Moja kwa moja, Jeshi la Marekani lasema limedungua ndege mbili zisizo na rubani za Iran katika Mlango wa Hormuz

Taarifa hiyo pia imesema kuwa vikosi vya Marekani vinaendelea kubaki katika maeneo yao ya operesheni na viko tayari kuendelea kujilinda dhidi ya kile ilichokiita uchokozi wa Iran.

Moja kwa moja

Na Mariam Mjahid

  1. Korea Kaskazini yasema mpango wake wa nyuklia hauko kwenye mazungumzo

    g

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Kim Yo-jong, dada wa kiongozi wa Korea Kaskazini Kim Jong-un, amesema katika taarifa kwamba mpango wa nyuklia wa nchi hiyo “hauwezi kujadiliwa kabisa”.

    “Taasisi yetu kuhusu nguvu za nyuklia haiwezi kujadiliwa kwa namna yoyote,” alisema katika taarifa hiyo iliyochapishwa na gazeti rasmi la chama tawala, Rodong Sinmun.

    Aliongeza pia kuwa Korea Kaskazini “haitavumilia vitisho vyovyote”.

    Kim Yo-jong, ambaye ni mmoja wa viongozi muhimu katika masuala ya mawasiliano na sera za nje za Korea Kaskazini, ameoa kauli hizo kabla ya ziara ya Rais wa China Xi Jinping nchini Korea Kaskazini, inayotarajiwa kuanza Jumatatu na kuendelea hadi Jumanne, kwa mujibu wa vyombo vya habari vya serikali.

    Ziara hiyo ya Xi Jinping mjini Pyongyang itakuwa ya kwanza katika kipindi cha miaka saba.

    Hii inakuja baada ya rais huyo wa China kufanya mfululizo wa mikutano na Rais wa Marekani Donald Trump na Rais wa Urusi Vladimir Putin mwezi uliopita.

    China inachukuliwa kuwa mmoja wa washirika muhimu zaidi wa kisiasa na kiuchumi wa Korea Kaskazini.

    Soma zaidi:

  2. Rais Tshisekedi amtunuku Fally Ipupa tuzo ya kitaifa kwa kuitangaza Congo kimataifa

    m

    Chanzo cha picha, PRESIDENCE RDC/X

    Rais Félix Tshisekedi amemtunuku mwanamuziki wa Congo Fally Ipupa nishani ya kitaifa kufuatia mafanikio yake ya kihistoria ya kufanya maonesho mawili mwezi Mei katika Stade de France jijini Paris.

    Fally Ipupa amekuwa msanii wa kwanza wa Afrika anayezungumza Kifaransa na kuishi barani Afrika kuwa msanii mkuu wa tamasha katika uwanja huo maarufu.

    Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Rais Tshisekedi alisema heshima hiyo haitambui msanii pekee bali pia “safari yake, nidhamu, uthabiti, bidii, sauti yake, umahiri wa jukwaani na uwezo wa kipekee wa kubeba roho ya Wakongo kuvuka mipaka ya kijiografia.”

    “Kupitia muziki wako, sehemu ya Congo inasafiri, inavutia, inaunganisha watu na kuzungumza na ulimwengu,” alisema Rais Tshisekedi.

    Rais huyo pia amewapa heshima magwiji waliochangia kujenga hadhi ya muziki wa Congo kimataifa, akiwemo Papa Wemba, Jossart N’Yoka Longo, Koffi Olomide, Werrason, JB Mpiana na Ferré Gola, akisema kila mmoja ameendelea kuitangaza nchi kwa mtindo wake na hadhira yake.

    Alisisitiza kuwa tuzo hiyo “haiweki daraja kati ya vipaji tofauti wala haimfungii yeyote mlango. Kinyume chake, inafungua njia ya Jamhuri inayojua kuwaheshimu mabinti na wanawe wanapoitumikia taifa kwa ubora, umaarufu na uwezo wa kuhamasisha wengine.”

    Jumatano, amri ya rais ilisomwa kupitia televisheni ya taifa ikitangaza kupandishwa hadhi kwa Fally Ipupa katika Daraja la Taifa la Heshima, hatua iliyotekeleza ahadi iliyotolewa na mkuu huyo wa nchi wakati wa mkutano na waandishi wa habari tarehe 6 Mei 2026.

