Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Zaidi ya watu 350 wafariki katika mafuriko nchini Nepal

Mamia ya watu hawajulikani walipo baada ya mafuriko Nepal, baadhi ni wakimbizi

Muhtasari

Moja kwa moja

Na Beldeen Waliaula& Ambia Hirsi

  1. Kiongozi wa upinzani wa Zambia ahojiwa na polisi - ripoti

    Shirika la utangazaji la Zambia ZNBC linaripoti kuwa kiongozi wa upinzani wa nchini hiyo, Brian Mundubile, ambaye alikuwa amejificha baada ya kupinga matokeo ya uchaguzi wa urais wa hivi karibuni, amekabidhiwa kwa polisi.

    Matokeo rasmi ya uchaguzi wa tarehe 13 Agosti yalionyesha kuwa Rais aliyeko madarakani, Hakainde Hichilema, alishinda kwa kupata asilimia 60 ya kura dhidi ya asilimia 38 alizopata Mundubile.

    Siku moja baada ya uchaguzi, vikosi vya usalama vilivamia eneo moja jijini Lusaka lililohusishwa na Mundubile, na kusababisha kifo cha waziri wa zamani wa serikali na kuwakamata wanasiasa wengine kadhaa.

    Mamlaka ziliishutumu upinzani kwa kupanga uasi wa kutumia silaha, madai ambayo upinzani uliyakataa. Kufuatia uvamizi huo, Mundubile alihamia "eneo salama chini ya ulinzi wa shirika la kimataifa la haki za binadamu kutokana na vitisho dhidi yake," chama chake cha NRPUP kilisema.

    ZNBC inaripoti kuwa kiongozi huyo wa upinzani, pamoja na mgombea mwenza wake Makebi Zulu, walikuwa wakilindwa na Umoja wa Mataifa jijini Lusaka.

    Shirika hilo linaongeza kuwa wawili hao sasa wanahojiwa na "maafisa wa vyombo vya dola" mbele ya mawakili wao kufuatia wito wa kuitwa kwa ajili ya mahojiano kuhusu "madai ya vitendo ambavyo polisi wanasema vina uwezo wa kutishia usalama wa taifa".

    Upinzani haukuweza kuwasilisha kesi ya kupinga matokeo ya uchaguzi mahakamani kwa sababu mahakama zilikuwa zimefungwa na mamlaka siku ya Jumatatu, ambayo ilikuwa siku ya mwisho ya kuweza kufungua kesi hiyo.

  2. Mkuu wa jeshi letu hakuzuru Iran kama 'mjumbe wa Trump' - Pakistan

    Pakistan imepuuzilia mbali ripoti kwamba mkuu wake wa majeshi, Jenerali Asim Munir, alizuru Iran hivi karibuni kama mjumbe wa Rais wa Marekani Donald Trump, ikizitaja taarifa hizo kuwa "za kupotosha na zisizo na msingi."

    Tahir Andrabi, msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Pakistan, alisema leo katika mkutano wa kila wiki na waandishi wa habari mjini Islamabad kuwa madai kwamba Mkuu wa Majeshi ya Pakistan kuzuru Iran kama mjumbe wa Bw.Trump au Marekani ni ya uongo, na kwamba safari hiyo ilifanyika ndani ya mfumo wa jukumu la upatanishi la Pakistan.

    Alisema Asim Munir alisafiri kwenda Tehran mnamo Agosti 24 ikiwa ni sehemu ya juhudi za kidiplomasia za Pakistan kusaidia kumaliza mzozo kati ya Marekani na Iran na kuwezesha kufunguliwa tena kwa Lango la Hormuz.

    Kulingana na msemaji huyo wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Pakistan, mazungumzo wakati wa ziara hiyo yalilenga kupunguza mivutano ya kikanda, kuvunja mkwamo wa kijeshi, na kutafuta suluhisho la mazungumzo ili kurejesha amani na utulivu katika eneo hilo.

    Aliongeza kuwa ziara hiyo ilionyesha jukumu la Islamabad la "uaminifu na lenye tija" katika kupunguza tofauti kati ya Washington na Tehran.

    Msemaji huyo wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Pakistan alisema kuwa nchi yake, pamoja na nchi "ndugu," itaendelea kufanya juhudi za pamoja kutatua migogoro katika Mashariki ya Kati na itaunga mkono juhudi zote za dhati za kurejesha mazungumzo ya amani na kufikia suluhisho la kudumu.

  3. Jeshi la majini la Yemen lakamata meli iliyokuwa na shehena ya silaha za Wahouthi

    Vyombo vya habari vya Yemen vinaripoti kwamba jeshi la majini la nchi hiyo lilizuia shambulio la wanamgambo wa Houthi katika operesheni ya majini asubuhi ya leo na kukamata meli iliyobeba vifaa vya kijeshi vya asili ya Iran.

    Kulingana na Al Jazeera, Jeshi la Wanamaji la Yemen linasema meli hiyo ilikuwa imebeba vifaa vya kutengeneza ndege zisizo na rubani kwa ajili ya Wahouthi na ilikamatwa karibu na pwani ya Al-Mokha katika Bahari ya Shamu.

