Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Moja kwa moja, Mazishi ya Ali Khamenei yaanza rasmi kwa kufunguliwa kwa msikiti wa Tehran

Ayatollah Ali Khamenei aliuawa pamoja na jamaa wanne wa familia yake mwanzoni mwa vita kati ya Marekani na Israel dhidi ya Iran.

Muhtasari

Moja kwa moja

Na Ambia Hirsi

  1. Jeshi Tanzania: Hatua kali zitachukuliwa dhidi ya watakaohusika na uvunjifu wa amani

    Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) limesema kuwa litachua hatua kali za kisheria dhidi ya watu watakaojihusisha na vitendo vinavyohamasisha vurugu na uvunjifu wa amani.

    Katika taarifa yake kwa umma, JWTZ imesema kuwa ina jukumu la kulinda usalama wa nchi na wananchi kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 pamoja na Sheria ya Ulinzi wa Taifa Sura ya 192.

    Jeshi hilo limeeleza kuwa litaendelea kushirikiana na vyombo vya dola kukabiliana na matukio yoyote ya vurugu, ghasia na uvunjifu wa amani.

    Aidha, wananchi wamehimizwa kutoa taarifa kwa viongozi wa vijiji, mitaa na vyombo vya ulinzi na usalama kuhusu viashiria vya uchochezi ili kudumisha utulivu nchini.JWTZ pia limewahakikishia wananchi kuwa litaendelea kutekeleza majukumu yake ya kulinda mipaka, Katiba na mamlaka ya nchi sambamba na kushirikiana na wananchi katika kuimarisha amani, umoja na maendeleo ya taifa.

  2. Colombia kukutana na Uswisi katika hatua ya 16

    Colombia iliifunga Ghana bao 1-0 na kufuzu kwa hatua ya 16 ya Kombe la Dunia kupitia bao lililofungwa na John Arias katika raundi ya timu 32

    Arias alifunga bao hilo katika dakika ya 14 kwa shuti la karibu kufuatia pasi kutoka kwa Luis Suarez, ambaye ndio mwanzo alikuwa ameingia uwanjani kuchukua nafasi ya John Cordoba aliyeumia.

    Luis Diaz alidhani ameongeza bao la pili dhidi ya Colombia katika dakika ya 56, lakini mwamuzi alilikataa bao hilo kwani alikuwa ameotea.

    Colombia ilitawala sehemu kubwa ya mchezo, huku kipa wa Ghana akifanya kazi nzuri ya kuokoa mikwaju mitatu hatari.

  3. 'Sharks' wa Cape Verde wawatikisa mabingwa watetezi wa Kombe la Dunia

    Cape Verde ilimaliza mbio yake ya kuwania Kombe la Dunia kwa kumaliza kishujaa, nusura kuwaondoa mabingwa watetezi, lakini Argentina, ikiongozwa na gwiji wao Lionel Messi, ilipata ushindi mgumu wa 3-2 baada ya muda wa ziada.

    Timu hiyo ya taifa ya visiwa vya Atlantiki, yenye idadi ya watu nusu milioni pekee, imekuwa kivutio kikubwa baada ya kukaidi matarajio kwa kutoka sare na mabingwa wa Ulaya Uhispania kabla ya kupata nafasi ya kuingia raundi inayofuata, ikimaliza mbele ya mabingwa mara mbili wa dunia Uruguay na Saudi Arabia katika Kundi H.

    Kocha wa Argentina, Lionel Scaloni, alisema kuwa kupoteza mechi dhidi ya Cape Verde "ingelikuwa jambo la ajabu sana".

    Scaloni aliongeza: "Ulikuwa mchezo mgumu sana; kilichotuwezesha kupata ushindi ni hulka ya timu hii (Argentina) haikati tamaa kamwe."

    Aliendelea kusema: "Tunawapongeza wapinzani wetu, kwa sababu wakati watu wakisema hakuna wapinzani dhaifu, leo wao wamethibitisha kuwa ni timu imara."

    Argentina inatarajia kuwa timu ya kwanza tangu mwaka 1962 kutetea taji lake la dunia.

    Baada ya Messi kufungua ukurasa wa mabao—akifunga bao lake la saba katika mashindano haya na kuongoza orodha ya wafungaji huku akifikisha jumla ya mabao 20 katika historia yake ya Kombe la Dunia—Deroy Duarte alijibu kwa kusawazisha matokeo.

    Soma zaidi:

  4. Kombe la Dunia 2026: Misri kukutana na Argentina katika hatua ya 16

    Kwa mara ya kwanza katika historia yake, Misri imefuzu kwa hatua ya 16 michuano ya Kombe la Dunia baada ya kuishinda Australia kwa penalti 4-2 (baada ya sare ya 1-1) siku ya Ijumaa mjini Dallas, Marekani.