  3. Marekani yataka mali za Iran zitumike kufidia washirika wake wa Ghuba

    f

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Vyombo vya habari vya Marekani vimeripoti kuwa Waziri wa Hazina wa nchi hiyo, Scott Bessent, anazingatia uwezekano wa kutumia mali za Iran zilizozuiwa kufidia uharibifu unaodaiwa kusababishwa na mashambulizi ya Iran dhidi ya mataifa ya Kiarabu katika eneo la Ghuba ya Uajemi.

    Kwa mujibu wa ripoti hizo, ambazo bado hazijathibitishwa rasmi, Bessent pia ameagiza timu ya wataalamu kufanya tathmini ya gharama za ukarabati wa miundombinu na mali zilizoharibiwa katika mashambulizi hayo.

    Kwa upande wake, Iran inaitaka Marekani kuachilia zaidi ya dola bilioni 20 za mali zake zilizowekwa zuio.

    Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran, Kazem Gharibabadi, ambaye pia ni mjumbe wa timu ya mazungumzo kati ya Tehran na Washington, amesema kuwa:

    "Jamhuri ya Kiislamu ya Iran inasisitiza kuwa asilimia 50 ya mali zake zilizowekewa zuio zitolewe mara moja baada ya kutiwa saini kwa hati ya makubaliano."

    Pendekezo la kutumia mali za Iran zilizowekewa zuio kufidia uharibifu wa vita katika mataifa washirika wa Marekani linaonekana kufanana na mapendekezo yaliyowahi kutolewa ya kutumia mali za Urusi zilizozuiwa kugharamia ujenzi upya wa Ukraine kufuatia vita vya nchi hiyo na Urusi.

    Pia unaweza kusoma:

  4. Tetesi za soka Ulaya: PSG yajiunga na Arsenal kumwinda Gibbs-White

    g

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Arsenal F.C. huenda ikakumbana na ushindani mkali kutoka kwa Paris Saint-Germain katika harakati za kumsajili kiungo mshambuliaji wa Nottingham Forest F.C., Morgan Gibbs-White.

    Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 26 yuko kwenye orodha ya Arsenal kama mbadala anayetarajiwa wa nyota wa Aston Villa F.C., Morgan Rogers, mwenye umri wa miaka 23.

    Hata hivyo, PSG pia inafuatilia kwa karibu hali yake.

    Wakati huo huo, inaelezwa kuwa winga wa Georgia wa PSG, Khvicha Kvaratskhelia, ndiye mchezaji ambaye rais wa Real Madrid C.F., Florentino Pérez, anapanga kumsajili iwapo atashinda uchaguzi wa urais wa klabu hiyo. (Teamtalk).

    Kocha mpya wa Real Madrid, José Mourinho, naye anaripotiwa kutaka huduma za kiungo wa Ureno Bernardo Silva baada ya nyota huyo kuondoka Manchester City F.C. mwishoni mwa msimu. (AS - in Spanish)

    Kwa upande mwingine, wakala wa Jürgen Klopp amesema Mjerumani huyo hana mpango wa kurejea kufundisha klabu yoyote kwa sasa, baada ya mgombea wa urais wa Real Madrid, Enrique Riquelme, kudai angejaribu kumshawishi kujiunga na klabu hiyo endapo angechaguliwa. (Sky sports-Germany)

    Tottenham Hotspur F.C. bado ina nia ya kumsajili winga wa Brazil Savinho. Inadaiwa mchezaji huyo mwenye miaka 22 yuko tayari kushinikiza uhamisho huo baada ya Manchester City kukataa ofa ya Spurs msimu uliopita. (Mirror).

