kalori 2,200 kwa siku na kutoa maelezo ya kina kuhusu mahitaji ya lishe.

Hayo yanajumuisha kilo 3 za nafaka, mkate na viazi; kilo 4 za mboga; kilo 2.5 za matunda; na kilo 1.2 za nyama, samaki na mayai.

Kwa hatua kali zaidi, Kanisa la Mormon linawashauri waumini wake kuwa na akiba ya chakula cha miezi mitatu.

Nchini Uingereza, hakuna ushauri kama huo rasmi. Kwa hiyo, ni nini unapaswa kuwa nacho kwenye kabati lako la chakula au bunker?

Mifano ya wazi ni vyakula vya makopo – hasa nyama na mboga zenye kiwango kidogo cha asidi, ambavyo vinaweza kudumu kwa miaka mitano au zaidi.

"Tuna makopo yenye muda wa matumizi wa miaka 25," anasema Leigh Price, mmiliki wa duka la vifaa vya kujiandaa kwa dharura na kuishi wakati wa majanga, The Bugout.

"Lakini kiuhalisia, ukiyahifadhi vizuri, hayataharibika."

Price pia huuza vyakula vilivyokaushwa kwa kugandishwa, sawa na vile vinavyohifadhiwa katika Kituo cha Kimataifa cha Anga za Juu.

"Ni chakula kilichopikwa – kwa mfano, pilipili yenye nyama – kisha hukausha kwa kugandisha ili kuondoa unyevu wote. Kwa njia hiyo kinaweza kuhifadhiwa kwa muda mrefu na kupashwa moto kwa usalama."

Kwa Price, ambaye alikulia katikati ya Wales, kuhifadhi chakula ni jambo la kawaida.

"Nakumbuka mwaka 1982 tulipokumbwa na dhoruba ya theluji na tukakatika na maeneo mengine kwa siku nne. Lakini watu wengi walikuwa na vyakula vya kutosha na makopo nyumbani. Waulize wakulima – siku zote wanahakikisha kuna chakula cha kutosha nyumbani. Ni mtindo wa maisha ambao watu wameupoteza kwa sababu ununuzi umekuwa rahisi sana siku hizi."

Mwaka 2023, watafiti wawili wa mifumo ya ugavi kutoka Chuo Kikuu cha Bradford walitoa hoja kwamba kuhifadhi kiasi cha chakula kwa ajili ya dharura ni jambo ambalo sote tunapaswa kuanza kufanya tena.

"Kujiandaa – kufikiria mapema na kuchukua hatua – ni kinyume cha kununua kwa hofu," walisema.

Maji

.

Chanzo cha picha, Getty Images

Binadamu anaweza kuishi kwa takriban siku 30 bila chakula, lakini siku tatu tu bila maji. Kwa hiyo, bunker yoyote ya chini ya ardhi inahitaji mpango wa kutosha wa maji.

Katika bunkers anazojenga, Weldon anasema anatumia njia rahisi.

"Tunatumia vyombo vikubwa vya maji safi kama vile vile vinavyoonekana ofisini, au vyombo vikubwa zaidi vinavyoweza kujazwa iwapo inaonekana kuna jambo linakaribia kutokea," anasema.

"Katika eneo moja tulilojenga, tulikuwa na sinki rahisi la chuma lenye matangi mawili chini yake – moja la maji safi na jingine la maji taka – yote yakitumiwa kwa pampu ya mguu."

Mfumo wa maji taka huwa muhimu ikiwa watu watakaa chini ya ardhi kwa muda mrefu, hivyo Weldon hujumuisha mfumo huo katika miundo yake pamoja na vyoo vyenye vali maalumu.

Kwa makazi makubwa zaidi au maeneo ya kiraia yaliyo chini ya ardhi, eneo linakuwa muhimu.

"Ikiwa unaweza kufikia maji ya chini ya ardhi au tabaka la maji chini ya ardhi, unaweza kuleta maji safi na kuondoa maji taka kwa kiwango kikubwa," anasema Antonia.

"Na visima, bila shaka, vinawezekana."

Lakini tukidhani huna kisima kwenye bustani yako, ni kiasi gani cha maji safi unapaswa kuhifadhi?

Kwa bahati nzuri, Shirika la Afya Duniani (WHO) limefanya hesabu hizo:

Matumizi ya maji Kiasi kinachohitajika kwa siku

Kunywa Lita 2.5–3

Usafi wa mwili Lita 2–6

Kupika Lita 3–6

Nini kiwe kwenye begi lako la dharura?

Kuanzia Shirika la Msalaba Mwekundu hadi serikali ya Uingereza, taasisi mbalimbali zinashauri kuwa na vifaa vya dharura tayari kwa matukio kama mafuriko, moto na kukatika kwa umeme.

Begi lako la dharura linapaswa kuwa na vitu vitakavyokuweka salama kulingana na hatari zinazoweza kutokea katika eneo unaloishi, anasema Price.

.

