Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, Marco Rubio, amesema kuwa wapatanishi wa Marekani na Iran wana kile alichokiita “mapendekezo madhubuti mezani”, na kwamba makubaliano kati ya nchi hizo mbili yanaweza kufikiwa leo Jumatatu.
“Bado tuko katika mchakato wa mazungumzo,” Rubio amesema akiwa katika ziara nchini India.
Kauli hiyo imekuja baada ya Rais wa Marekani, Donald Trump, kusema kuwa amewaagiza wapatanishi kutoharakisha kufikia makubaliano, licha ya kuwa hapo awali alikuwa ameashiria kuwa mwafaka ulikuwa karibu kupatikana.
Makubaliano yanayojadiliwa yanaripotiwa kujumuisha kuongezwa kwa muda wa usitishaji mapigano kwa siku 60, kufunguliwa tena kwa Mlango Bahari wa Hormuz na mpango wa kuendelea na mazungumzo kuhusu mpango wa nyuklia wa Iran.
Matumaini ya kufikiwa kwa makubaliano hayo yalisababisha bei za mafuta kushuka kwa kiasi kikubwa huku masoko ya hisa ya Asia yakipanda siku ya Jumatatu.
Akizungumza mjini Delhi, Rubio alisema:
“Bado tuko katika hatua ya mazungumzo. Tulidhani huenda tungepata taarifa muhimu jana usiku, lakini pengine leo.”
Aliongeza kuwa kuna msingi imara wa makubaliano kuhusu kufunguliwa kwa Mlango Bahari wa Hormuz, njia muhimu ya majini inayopitisha takribani asilimia 20 ya mafuta na gesi asilia iliyoyeyushwa inayouzwa duniani, na ambayo imekuwa ikizuiwa na Iran.
Hata hivyo, Rubio alionya dhidi ya kutoa hitimisho la haraka, akisema kuwa bado inachukua muda kupata majibu kutoka Iran.
Wakati huo huo, kwa mujibu wa CBS News, mashirika ya kijasusi ya Marekani yanaamini kuwa Kiongozi Mkuu wa Iran, Mojtaba Khamenei, ambaye alijeruhiwa katika shambulio la Israel siku ya kwanza ya vita, yuko katika eneo lisilojulikana. Ripoti hiyo inaeleza kuwa hali hiyo imefanya mawasiliano kati yake na wajumbe wake kuwa magumu na hivyo kupunguza kasi ya mazungumzo na Marekani.
Mwishoni mwa wiki, msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran, Esmail Baghaei, alisema kuwa pande hizo mbili ziko “karibu sana na pia mbali sana” na kufikia makubaliano.
Kwa mujibu wa vyombo vya habari vya Marekani, makubaliano yanayojadiliwa kwa sasa si suluhisho la mwisho, bali yanaacha baadhi ya masuala magumu zaidi yaamuliwe katika mazungumzo ya baadaye.
Miongoni mwa masuala hayo ni muda na kiwango cha kuondolewa kwa vikwazo dhidi ya Iran, kuachiliwa kwa fedha za Iran zilizozuiwa nje ya nchi, pamoja na matakwa ya Washington ya kuizuia Iran kuendeleza shughuli zake za nyuklia.