    Mshambuliaji wa Italia Federico Chiesa amesema anahitaji kupata muda zaidi wa kucheza akiwa Liverpool na atazungumza na kocha mpya wa Reds, Andoni Iraola, kabla ya kufanya uamuzi kuhusu mustakabali wake. (Gazzetta dello Sport - in Italian)

    Liverpool pia haina mpango wa kumuuza winga chipukizi wa England Rio Ngumoha mwenye miaka 17, licha ya taarifa kwamba FC Bayern Munich inamfuatilia kwa ajili ya usajili wa majira ya joto.(Sky Sports)

    Kwingineko, winga wa Newcastle United F.C., Harvey Barnes, ameibuka kulengwa kusajiliwa na Aston Villa. (Football Insider)

    Nazo Leeds United F.C. na Ipswich Town F.C. zinashindania saini ya kipa wa England Nick Pope kutoka Newcastle. (Sun)

    Aidha, kocha Russell Martin yuko katika mazungumzo ya hatua za mwisho na Leicester City F.C. huku akitafakari kurejea kwenye ukocha. (Telegraph - subscription required)

    Pia unaweza kusoma:

  5. Iran yadai maafisa wake wamezuiwa kuingia Marekani licha ya wachezaji kupewa visa vya Kombe la Dunia

    f

    Chanzo cha picha, TABNAK

    Iran imeishutumu Marekani kwa kuwanyima viza baadhi ya maafisa muhimu wa benchi la ufundi na uongozi wa timu yake ya taifa ya soka, saa chache baada ya Washington kuthibitisha kuwa wachezaji wa Iran wamepewa ruhusa ya kusafiri kushiriki Kombe la Dunia lijalo.

    Maafisa wa Marekani walisema Ijumaa kuwa viza zimetolewa kwa wachezaji wote pamoja na “wahudumu muhimu wa timu”, siku kumi kabla ya Iran kucheza mechi yake ya kwanza dhidi ya wapinzani wake mjini Los Angeles tarehe 15 Juni.

    Hata hivyo, maafisa hao waliongeza kuwa Iran haitaruhusiwa “kutumia vibaya mfumo huo kuwaingiza magaidi nchini Marekani kwa kisingizio cha ushiriki wa michezo”.

    Ubalozi wa Iran nchini Uturuki uliishutumu Marekani kwa kile ulichokiita “uingiliaji wa kisiasa wenye upendeleo katika michezo” baada ya kuwanyima viza sehemu kubwa ya viongozi wa timu, maafisa wa utawala na washauri wa kiufundi.

    Vyombo vya habari vinavyohusishwa na serikali ya Iran viliripoti kuwa maafisa 15 wa utawala, akiwemo rais wa shirikisho la soka la Iran, naibu wake na mkurugenzi wa habari, ni miongoni mwa waliozuiwa kuingia Marekani.

    Timu hiyo iliondoka katika kambi yake ya mazoezi nchini Uturuki siku ya Jumamosi kuelekea Mexico, ambako itakuwa imeweka makazi yake wakati wa mashindano hayo. Inatarajiwa kuwasili mapema Jumapili baada ya safari ya saa 20.

    Kwa mujibu wa masharti ya viza walivyopewa, wachezaji na maafisa watakaoruhusiwa kusafiri watalazimika kuingia na kuondoka Marekani siku hiyo hiyo ya mechi zao, kwa mujibu wa balozi wa Iran nchini Mexico.

    Katika taarifa yake, Iran ilielezea tangazo la Marekani kuwa ni “jaribio la kuficha ukweli”, ikisema: “Sasa mmefikisha kiwango cha juu kabisa cha matendo ya makusudi na ya kibaguzi dhidi ya timu ya taifa ya Iran.” Maafisa wa ubalozi wa Iran pia wameitaka FIFA kuingilia kati suala hilo.

    Kombe la Dunia la mwaka 2026, ambalo linaandaliwa kwa pamoja na Marekani, Canada na Mexico, linatarajiwa kuanza tarehe 11 Juni.

    Iran ilifuzu mashindano hayo baada ya kumaliza kinara wa kundi lake la kufuzu mwezi Machi 2025, karibu mwaka mmoja kabla ya kuzuka kwa vita.