Chanzo cha picha, Alamy

"Inategemea kama unaishi, kwa mfano, katika eneo linalokumbwa na mafuriko – ni vitu gani muhimu ungehitaji? Huhitaji bastola za milimita 9 wala upuuzi kama huo. Ni vitu vya kawaida na vya matumizi."

"Ikiwa una watoto, unaweza kutaka kuchukua vifaa vya kuchorea na kadi za kucheza iwapo mtalazimika kuondoka nyumbani na kwenda katika ukumbi wa michezo wa eneo lenu, labda kwa usiku mmoja."

"Watu wanaojiandaa kwa majanga wamepata sifa kwamba wote wanasubiri mwisho wa dunia. Lakini si hivyo; ni kuwa na tahadhari na kuhakikisha wewe na familia yako mko salama na mnaweza kuwa na maisha yenye starehe kadiri inavyowezekana iwapo jambo fulani litatokea."

Hii ni orodha ya kuanzia, kwa kuzingatia ushauri wa serikali na mashirika mbalimbali ya misaada:

Maji ya chupa (angalau galoni tatu kwa kila mtu, ikiwezekana)

Nyama, matunda na mboga za makopo

Vyakula vingine visivyoharibika, kama vile vilivyokaushwa kwa kugandishwa au kwa kuondolewa unyevu

Nguo za joto na zinazozuia maji

Sanduku la huduma ya kwanza pamoja na dawa zozote unazotumia mara kwa mara

Tochi inayotumia betri au inayochajiwa kwa kuzungusha mkono

Redio inayotumia betri au inayochajiwa kwa kuzungusha mkono

Betri zinazotumia nishati ya sola

Kifaa cha matumizi mbalimbali (multitool)

Dawa ya kusafisha mikono na/au vitambaa vya kufutia

Mahitaji ya watoto wachanga, kama nepi na maziwa ya kopo, ikiwa yanahitajika

Ramani za eneo lako

Orodha ya namba muhimu za simu na anwani

Je, mustakabali wetu uko chini ya ardhi?

Maeneo ya chini ya ardhi hayahusiani tu na "mwisho wa dunia". Baadhi ya wapangaji miji na wanamazingira wanaamini kuwa maeneo yaliyo chini ya ardhi ni rasilimali ambayo bado haijatumika kikamilifu.

Kwa hiyo, tunaweza kufanya nini huko chini?

Kilimo

.

Chanzo cha picha, Alamy

Kilimo cha chini ya ardhi kinahusisha kupanda mazao chini ya uso wa dunia katika mazingira yanayodhibitiwa, kama vile vichuguu, vyumba vya chini ya ardhi na migodi iliyoachwa.

Kinatumia mwanga wa kutengenezwa, kilimo cha maji (hydroponics) na udhibiti wa hali ya hewa ili kuunda mazingira bora ya kilimo bila kutegemea mwanga wa jua au hali ya hewa.

Wanaounga mkono wazo hilo, wakiwemo waendeshaji wa shamba lililoko katika London Underground, wanasema njia hiyo huokoa maji, hupunguza matumizi ya dawa za kuulia wadudu na kuwezesha uzalishaji wa mazao mwaka mzima, huku ikiimarisha usalama wa chakula katika maeneo yenye watu wengi.

Majengo ya kwenda chini badala ya juu

.

Chanzo cha picha, Bnkr Arquitectura/Solent News/Shutterstock (1469925e)

Fikiria jengo refu linalokwenda chini ya ardhi kwa ghorofa nyingi badala ya kwenda juu kuelekea angani.

Waendelezaji wa wazo hilo wanasema kujenga majengo hayo chini ya ardhi kunaweza kupunguza gharama za matumizi ya chuma, pamoja na mifumo ya kupasha na kupooza majengo.

Mifano iliyopendekezwa ni pamoja na Underground Science City, jengo linalopangwa kujengwa Singapore ambalo limeundwa kustahimili matetemeko ya ardhi na linatarajiwa kuwa na nafasi kwa watafiti 4,500.

Mwaka 2018, hoteli ya InterContinental Shanghai Wonderland ilijengwa ndani ya machimbo yaliyotelekezwa nje ya Shanghai.

Hyperloop

.

Chanzo cha picha, Getty Images

Moja ya miradi mingi ya Elon Musk, Hyperloop ni mfumo unaopendekezwa wa usafiri wa kasi kubwa na unaotumia nishati kidogo, ambapo maganda ya abiria husafiri ndani ya mirija yenye shinikizo la chini ili kupunguza msuguano wa hewa na kuwezesha kufikia kasi ya zaidi ya kilomita 1,120 kwa saa.

Wazo hilo linatumia teknolojia ya kuelea kwa sumaku na msukumo wa umeme ili kupunguza muda wa safari kati ya miji mikubwa.

Hata hivyo, mradi huo bado unakabiliwa na changamoto nyingi za kiteknolojia kabla ya kuwa mfumo halisi wa usafiri.