Urusi yatishia mashambulizi mapya dhidi ya Kyiv, yawataka raia wa kigeni kuondoka

Chanzo cha picha, Reuters
Urusi imetishia kuanzisha wimbi jipya la mashambulizi ya “kimfumo” dhidi ya mji mkuu wa Ukraine, Kyiv, siku chache baada ya kutekeleza moja ya mashambulizi makubwa zaidi dhidi ya jiji hilo tangu kuanza kwa vita.
Katika taarifa yake, Wizara ya Mambo ya Nje ya Urusi ilisema mashambulizi hayo yatalenga “vituo vya kufanya maamuzi” na makao ya uongozi wa kijeshi, pamoja na maeneo ya kutengeneza ndege zisizo na rubani (droni) ndani ya Kyiv.
Moscow pia imewataka raia wa kigeni na wanadiplomasia kuondoka Kyiv “haraka iwezekanavyo”, huku ikiwatahadharisha watu kuepuka majengo ya utawala na vituo vya kijeshi.
Kwa upande wake, Ukraine imeelezea vitisho hivyo kuwa “siyo chochote zaidi ya usaliti wa wazi na mbinu za vitisho,” na kuzitaka nchi washirika kuongeza shinikizo dhidi ya Moscow.
Serikali ya Ukraine ilisema onyo la Urusi kwa raia wa kigeni linaashiria kwamba mashambulizi hayo yanalenga pia kuwatisha wanadiplomasia wa kigeni waliopo nchini humo.
Ukraine imeongeza kuwa mashambulizi ya Urusi dhidi ya Kyiv hayajawahi kusimama kwa kipindi cha hata wiki moja tangu kuanza kwa vita, huku tishio la usalama kutoka Moscow likiendelea kuwa kubwa kama ilivyokuwa miezi na miaka iliyopita.
Kwa mujibu wa Rais wa Ukraine, Volodymyr Zelenskyy, mashambulizi makubwa ya Urusi yaliyofanyika usiku wa Jumamosi yaliua watu wanne na kujeruhi takribani 100 katika Kyiv na maeneo mengine.
Urusi imesema mashambulizi hayo na vitisho vya mashambulizi zaidi ni jibu la kile inachodai kuwa shambulio la makusudi la Ukraine dhidi ya bweni la wanafunzi katika mji wa Starobilsk siku ya Ijumaa, ambapo maafisa wa Urusi wanasema watu 21 waliuawa.









