Mkuu wa Ujasusi Ecuador, Wamarekani 5 wafariki kwa ajali ya helikopta Kenya

Chanzo cha picha, Kenya Red Cross/Handout via Reuters
Serikali ya Ecuador imesema mkuu wake wa Idara ya Ujasusi na mke wake wamefariki dunia katika ajali ya helikopta iliyoanguka jana Jumatano katika kaunti ya Samburu nchini Kenya.
Raia watano wa Marekani pia walifariki dunia katika ajali hiyo, Msemaji wa Idara ya Mambo ya Nje ya Marekani alisema.
Mamlaka ya Usafiri wa Anga ya Kenya (KCAA) ilisema kuwa helikopta hiyo ilikuwa katika safari ya kutalii mandhari ikitoka kwenye hifadhi ya wanyamapori ya Loisaba kuelekea Ewaso Nyiro, mto unaopita kando ya hifadhi kadhaa za taifa.
Kaunti ya Samburu ni mojawapo ya maeneo maarufu ya utalii nchini Kenya, ikiwa na hifadhi nyingi za wanyamapori zinazomilikiwa na sekta binafsi, na inajulikana kwa mandhari yake ya kuvutia na ya kipekee.
Picha kutoka eneo la tukio zinaonesha moshi ukifuka katika eneo lenye miti ambapo helikopta hiyo ilianguka kwenye Mlima Ololokwe, huku wahudumu wa Shirika la Msalaba Mwekundu Kenya wakikaribia mabaki ya helikopta ambayo bado yalikuwa yakiteketea kwa moto.
Ecuador haijatoa maelezo kuhusu kifo cha Sensi-Contugi, mwenye umri wa miaka 44, ambaye aliteuliwa kuwa Mkurugenzi Mkuu wa Kituo cha Ujasusi wa Kimkakati mwaka 2024.






















