Upinzani wataka raia kususia kutoka nje ishara ya kupinga jaribio la kurekebisha Katiba DRC
Viongozi wa upinzani nchini Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo wamewataka wananchi kushiriki katika mgomo wa kutotoka mijini leo Jumatano, ili kupinga kile wanachokieleza kuwa ni vitisho dhidi ya Katiba ya nchi hiyo.
Hatua hiyo inakuja wakati bunge likijadili mswada wa kura ya maoni, ambao wachambuzi wanasema unaweza kufungua njia ya uwezekano wa kuongeza muda wa utawala wa Rais Félix Tshisekedi.
Viongozi mashuhuri wa upinzani kama vile Moïse Katumbi na Martin Fayulu walioshika nafasi ya pili na ya tatu mtawalia katika uchaguzi wa rais wa 2023, wanasema wanapinga jaribio lolote la kubadilisha katiba ya sasa, ambayo inaruhusu mihula miwili ya miaka mitano kila mmoja.
Katika matamko tofauti, waliwataka raia kukaa nyumbani Jumatano, na kuongeza kwamba shule, majengo ya biashara na huduma za umma zinapaswa kufungwa kama kielelezo cha wao kupinga.
"Mtu yeyote asitoke nje, ili kuonesha kwamba tunapinga ukoloni wa nchi yetu, mabadiliko ya Katiba, na kukataa kuruhusu mtu kubaki madarakani milele," Fayulu alisema katika ujumbe wa video kwa wafuasi wake.
Mamlaka za DRC ziliwataka watu - hasa watumishi wa umma - kutotii wito kama huo wa kususia.
"Wasimamizi na wafanyakazi ambao, katika kipindi husika...hawapo wenyewe kwenye vituo vyao vya kazi bila uhalali watakabiliwa na sheria kwa mujibu wa kanuni zinazotumika," Jean-Pierre Lihau Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Utumisi wa Umma alisema katika taarifa kwa umma.
Pia alisisitizia uhitaji wa watumishi wa umma kutoegemea upande wowote kisiasa na kutopendelea.
Mwezi uliopita, Rais Felix Tshisekedi alisema yuko tayari kugombea muhula wa tatu iwapo "wananchi wanataka" abaki. Alisema ili hilo lifanyike, kutahitajika marekebisho ya katiba baada ya kura ya maoni. Rais pia alipendekeza kwamba mzozo wa mashariki mwa nchi unaweza kusababisha kucheleweshwa kwa uchaguzi wa 2028, na kuzua hasira miongoni mwa upinzani.
Wengi wanasema anapanga mkakati wa kusalia madarakani, huku wabunge wa upinzani wakiondoka kwenye kikao cha bunge cha Mei 27, kilichokusudiwa kujadili muswada wa kura ya maoni.
Kilichosalia ni kusubiri kuona iwapo watu wataitikia miito ya upinzani.
Pia unaweza kusoma: