Guyana yampendekeza balozi wake kuwania ukatibu mkuu wa Umoja wa Mataifa

Chanzo cha picha, Wizara ya mambo ya kigeni ya Guyana
Guyana imemteua balozi wake katika Umoja wa Mataifa kugombea wadhifa wa Katibu Mkuu wa Umoja huo wa kimataifa, jambo lililotangazwa na Rais wa taifa hilo la Amerika Kusini, Irfaan Ali, usiku wa Ijumaa.
Katibu Mkuu wa sasa wa Umoja wa Mataifa, António Guterres wa Ureno, anatarajiwa kuondoka madarakani mwishoni mwa mwaka huu baada ya kuhudumu kwa mihula miwili tangu mwaka 2017.
Carolyn Rodrigues-Birkett amekuwa mwakilishi wa Guyana katika Umoja wa Mataifa tangu mwaka 2020.
Guyana ni taifa la pwani ya Bahari ya Atlantiki lililopo kati ya Venezuela na Brazil, lenye idadi ya watu isiyofikia milioni moja.
Akizungumza katika hotuba yake, Rais Ali alisema maono ya Rodrigues Birkett kwa Umoja wa Mataifa yanajikita katika kuimarisha ushirikiano wa kimataifa, kuongeza ufanisi na mwitikio wa taasisi hiyo, kukuza utawala jumuishi wa dunia na kuhakikisha Umoja wa Mataifa una uwezo wa kukabiliana na changamoto za kisasa.
Ali pia alisifu uongozi wa balozi huyo mwenye umri wa miaka 52 wakati Guyana ilipohudumu kwa muhula wa miaka miwili kama mwanachama asiye wa kudumu wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kati ya mwaka 2024 na 2025.
“Uchaguzi wetu katika Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa na utekelezaji wenye mafanikio wa muhula wetu wa 2024 hadi 2025 umeonyesha kwa dunia kuwa Guyana inaweza kutoa uongozi katika ngazi mbalimbali za mfumo wa kimataifa,” alisema Ali.
Rodrigues Birkett aliwahi kuwa Waziri wa Mambo ya Nje wa Guyana kati ya mwaka 2008 na 2015 kabla ya kujiunga na Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO) kama Mratibu Maalumu wa Ushirikiano na Mabunge.
Mwaka 2017 aliteuliwa kuwa mkuu wa Ofisi ya Mawasiliano ya FAO mjini Geneva, Uswisi, ambako alihudumu hadi mwaka 2020.
Hadi sasa, hakuna mwanamke aliyewahi kushika wadhifa wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa.
Mataifa mengi yanaendelea kushinikiza mwanamke achaguliwe kwa mara ya kwanza kuongoza taasisi hiyo, huku nchi za Amerika ya Kusini zikidai ni zamu yao kwa kuzingatia utamaduni wa mzunguko wa kijiografia katika uteuzi wa nafasi hiyo, ingawa si mara zote kanuni hiyo imekuwa ikifuatwa kikamilifu.
Miongoni mwa wanaotajwa kuwania nafasi hiyo ni Michelle Bachelet, aliyewahi kuwa Rais wa Chile na Kamishna Mkuu wa Haki za Binadamu wa Umoja wa Mataifa, Rebeca Grynspan wa Costa Rica, pamoja na María Fernanda Espinosa.
Wagombea wengine waliotangaza nia ni Rafael Grossi kutoka Argentina na aliyekuwa rais wa Senegal Macky Sall.
Soma zaidi:




