Moja kwa moja, Trump asema makubaliano ya kumaliza vita na Iran yako karibu baada ya kusitisha mashambulizi

Rais wa Marekani, Donald Trump, amedai kuwa makubaliano ya awali yanayolenga kumaliza vita na Iran yako karibu kufikiwa, baada ya kutangaza kuwa amesitisha mashambulizi yaliyokuwa yamepangwa dhidi ya nchi hiyo.

Muhtasari

Skip Video and continue reading
  • s
  • a
  • Sonko
  • xx
  • xx
  • xx
  • xx
  • xx
  • Dangote
  • xx
  • Lydia Wanjiku

Moja kwa moja

Na Lizzy Masinga

  1. Shambulio la droni nchini Sudan lalenga msafara wa mazishi na kuua watu kadhaa

    Mji wa El-Obeid umekuwa ukilengwa katika mashambulizi kadhaa ya droni, ikiwa ni pamoja na wakati picha hii ilipopigwa mwezi Machi.

    Chanzo cha picha, Los Angeles Times via Getty Images

    Shambulio la ndege isiyo na rubani lililolenga msafara wa mazishi katika makaburi ya mji wa El-Obeid nchini Sudan limeua takribani watu wanne na kuwajeruhi wengine kadhaa, kwa mujibu wa makundi mawili ya kutetea haki za binadamu na huduma za afya, Sudan Doctors Network na Emergency Lawyers.

    Makundi yote mawili yamelilaumu kundi la wanamgambo la Rapid Support Forces (RSF) kwa kuhusika na shambulio hilo. Kundi la Emergency Lawyers limesema kuwa shambulio hilo ni sehemu ya mfululizo wa mashambulizi ya droni yaliyoanza Jumatano jioni, ambapo kwa jumla watu wasiopungua 23 wameuawa.

    RSF haijatoa tamko lolote kuhusu madai hayo.

    Mji wa El-Obeid, ambao kwa sasa unadhibitiwa na jeshi la Sudan, ni moja ya maeneo muhimu ya mapigano katika vita vya wenyewe kwa wenyewe vya Sudan vilivyoanza miaka mitatu iliyopita baada ya viongozi wa jeshi na RSF kutofautiana kuhusu mustakabali wa nchi hiyo.

    Mapigano hayo yamesababisha kile kinachotajwa kuwa janga kubwa zaidi la kibinadamu duniani kwa sasa, ambapo zaidi ya watu milioni 11 wamelazimika kuyahama makazi yao na watu milioni 28 wanakabiliwa na njaa kali.

    Hakuna takwimu rasmi na za kuaminika kuhusu idadi kamili ya waliopoteza maisha tangu vita hivyo vianze, lakini inakadiriwa kuwa zaidi ya watu 50,000 wamefariki dunia.

    Unaweza kusoma;

  2. Tetesi za soka Ijumaa: Lewis Hall wa Newcastle ana nia ya kuondoka

    Lewis Hall

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Manchester United inaonesha nia ya kumsajili mlinzi wa Newcastle United na timu ya taifa ya England, Lewis Hall (21), ambaye anaripotiwa kutaka kuondoka klabuni hapo.

    Mlinzi wa kushoto wa Fulham na timu ya taifa ya Marekani, Antonee Robinson (28), pia anatazamwa na Manchester United kama usajili wao kwa msimu ujao.

    Barcelona haitalingana na ofa kubwa za kifedha zinazotolewa kwa kiungo wa Ureno Bernardo Silva (31) na Atletico Madrid pamoja na Real Madrid, ambazo zote zinataka kumsajili mkataba wake na Manchester City utakapoisha mwishoni mwa Juni.

    Real Madrid inaonekana kuwa mbele katika mbio za kumsajili Bernardo Silva na tayari ipo kwenye mazungumzo ya hatua za mwisho kuhusu makubaliano binafsi ya mchezaji huyo.

    Beki wa Croatia wa Manchester City, Josko Gvardiol (24), ameibuka kuwa chaguo kuu la Jose Mourinho kwa ajili ya kuimarisha safu ya ulinzi ya Real Madrid.

    Kocha wa zamani wa Manchester United, Ruben Amorim (41), anawindwa na AC Milan, ambao wanaamini anaweza kuleta nguvu mpya katika timu hiyo.

    Barcelona inatarajiwa kukataa fursa ya kumsajili mshambuliaji wa Manchester United Marcus Rashford (28) kwa ada yake ya kuachiliwa ya pauni milioni 26, huku kipengele hicho kikitarajiwa kuisha muda wake Jumatatu.

    Manchester United pia inaweza kuelekeza nguvu zake kwa kiungo wa Lens, Mamadou Sangare (23), baada ya kushindwa kumudu gharama za kumsajili kiungo wa England Elliot Anderson (23) kutoka Nottingham Forest.

    Beki wa Borussia Dortmund na Ujerumani, Nico Schlotterbeck (26), ameweka pembeni mawazo ya kuhamia Real Madrid ili kuzingatia kwanza FIFA World Cup.

    Trabzonspor inataka kukamilisha usajili wa moja kwa moja wa mlinda lango wa Cameroon wa Manchester United, Andre Onana (30), msimu huu wa kiangazi.

    Manchester United pia inatafuta kuwaondoa mlinda lango Altay Bayindir (28) wa Uturuki na Radek Vitek (22) wa Czech Republic, ambaye alikuwa kwa mkopo katika Bristol City msimu uliopita.

    Sunderland imejiunga na mbio za kumsajili mshambuliaji chipukizi wa Bosnia, Kerim Alajbegovic (18), kutoka Red Bull Salzburg.

    Wolverhampton Wanderers inaweza kuvutiwa kumrejesha mshambuliaji wa West Ham United, Pablo (22), kufanya kazi tena na kocha mpya Cesar Peixoto, ambaye aliwahi kufanya naye kazi Gil Vicente FC.

    Real Madrid inatafuta kumtoa kwa mkopo mshambuliaji wa Argentina Franco Mastantuono (18) kwenda Juventus.

    Unaweza kusoma;

  3. Vance asema Waziri Mkuu wa Israel Netanyahu ‘amekosea katika baadhi ya mambo’

    Vance

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Makamu wa Rais wa Marekani, JD Vance, amesema kwamba Waziri Mkuu wa Israel, Benjamin Netanyahu, "bila shaka amekosea katika baadhi ya mambo", huku uhusiano kati ya washirika hao wawili katika vita dhidi ya Iran ukionekana kuwa na msukosuko katika wiki za hivi karibuni.

    Ingawa Vance hakutoa mifano maalumu, aliiambia CBS News kwamba Netanyahu "anapigania kwa nguvu maslahi ya nchi yake", lakini maslahi hayo si mara zote yanalingana na yale ya Marekani.

    Kauli zake zinaashiria waziwazi zaidi kwamba uhusiano kati ya washirika hao wa muda mrefu umekuwa ukikabiliwa na changamoto hivi karibuni.

    Hivi karibuni, Rais wa Marekani Donald Trump anaripotiwa kutofautiana na Netanyahu kuhusu hatua za kijeshi za Israel nchini Lebanon, ambazo zilisababisha mashambulizi mapya na kutishia juhudi za mazungumzo ya amani na Iran.

    Marekani na Iran zilirushiana mashambulizi kwa siku ya pili mfululizo usiku kucha, jambo lililoongeza shinikizo kwenye makubaliano ya kusitisha mapigano yaliyokuwepo tangu mwezi Aprili.

    Hali hiyo ilikuja baada ya Trump kusema kwamba Tehran ilikuwa imechukua "muda mrefu sana kufikia makubaliano" ya kumaliza vita. Hata hivyo, kuongezeka kwa mapigano kulichochewa na matukio nchini Lebanon, ambako Israel imeendelea na operesheni dhidi ya Hezbollah, kundi linaloungwa mkono na Iran.

    Wiki iliyopita, Trump alimwambia mwandishi wa habari wa Axios kwamba alimwita Netanyahu "mwendawazimu kabisa" katika mazungumzo ya simu, akisema alikuwa amekerwa na "kupigana kwake mara kwa mara na Lebanon."

    Katika mahojiano yanayotarajiwa kurushwa hewani Jumapili, Vance alisema:

    "Waziri Mkuu Netanyahu, anaongoza nchi ambayo kwa hakika imekuwa mshirika wa karibu sana wa Marekani."

    Hata hivyo, aliongeza kuwa Marekani na Israel si lazima zikubaliane katika kila suala la sera au hatua za kijeshi, licha ya ushirikiano wao wa muda mrefu.

