'Sharks' wa Cape Verde wawatikisa mabingwa watetezi wa Kombe la Dunia

Chanzo cha picha, EPA
Cape Verde ilimaliza mbio yake ya kuwania Kombe la Dunia kwa kumaliza kishujaa, nusura kuwaondoa mabingwa watetezi, lakini Argentina, ikiongozwa na gwiji wao Lionel Messi, ilipata ushindi mgumu wa 3-2 baada ya muda wa ziada.
Timu hiyo ya taifa ya visiwa vya Atlantiki, yenye idadi ya watu nusu milioni pekee, imekuwa kivutio kikubwa baada ya kukaidi matarajio kwa kutoka sare na mabingwa wa Ulaya Uhispania kabla ya kupata nafasi ya kuingia raundi inayofuata, ikimaliza mbele ya mabingwa mara mbili wa dunia Uruguay na Saudi Arabia katika Kundi H.
Kocha wa Argentina, Lionel Scaloni, alisema kuwa kupoteza mechi dhidi ya Cape Verde "ingelikuwa jambo la ajabu sana".
Scaloni aliongeza: "Ulikuwa mchezo mgumu sana; kilichotuwezesha kupata ushindi ni hulka ya timu hii (Argentina) haikati tamaa kamwe."
Aliendelea kusema: "Tunawapongeza wapinzani wetu, kwa sababu wakati watu wakisema hakuna wapinzani dhaifu, leo wao wamethibitisha kuwa ni timu imara."
Argentina inatarajia kuwa timu ya kwanza tangu mwaka 1962 kutetea taji lake la dunia.
Baada ya Messi kufungua ukurasa wa mabao—akifunga bao lake la saba katika mashindano haya na kuongoza orodha ya wafungaji huku akifikisha jumla ya mabao 20 katika historia yake ya Kombe la Dunia—Deroy Duarte alijibu kwa kusawazisha matokeo.
Soma zaidi:



















