Moja kwa moja, “Kwa nini tupigane ikiwa tunaweza kuzungumza?” – Rais wa Iran

Kwa upande mwingine, afisa mmoja wa Marekani ameiambia Reuters kuwa kumekuwa na maendeleo mazuri katika mazungumzo kati ya Iran na Oman kuhusu Mlango Bahari wa Hormuz, huku Washington ikitarajia makubaliano kufikiwa hivi karibuni.

Moja kwa moja

Na Abdalla Seif Dzungu

  1. Guimaraes ‘aliililia Arsenal’, hatukutaka aondoke - Newcastle

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Mkurugenzi wa michezo wa Newcastle United, Ross Wilson, amesema klabu hiyo haikupanga kumuuza nahodha wake Bruno Guimaraes, lakini kiungo huyo mwenye umri wa miaka 28 alitaka kujiunga na Arsenal.

    Mabingwa hao wa Ligi Kuu ya England wanatarajiwa kukamilisha usajili wa Guimaraes kwa ada ya pauni milioni 75, baada ya mazungumzo kati ya klabu hizo kukamilika, ikielezwa na vipimo vya afya ameshafanya.

    Ingawa Wilson amesema ilikuwa "jambo la kukatisha tamaa" kumuona Guimaraes akiondoka, amesisitiza kuwa mchezaji huyo hakutaka tena kuendelea kuichezea Newcastle.

    "Kwa heshima kubwa kwa Bruno kutokana na namna alivyotueleza, na pia kwa hisia nyingi, alituambia wazi kwamba alitaka kuondoka na kuendelea na maisha yake," Wilson alisema.

    Aliongeza kuwa kutaka kwa mchezaji kuondoka hakumaanishi moja kwa moja kwamba klabu itamuuza, lakini hali hiyo ilizingatiwa wakati Newcastle ilipokuwa ikifikiria kiwango cha ada ambacho ingekubali.

    Wilson amesema kumuuza Guimaraes haikuwa sehemu ya mkakati wa Newcastle katika dirisha hili la usajili.

    Guimaraes aliagana na wachezaji wenzake kwa hisia pamoja na wafanyakazi wa Newcastle kabla ya kuondoka kwenye kambi ya maandalizi ya msimu nchini Hispania.

    Ataondoka Newcastle akiwa mchezaji muhimu wa nne kuondoka ndani ya kipindi cha chini ya mwaka mmoja. Sandro Tonali (Tottenham Hotspur) na Anthony Gordon ( Barcelona) wameondoka katika dirisha hili, huku Alexander Isak akijiunga na Liverpool msimu uliopita.

    Kuondoka kwa Guimaraes ni pigo kubwa kwa Newcastle kutokana na nafasi yake kama mmoja wa wachezaji muhimu zaidi wa klabu hiyo.

  2. Rais wa Iran: Kwa nini tupigane ikiwa tunaweza kupata haki zetu kwa mazungumzo?

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Rais wa Iran, Masoud Pezeshkian, ametetea kuendelea kwa mazungumzo na Marekani, akisema Iran inaweza kupata haki zake kupitia diplomasia badala ya kuendelea na vita.

    Akizungumza katika hafla ya kuadhimisha miaka miwili tangu aingie madarakani, Pezeshkian aliuliza: “Kwa nini tupigane ikiwa tunaweza kupata haki zetu kupitia mazungumzo?”

    Hata hivyo, amesema Iran haitarudi nyuma katika misimamo yake, akidai kuwa kuendelea kwa vita ndilo chaguo ambalo Israel inataka ili kuilazimisha Iran kujisalimisha.

    Pezeshkian amesema mazungumzo yaliyopita yalisaidia kumaliza vita nchini Lebanon, kuondoa vizuizi na kupunguza baadhi ya vikwazo vilivyowekwa dhidi ya Iran.

    Amesema pia Spika wa Bunge la Iran, Mohammad Baqer Qalibaf, amekubali kujiunga na ujumbe wa Iran unaoshiriki katika mazungumzo hayo. Ujumbe huo pia unajumuisha wawakilishi kutoka mahakama, bunge, jeshi na taasisi nyingine za nchi hiyo.

    Kwa mujibu wa Pezeshkian, muundo huo unalenga kuonyesha kwamba “sote tuko upande mmoja” katika mazungumzo hayo.

    Kauli hiyo imekuja wakati mazungumzo kuhusu mustakabali wa Mlango Bahari wa Hormuz yakiendelea kati ya Iran na Oman.

    Afisa mmoja wa Marekani ameiambia Reuters kuwa kumekuwa na maendeleo katika mazungumzo hayo na kwamba Washington inatarajia makubaliano kufikiwa hivi karibuni. Kwa mujibu wa afisa huyo, Marekani inaweza kuondoa kizuizi katika bandari za Iran baada ya makubaliano hayo kutangazwa.

    Pezeshkian pia amekosoa watu anaodai wanazungumza kuhusu masuala ya kisiasa, kiuchumi na kijamii bila kuwa na taarifa kamili, akisema kufanya hivyo kunaweza “kuipotosha jamii.”

    Rais huyo amesema Iran pia imefanikiwa kukabiliana na juhudi za wapinzani wake za kuidhoofisha au kuivuruga nchi kupitia shinikizo la kijeshi.