    Misri sasa itakutana na mabingwa watetezi Argentina, ambao walinusurika kwa shida dhidi ya Cape Verde, kwa ushindi wa 3-2 katika muda wa nyongeza.

    Wachezaji wa timu ya 'Mafarao' walilipuka kwa furaha baada ya Hossam Abdel-Maguid kufunga penalti ya nne, huku sherehe zikianza kushuhudiwa miongoni mwa wachezaji na mashabiki viwanjani Arlington mbele ya watazamaji 80,000, wakati timu hiyo ikifikia mafanikio mapya.

    Kombe hili la Dunia ndilo lenye mafanikio makubwa zaidi kwa Misri katika mashindano manne (1934, 1990 na 2018), baada ya kupata ushindi wao wa kwanza dhidi ya New Zealand (3-1) katika hatua ya makundi na kufuzu kwa raundi ya mtoano kwa mara ya kwanza.

    Misri imekuwa nchi ya tano barani Afrika kufuzu kutoka hatua ya mtoano, baada ya Cameroon (1990), Senegal (2002), Ghana (2010) na Morocco (2022 na 2026).

    Panenka ya nyota Mohamed Salah iliiwezesha Misri kuongoza kwa mabao 3-2.

    Soma pia:

  5. Marekani yawaondoa wanajeshi wake Nigeria baada ya operesheni dhidi ya Islamic State

    Marekani imewaondoa wanajeshi wake waliopelekwa nchini Nigeria mapema mwaka huu katika juhudi za kusaidia kupambana na makundi ya wapiganaji wenye itikadi kali za kidini.

    Mnamo Desembam waka jana, vikosi vya Marekani na Nigeria vilianzisha operesheni ya pamoja katika eneo la Bonde la Ziwa Chad, ambayo ilihusisha mashambulizi dhidi ya wanamgambo siku ya Krismasi, na kufuatiwa na kutumwa kwa wanajeshi 200 miezi miwili baadaye.

    Kiongozi mkuu wa Islamic State (IS) Abu-Bilal al-Minuki aliuawa wakati wa operesheni hiyo iliyodumu kwa miezi kadhaa.

    Siku ya Alhamisi, Marekani iliangazia mafanikio yaliyofikiwa katika operesheni hiyo, huku msemaji wa jeshi la Nigeria akiiambia BBC kuwa kujiondoa kwa wanajeshi wa Marekani "hakutaathiri kasi yetu kwa vyovyote vile".

    Licha ya oparesheni hizo, makundi ya kijihadi yameendelea na mashambulizi hasa katika maeneo ya kaskazini mashariki mwa Nigeria.

    Meja Jenerali Michael Onoja alisema ushirikiano wa kijasusi kati ya nchi hizo mbili utaendelea, jambo ambalo jeshi la Marekani pia lilisema katika mkutano wake.

    Ushirikiano wa kijeshi kati ya Nigeria na Marekani uliongezeka baada ya Washington kushutumu mamlaka ya Nigeria kwa kushindwa kuwakabili vilivyo wapiganaji wa kijihadi, na kudai kulikuwa na "mauaji ya kimbari dhidi ya waumini wa Kikristo" nchini humo.

    Nigeria imekanusha madai hayo, ikisema ghasia hizo zinaathiri watu kutoka jamii zote.

    Maelezo zaidi:

  6. Mazishi ya Ali Khamenei yaanza rasmi kwa kufunguliwa kwa msikiti wa Tehran

    Vyombo vya habari vya Iran vinasema kuwa kadiri idadi ya watu inavyoongezeka katika eneo la Mosalla mjini Tehran, milango ya kaskazini ya eneo hilo imefunguliwa pia kwa ajili ya washiriki wa mazishi ya Ali Khamenei, kiongozi Mkuu wa zamani wa Jamhuri hiyo ya Kiislamu aliyeuawakatika mashambulizi ya Marekani na Israel.

    Jeneza la Khamenei linatarajiwa kuwekwa hadharani katika msikiti wa Mosalla mjini Tehran, ambapo watu watapita fursa ya kuliona.

    Maafisa wa Iran wanasema wanatarajia watu kati ya milioni 15 na 20 kuhudhuria shughuli hiyo ya siku sita katika miji mbalimbali nchini Iran na Iraq.

    Wakati huo huo, vyanzo vya habari nchini Iraq vinasema kuwa Baghdad, mji mkuu wa nchi hiyo, utasitisha shughuli zake kwa siku ya Jumatano kwa ajili ya mazishi ya Ali Khamenei.

    Kwa mujibu wa ratiba iliyotangazwa, shughuli hiyo itahitimishwa kwa mazishi ya Bw. Khamenei katika mji wake wa asili wa Mashhad siku ya Alhamisi.

    Ayatollah Ali Khamenei aliuawa pamoja na jamaa wanne wa familia yake mwanzoni mwa vita kati ya Marekani na Israel dhidi ya Iran.

    Soma zaidi:

  7. Natumai hujambo