    Shirika la habari la Saba lenye makao yake Aden liliripoti, likinukuu jeshi la majini la nchi hiyo, kwamba vifaa hivyo vilisafirishwa kinyemela na Kikosi cha Walinzi wa Mapinduzi ya Iran na vilikusudiwa kutumwa kwa Wahouthi.

    Saa chache baadaye, doria za majini zilifyatua risasi kwenye boti tano za Wahouthi zinazokaribia visiwa vinavyoangalia njia za kimataifa za meli, na kuvilazimisha kurudi kaskazini, kulingana na vyombo vya habari vya kijeshi vinavyounga mkono serikali, ambavyo pia vilisema ndege isiyo na rubani ya upelelezi ya Wahouthi ilipigwa risasi.

  4. Waziri wa Mambo ya Nje wa Qatar akutana na Abbas Araqchi mjini Tehran

    Waziri wa Mambo ya Nje wa Qatar, Mohammed bin Abdulrahman Al Thani, alikutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran, Abbas Araqchi, Alhamisi jioni kwa saa za Tehran.

    Maelezo kuhusu mkutano huo hayajawekwa wazi. Ziara hiyo ya afisa wa ngazi ya juu wa Qatar ilifanyika siku mbili baada ya ziara ya Field Marshal Asim Munir, kamanda wa jeshi la Pakistan, jijini Tehran.

    Qatar na Pakistan zilikuwa miongoni mwa nchi zilizohusika katika upatanishi wakati wa kusainiwa kwa hati ya makubaliano kati ya Iran na Marekani.

    Jana, msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran, Esmail Baghaei, alitangaza ziara ya Waziri wa Mambo ya Nje wa Qatar nchini Iran na kusema: "Waziri wa Mambo ya Nje wa Qatar atajadili na kubadilishana mawazo na maafisa wa nchi yetu kuhusu mwendelezo wa juhudi na mipango ya upatanishi ya Qatar pamoja na masuala mengine yanayoendelea katika eneo hilo."

  5. Pezeshkian kukutana na Putin nchini Kyrgyzstan

    Balozi wa Iran mjini Moscow ametangaza kuwa Rais Masoud Pezeshkian atakutana na Rais wa Russia Vladimir Putin wiki ijayo, pembezoni mwa mkutano wa kilele wa Shirika la Ushirikiano la Shanghai nchini Kyrgyzstan.

    Mkutano wa kilele wa Shirika la Ushirikiano la Shanghai wa mwaka 2026 umepangwa kufanyika tarehe 1 Septemba 2026 mjini Bishkek, mji mkuu wa Kyrgyzstan.

    Balozi wa Iran, Kazem Jalali, alisema siku ya Jumatano—katika taarifa iliyoripotiwa na shirika rasmi la habari la Iran, IRNA—kwamba mpaka sasa Rais Masoud Pezeshkian amefanya mazungumzo ya ana kwa ana mara tano na Putin, na atashiriki katika mkutano wa Shanghai wiki ijayo, ambapo atafanya naye mkutano wa sita.

    Shirika la Ushirikiano la Shanghai lina nchi kumi wanachama, zikiwemo Iran, Russia, China, India, Pakistan na nchi za Asia ya Kati.

    Haya yanajiri wakati Iran ikiwa katika mzozo mkali na Marekani, miezi sita baada ya kuzuka kwa vita kufuatia mashambulizi ya Marekani na Israel yaliyofanyika tarehe 28 Februari.

    Maelezo zaidi:

  6. Mzozo wa Tigray: Marekani na EU zakaribisha juhudi za upatanishi za AU

    Marekani na Umoja wa Ulaya zimeashiria kuunga mkono juhudi mpya za upatanishi za Umoja wa Afrika katika eneo la Tigray nchini Ethiopia, huku hofu ya kuzuka upya kwa mapigano ikiongezeka katikati ya mashambulizi yanayoendelea ya ndege zisizo na rubani.

    Katika taarifa iliyotolewa Jumanne, tarehe 25 Agosti 2026, Ubalozi wa Marekani nchini Ethiopia ulikaribisha hatua za mjumbe wa Umoja wa Afrika (AU) Olusegun Obasanjo, ukielezea jukumu la AU kuwa muhimu sana wakati ambapo "mvutano na hofu kubwa" vinaendelea miongoni mwa jamii za kaskazini mwa Ethiopia.

    "Tunatumai atarejea hivi karibuni," taarifa hiyo iliongeza, ikibainisha kuwa kurejea salama kwa watu waliokimbia makazi yao kunapaswa kuwa kipaumbele chaa viongozi wote.

    Umoja wa Ulaya na nchi wanachama wake, pamoja na balozi za Canada, Norway, na Uingereza, zilitoa taarifa tofauti siku ya Jumatano zikionyesha "wasiwasi mkubwa" kuhusu hali inayoendelea huko Tigray.

