UAE iliwazuia mabahari 10 wa Iran kurejea nyumbani - Iran

Chanzo cha picha, Sailor provided to BBC News
Iran imesema mamlaka za Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) zilizuia kurejea kwa mabaharia 10 wa Iran waliokuwa wanashikiliwa nchini humo, licha ya maandalizi yote ya safari yao kukamilika.
Kwa mujibu wa Ofisi ya mwakilishi wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran katika mkoa wa Hormozgan, tiketi za kurejea Bandar Abbas zilikuwa tayari zimetolewa na uratibu wote muhimu ulikuwa umefanyika kati ya maafisa wa Iran na UAE.
Hata hivyo, ofisi hiyo ilisema kuwa katika dakika za mwisho, upande wa UAE ulisitisha kuondoka kwa wavuvi hao bila kutoa sababu yoyote rasmi.
"Tiketi za kurejea Bandar Abbas kwa ajili ya mabaharia waliokamatwa UAE zilikuwa zimetolewa, na uratibu wote muhimu ulikuwa umefanyika kwa ajili ya kurejea kwao. Hata hivyo, katika dakika za mwisho, upande wa UAE ulizuia kuondoka kwa raia hao wa Hormozgan bila kutoa sababu ya msingi," taarifa hiyo ilisema.
Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran imesema wmabahariai hao 10, ambao waliripotiwa kupotea katika maji ya Ghuba ya Uajemi wiki chache zilizopita, wako hai na wako nchini UAE.
Mamlaka za Iran zilisema zinatarajia mabaharia hao kurejea nyumbani hivi karibuni.
Habari za kupotea kwao zilianza kuripotiwa mwishoni mwa mwezi Agosti. Mashuhuda waliiambia Iran News Network kwamba mabaharia hao walionekana mara ya mwisho karibu na Kisiwa cha Siri.
Kisiwa hicho ni miongoni mwa visiwa vya kusini mwa Iran vilivyopo katika Ghuba ya Uajemi, karibu na Kisiwa cha Abu Musa.
Wakati huo, Shirika la Utangazaji la Iran liliripoti kuwa kuvuka bila ruhusa katika maji ya nchi jirani ni tukio linalojitokeza mara kwa mara kwa baadhi ya mabaharia katika eneo hilo. Hata hivyo, lilisema hali ya mvutano wa kikanda ilikuwa imeongeza wasiwasi kuhusu usalama wao.



































