Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Moja kwa moja, “Kwa nini tupigane ikiwa tunaweza kuzungumza?” – Rais wa Iran

Kwa upande mwingine, afisa mmoja wa Marekani ameiambia Reuters kuwa kumekuwa na maendeleo mazuri katika mazungumzo kati ya Iran na Oman kuhusu Mlango Bahari wa Hormuz, huku Washington ikitarajia makubaliano kufikiwa hivi karibuni.

Moja kwa moja

Na Abdalla Seif Dzungu

  1. Besigye arejeshwa gerezani Luzira licha ya utata wa hali yake ya kiafya

    Kiongozi wa muda mrefu wa upinzani nchini Uganda, Dk Kizza Besigye, amerudishwa katika gereza la Luzira kutoka Hospitali ya Taifa ya Rufaa ya Mulago, hatua ambayo imezua malalamiko kutoka kwa familia yake na wafuasi wa kisiasa.

    Besigye, ambaye amewahi kugombea urais mara nne, alilazwa hospitalini baada ya kuanguka akiwa mahakamani tarehe 29 Julai wakati akiendelea na kesi yake ya uhaini. Kwa mujibu wa familia yake, bado alikuwa katika hali dhaifu na hakuweza kutembea wala kuzungumza vizuri aliporejeshwa gerezani.

    Kwa mujibu wa Monitor, Mke wake, Winnie Byanyima, amesema madaktari walikuwa na wasiwasi kuhusu hali yake na kwamba maafisa wa magereza walikuwa wameeleza awali kuwa gereza la Luzira halikuwa na uwezo wa kutoa huduma ya afya aliyohitaji. Amesema uamuzi wa kumrudisha gerezani ulifuatia ziara ya Waziri wa Afya, Chris Baryomunsi, hospitalini.

    Hata hivyo, Baryomunsi alisema baada ya kumtembelea Besigye kuwa mwanasiasa huyo alikuwa akiendelea kuimarika na akamtakia apone haraka. Kauli hiyo inapingana na madai ya familia yake na chama chake cha People’s Front for Freedom, ambacho kimetaka aachiliwe na apelekwe nje ya nchi kwa matibabu maalumu.

    Besigye anashikiliwa kwa tuhuma za uhaini na kushindwa kutoa taarifa kuhusu njama ya uhaini, pamoja na washtakiwa wengine wawili. Serikali inamtuhumu kupanga njama ya kuipindua serikali kwa nguvu kati ya mwaka 2023 na Novemba 2024. Kesi yake ilihamishiwa Mahakama Kuu baada ya Mahakama ya Juu kuamua kwamba raia hawapaswi kushtakiwa katika mahakama za kijeshi alikopelekwa awali.

  2. Guimaraes ‘aliililia Arsenal’, hatukutaka aondoke - Newcastle

    Mkurugenzi wa michezo wa Newcastle United, Ross Wilson, amesema klabu hiyo haikupanga kumuuza nahodha wake Bruno Guimaraes, lakini kiungo huyo mwenye umri wa miaka 28 alitaka kujiunga na Arsenal.

    Mabingwa hao wa Ligi Kuu ya England wanatarajiwa kukamilisha usajili wa Guimaraes kwa ada ya pauni milioni 75, baada ya mazungumzo kati ya klabu hizo kukamilika, ikielezwa na vipimo vya afya ameshafanya.

    Ingawa Wilson amesema ilikuwa "jambo la kukatisha tamaa" kumuona Guimaraes akiondoka, amesisitiza kuwa mchezaji huyo hakutaka tena kuendelea kuichezea Newcastle.

    "Kwa heshima kubwa kwa Bruno kutokana na namna alivyotueleza, na pia kwa hisia nyingi, alituambia wazi kwamba alitaka kuondoka na kuendelea na maisha yake," Wilson alisema.

    Aliongeza kuwa kutaka kwa mchezaji kuondoka hakumaanishi moja kwa moja kwamba klabu itamuuza, lakini hali hiyo ilizingatiwa wakati Newcastle ilipokuwa ikifikiria kiwango cha ada ambacho ingekubali.

    Wilson amesema kumuuza Guimaraes haikuwa sehemu ya mkakati wa Newcastle katika dirisha hili la usajili.

    Guimaraes aliagana na wachezaji wenzake kwa hisia pamoja na wafanyakazi wa Newcastle kabla ya kuondoka kwenye kambi ya maandalizi ya msimu nchini Hispania.

    Ataondoka Newcastle akiwa mchezaji muhimu wa nne kuondoka ndani ya kipindi cha chini ya mwaka mmoja. Sandro Tonali (Tottenham Hotspur) na Anthony Gordon ( Barcelona) wameondoka katika dirisha hili, huku Alexander Isak akijiunga na Liverpool msimu uliopita.

    Kuondoka kwa Guimaraes ni pigo kubwa kwa Newcastle kutokana na nafasi yake kama mmoja wa wachezaji muhimu zaidi wa klabu hiyo.

  3. Rais wa Iran: Kwa nini tupigane ikiwa tunaweza kupata haki zetu kwa mazungumzo?

    Rais wa Iran, Masoud Pezeshkian, ametetea kuendelea kwa mazungumzo na Marekani, akisema Iran inaweza kupata haki zake kupitia diplomasia badala ya kuendelea na vita.

    Akizungumza katika hafla ya kuadhimisha miaka miwili tangu aingie madarakani, Pezeshkian aliuliza: “Kwa nini tupigane ikiwa tunaweza kupata haki zetu kupitia mazungumzo?”

    Hata hivyo, amesema Iran haitarudi nyuma katika misimamo yake, akidai kuwa kuendelea kwa vita ndilo chaguo ambalo Israel inataka ili kuilazimisha Iran kujisalimisha.

    Pezeshkian amesema mazungumzo yaliyopita yalisaidia kumaliza vita nchini Lebanon, kuondoa vizuizi na kupunguza baadhi ya vikwazo vilivyowekwa dhidi ya Iran.

    Amesema pia Spika wa Bunge la Iran, Mohammad Baqer Qalibaf, amekubali kujiunga na ujumbe wa Iran unaoshiriki katika mazungumzo hayo. Ujumbe huo pia unajumuisha wawakilishi kutoka mahakama, bunge, jeshi na taasisi nyingine za nchi hiyo.

    Kwa mujibu wa Pezeshkian, muundo huo unalenga kuonyesha kwamba “sote tuko upande mmoja” katika mazungumzo hayo.

    Kauli hiyo imekuja wakati mazungumzo kuhusu mustakabali wa Mlango Bahari wa Hormuz yakiendelea kati ya Iran na Oman.

    Afisa mmoja wa Marekani ameiambia Reuters kuwa kumekuwa na maendeleo katika mazungumzo hayo na kwamba Washington inatarajia makubaliano kufikiwa hivi karibuni. Kwa mujibu wa afisa huyo, Marekani inaweza kuondoa kizuizi katika bandari za Iran baada ya makubaliano hayo kutangazwa.

    Pezeshkian pia amekosoa watu anaodai wanazungumza kuhusu masuala ya kisiasa, kiuchumi na kijamii bila kuwa na taarifa kamili, akisema kufanya hivyo kunaweza “kuipotosha jamii.”

    Rais huyo amesema Iran pia imefanikiwa kukabiliana na juhudi za wapinzani wake za kuidhoofisha au kuivuruga nchi kupitia shinikizo la kijeshi.