    Pia unaweza kusoma:

  6. Kenya yaagiza waajiri kuwalipa wafanyakazi wa nyumbani angalau dola 140 kwa mwezi

    g

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Kanuni mpya za mishahara ya chini kwa wafanyakazi wa majumbani nchini Kenya zimeongeza kiwango cha chini cha mshahara wao wa kila mwezi hadi shilingi 18,047 za Kenya, sawa na takriban dola 140 za Marekani.

    Waajiri watakaokiuka masharti hayo wanakabiliwa na kifungo cha hadi miezi mitatu jela au faini ya shilingi 50,000 pesa za Kenya.

    Marekebisho hayo yanafuatia uamuzi wa hivi karibuni wa serikali wa kuongeza kiwango cha chini cha mshahara kwa asilimia 12, hatua inayolenga kuwasaidia wafanyakazi kukabiliana na ongezeko la gharama za maisha.

    Kwa mujibu wa gazeti la Daily Nation, viwango hivyo vipya vinawahusu maelfu ya wafanyakazi wa majumbani, wakiwemo wasaidizi wa nyumbani, walezi wa watoto, watunza bustani na wafanyakazi wengine wa huduma za nyumbani kote nchini.

    Chini ya muundo huo mpya wa mishahara, wafanyakazi wa majumbani katika miji mikuu ikiwemo Nairobi, Mombasa, Kisumu, Nakuru na Eldoret sasa wanastahili kulipwa angalau shilingi 18,047 kwa mwezi.

    Ongezeko hilo ni sehemu ya mageuzi mapana ya sekta ya ajira yanayolenga kuboresha ustawi wa wafanyakazi na kuimarisha utekelezaji wa sheria za kazi nchini Kenya.

    Hata hivyo, wakenya wameingia mitandaoni na kueleza kutoridhishwa kwao na agizo hilo mpya.

    Pia unaweza kusoma:

  7. Papa Leo aipongeza Uhispania kwa kupinga vita vinavyoendelea mashariki ya kati

    h

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Papa Leo XIV, kiongozi wa Kanisa Katoliki duniani, ameipongeza Uhispania kwa kile alichokitaja kuwa ni “kujitoa kwake kwa amani na umoja miongoni mwa mataifa” wakati wa ziara rasmi nchini humo siku ya Jumamosi.

    Serikali ya Uhispania imekuwa ikipinga vita vinavyoendelea katika Ukanda wa Gaza, Iran na Ukraine katika miaka ya karibuni.

    “Ninatoa shukrani zangu za dhati kwa taifa lenu, ambalo daima limezingatia sheria za kimataifa na mfumo wa ushirikiano wa kimataifa wa pande nyingi. Msimamo huu unaonesha wazi kujitolea kwake kwa amani na mshikamano kati ya mataifa,” Papa alisema wakati wa hafla ya mapokezi iliyofanyika katika Kasri la Kifalme mjini Madrid.

    Kauli hiyo imekuja huku Uhispania ikiendelea kusisitiza suluhu za kidiplomasia na kuheshimu sheria za kimataifa katika kushughulikia migogoro mbalimbali ya kimataifa.

    Soma zaidi:

  8. Jeshi la Marekani lasema limedungua ndege mbili zisizo na rubani za Iran katika Mlango wa Hormuz

    g

    Chanzo cha picha, AFP VIA Getty

    Kamandi Kuu ya Jeshi la Marekani katika Mashariki ya Kati (CENTCOM) imedai kuwa imedungua ndege mbili zisizo na rubani ambazo ilisema zilirushwa na Iran.

    Katika taarifa iliyochapishwa kwenye mtandao wa kijamii wa X, CENTCOM ilisema:

    "Vikosi vya Marekani katika Mashariki ya Kati vilidungua ndege mbili za mashambulizi zisizo na rubani za Iran ambazo zilikuwa zikitishia usafirishaji wa kimataifa katika Mlango wa Hormuz."

    Taarifa hiyo iliongeza kuwa vikosi vya Marekani vinaendelea kubaki katika maeneo yao ya operesheni na viko tayari kuendelea kujilinda dhidi ya kile ilichokitaja kuwa uchokozi wa Iran.

    Pia unaweza kusoma:

  9. Hujambo na karibu kwa matangazo yetu ya moja kwa moja ya tarehe 07 mwezi Juni 2026.