    Unaweza kusoma;

  4. SpaceX ya Elon Musk yapata dola bilioni 75 kabla ya kuanza kuuzwa katika soko la hisa

    Space X

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Space X imepata uwekezaji wa dola bilioni 75 (takribani pauni bilioni 56) kutoka kwa taasisi za kifedha kabla ya kuanza kuuzwa katika soko la hisa kwa umma siku ya Ijumaa, katika kile kinachotarajiwa kuwa uorodheshaji wa hisa wenye thamani kubwa zaidi katika historia.

    Katika nyaraka zilizowasilishwa kwa U.S. Securities and Exchange Commission (SEC), kampuni hiyo ya safari za anga za juu na akili mnemba imeuza hisa zenye thamani ya dola bilioni 75 kwa bei ya dola 135 kwa kila hisa.

    Bei hiyo ya hisa inalingana na makadirio ambayo SpaceX ilitoa wiki iliyopita, jambo linaloweka thamani ya awali ya kampuni hiyo sokoni kufikia karibu dola trilioni 1.8.

    Kwa thamani hiyo, mtendaji mkuu wa kampuni hiyo, Elon Musk, ambaye tayari ndiye mtu tajiri zaidi duniani, anatarajiwa kuwa mtu wa kwanza duniani kufikia utajiri wa dola trilioni moja.

    Mara tu hisa zitakapoanza kuuzwa sokoni, thamani yake inaweza kupanda au kushuka kulingana na idadi ya hisa zitakazopatikana kwa ajili ya kuuzwa na kiwango cha mahitaji kutoka kwa wanunuzi.

    Ikiwa hisa za kampuni zitauzwa kwa dola 135 au zaidi wakati biashara itakapoanza siku ya Ijumaa, SpaceX itakuwa mara moja miongoni mwa kampuni zenye thamani kubwa zaidi duniani zinazouzwa hadharani katika soko la hisa.

    Hata hivyo, ni jukumu la wawekezaji kuamua kama wanaamini hisa hizo zina thamani hiyo.

    Maslahi ya kununua sehemu ya umiliki wa SpaceX miongoni mwa mifuko ya uwekezaji na wawekezaji binafsi (wanaojulikana kama retail investors) yanatarajiwa kuwa makubwa sana.

  5. Trump asema makubaliano ya kumaliza vita na Iran yako karibu baada ya kusitisha mashambulizi

    Trump

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Rais wa Marekani, Donald Trump, amedai kuwa makubaliano ya awali yanayolenga kumaliza vita na Iran yako karibu kufikiwa, baada ya kutangaza kuwa amefuta mashambulizi yaliyokuwa yamepangwa dhidi ya nchi hiyo.

    "Ndiyo kwanza tumefikia makubaliano mazuri kuhusu vita na Iran," aliwaambia waandishi wa habari ofisini kwake siku ya Alhamisi.

    Hata hivyo, msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran, Esmail Baghaei, aliiambia televisheni ya taifa kwamba taarifa za kuwepo kwa makubaliano ni "za kubahatisha" na kwamba "hakuna jambo lolote lililokamilishwa."

    Trump amewahi kutoa madai kama hayo hapo awali kwamba Marekani na Iran ziko karibu kufikia makubaliano ya kumaliza mzozo huo. Saa chache kabla ya tangazo hilo, alikuwa ametishia kuishambulia Iran "kwa nguvu kubwa sana."

    Marekani na Israel zilianzisha mashambulizi makubwa dhidi ya Iran tarehe 28 Februari. Iran ilijibu kwa kushambulia Israel na mataifa washirika wa Marekani katika eneo la Ghuba, na kwa kiasi kikubwa kufunga mlango bahari wa Hormuz, njia muhimu ya usafirishaji wa mafuta na gesi asilia duniani.

    Licha ya makubaliano ya kusitisha mapigano yaliyofikiwa mwezi Aprili, Marekani na Iran zimeendelea kurushiana mashambulizi mara kwa mara, ikiwa ni pamoja na duru mbili za mashambulizi ya kulipizana kisasi wiki hii. Wakati huohuo, Trump ameendelea kuzungumzia uwezekano wa kufikiwa kwa makubaliano na Iran.

    Unaweza kusoma;

  6. Habari za asubuhi, karibu katika taarifa zetu hii leo