Besigye arejeshwa gerezani Luzira licha ya utata wa hali yake ya kiafya
Kiongozi wa muda mrefu wa upinzani nchini Uganda, Dk Kizza Besigye, amerudishwa katika gereza la Luzira kutoka Hospitali ya Taifa ya Rufaa ya Mulago, hatua ambayo imezua malalamiko kutoka kwa familia yake na wafuasi wa kisiasa.
Besigye, ambaye amewahi kugombea urais mara nne, alilazwa hospitalini baada ya kuanguka akiwa mahakamani tarehe 29 Julai wakati akiendelea na kesi yake ya uhaini. Kwa mujibu wa familia yake, bado alikuwa katika hali dhaifu na hakuweza kutembea wala kuzungumza vizuri aliporejeshwa gerezani.
Kwa mujibu wa Monitor, Mke wake, Winnie Byanyima, amesema madaktari walikuwa na wasiwasi kuhusu hali yake na kwamba maafisa wa magereza walikuwa wameeleza awali kuwa gereza la Luzira halikuwa na uwezo wa kutoa huduma ya afya aliyohitaji. Amesema uamuzi wa kumrudisha gerezani ulifuatia ziara ya Waziri wa Afya, Chris Baryomunsi, hospitalini.
Hata hivyo, Baryomunsi alisema baada ya kumtembelea Besigye kuwa mwanasiasa huyo alikuwa akiendelea kuimarika na akamtakia apone haraka. Kauli hiyo inapingana na madai ya familia yake na chama chake cha People’s Front for Freedom, ambacho kimetaka aachiliwe na apelekwe nje ya nchi kwa matibabu maalumu.
Besigye anashikiliwa kwa tuhuma za uhaini na kushindwa kutoa taarifa kuhusu njama ya uhaini, pamoja na washtakiwa wengine wawili. Serikali inamtuhumu kupanga njama ya kuipindua serikali kwa nguvu kati ya mwaka 2023 na Novemba 2024. Kesi yake ilihamishiwa Mahakama Kuu baada ya Mahakama ya Juu kuamua kwamba raia hawapaswi kushtakiwa katika mahakama za kijeshi alikopelekwa awali.