Guimaraes ‘aliililia Arsenal’, hatukutaka aondoke - Newcastle

Chanzo cha picha, Getty Images
Mkurugenzi wa michezo wa Newcastle United, Ross Wilson, amesema klabu hiyo haikupanga kumuuza nahodha wake Bruno Guimaraes, lakini kiungo huyo mwenye umri wa miaka 28 alitaka kujiunga na Arsenal.
Mabingwa hao wa Ligi Kuu ya England wanatarajiwa kukamilisha usajili wa Guimaraes kwa ada ya pauni milioni 75, baada ya mazungumzo kati ya klabu hizo kukamilika, ikielezwa na vipimo vya afya ameshafanya.
Ingawa Wilson amesema ilikuwa "jambo la kukatisha tamaa" kumuona Guimaraes akiondoka, amesisitiza kuwa mchezaji huyo hakutaka tena kuendelea kuichezea Newcastle.
"Kwa heshima kubwa kwa Bruno kutokana na namna alivyotueleza, na pia kwa hisia nyingi, alituambia wazi kwamba alitaka kuondoka na kuendelea na maisha yake," Wilson alisema.
Aliongeza kuwa kutaka kwa mchezaji kuondoka hakumaanishi moja kwa moja kwamba klabu itamuuza, lakini hali hiyo ilizingatiwa wakati Newcastle ilipokuwa ikifikiria kiwango cha ada ambacho ingekubali.
Wilson amesema kumuuza Guimaraes haikuwa sehemu ya mkakati wa Newcastle katika dirisha hili la usajili.
Guimaraes aliagana na wachezaji wenzake kwa hisia pamoja na wafanyakazi wa Newcastle kabla ya kuondoka kwenye kambi ya maandalizi ya msimu nchini Hispania.
Ataondoka Newcastle akiwa mchezaji muhimu wa nne kuondoka ndani ya kipindi cha chini ya mwaka mmoja. Sandro Tonali (Tottenham Hotspur) na Anthony Gordon ( Barcelona) wameondoka katika dirisha hili, huku Alexander Isak akijiunga na Liverpool msimu uliopita.
Kuondoka kwa Guimaraes ni pigo kubwa kwa Newcastle kutokana na nafasi yake kama mmoja wa wachezaji muhimu zaidi wa klabu hiyo.