    Zilihimiza pande zote kuzingatia Makubaliano ya Pretoria, ambayo yalimaliza vita vya Tigray vya mwaka 2020–2022, na kuonya kwamba "kuzuka upya kwa mapigano ya kijeshi katika eneo la Tigray—ambalo tayari limeathiriwa vibaya na ukame na lilillo na mahitaji makubwa ya kibinadamu—kutakuwa na madhara makubwa kwa watu wa kaskazini mwa Ethiopia."

    Obasanjo, ambaye ni Mwakilishi Mkuu wa AU katika Pembe ya Afrika, alizuru mji wa Mekelle siku ya Jumatatu kwa ajili ya mazungumzo na mamlaka za Tigray, ambazo ziliweka masharti ya awali ya kuanza tena mazungumzo na serikali kuu.

    Masharti hayo ni pamoja na kuondolewa kwa vikwazo vya kiuchumi, kuwaondoa wanajeshi waliozingira Tigray, kurejeshewa mamlaka yao, kuwahakikishia usalama waliokimbia makazi yao, na kurejeshewa hadhi ya kisiasa na kisheria kwa chama cha TPLF.

    Huku hayo yakijiri, jeshi la Ethiopia limeendelea kufanya mashambulizi ya ndege zisizo na rubani katika eneo hilo.

    Tarehe 26 Agosti, vyombo vya habari vya eneo hilo viliripoti shambulio dhidi ya shule ya sekondari huko Gijet, kusini-mashariki mwa Tigray.

    "Hakukuwa na shabaha za kijeshi, mapigano, au uwepo wa watu wenye silaha karibu na eneo hilo.

    Soma pia:

  7. M23 yapinga hatua ya kusitishwa kwa masomo katika vyuo vikuu vya Goma na Bukavu

    Kundi la waasi la M23 limekosoa uamuzi wa hivi karibuni wa serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), wa kusimamisha kwa muda masomo katika vyuo vikuu kadhaa, katika miji ya Goma na Bukavu, kutokana na sababu za kiusalama.

    Katika taarifa iliyotolewa na kundi hilo, imesema kuwa uamuzi uliochukuliwa na mamlaka za Kinshasa “ulikuwa wa haraka na haukuzingatia madhara yanayoweza kujitokeza”

    M23 inasema kuwa kulingana na katiba ya taifa hilo, kila mtu ana haki ya kupata elimu, na elimu haifai kutumiwa katika maslahi ya kisiasa.

    “Hakuna mwanafunzi anayepaswa kulazimishwa kupoteza mwaka wa masomo au elimu yake kutokana na hali ambayo nchi inakabiliwa nayo,” taarifa ya M23 imesema.

    Mwaka uliopita, M23 iliteka maeneo kadhaa yaliyokuwa chini ya udhibiti wa majeshi ya serikali ya DRC ikiwemo mji wa Goma na Bukavu.

    Ingawa M23 inasema maeneo inayodhibiti yako salama, mapigano ya hapa na pale kati ya kundi hilo na majeshi ya serikali yamekuwa yakishuhudiwa.

    Waziri wa Elimu ya Juu na Vyuo Vikuu nchini DRC, Prof Marie-Thérèse Sombo Ayanne, amesema ukosefu wa usalama umetatiza shughuli za kawaida za taasisi za elimu.

    Waziri huyo amewaagiza viongozi wa vyuo vilivyoko katika maeneo salama kuwapokea wanafunzi kutoka maeneo yaliyoathiriwa na vita ili waweze kuendelea na masomo yao.

    Soma pia:

  8. Raia 173 wa Tanzania warejea kutoka Afrika Kusini

    Takriban raia 173 wa Tanzania wamerejea nyumbani kutoka Afrika Kusini.

    Serikali ya Tanzania kupitia ubalozi wake ulikuwa umetoa mwito wa wale wanaotaka kurejea kwa hiari kufika katika ubalozi wa taifa hilo ulioko mjini Pretoria Afrika Kusini.

    Kundi la kwanza liliwasili usiku wa kuamkia leo, huku kundi lingine likitarajiwa kuwasili hii leo.

    Zoezi hilo litawahusisha Watanzania wasio na pasipoti, ambao muda wa kutumika wa pasipoti zao umekwisha au kupotea, pamoja na watoto waliozaliwa Afrika Kusini.

    Watanzania wasio na pasipoti watapewa hati za dharura za kusafiria ili kuwawezesha kurejea nchini humo.

    Uamuzi wa kuwarejesha Watanzania nchini unakuja wakati kumekuwa na maandamano ya kupinga wahamiaji nchini Afrika Kusini.

    Mataifa kadhaa ya Afrika tayari yamewaondoa raia wao nchini humo.

    Soma pia:

  9. Tunachokijua kufikia sasa kuhusu maporomoko ya ardhi nchini Nepal

    Maporomoko makubwa ya ardhi na mafuriko ya ghafla yameshuhudiwa katika mpaka wa Nepal na Tibet,na kusababisha uharibifu mkubwa wa mali, miundombinu na kuwauwa watu.

    Idadi ya waliofariki kutokana na janga hilo kwa sasa imefikia watu 177.

    Juhudi za kuwatafuta manusura bado zinaendelea

    Nini kimesababisha maporomoko hayo ya ardhi?

    Waziri wa Mambo ya Kigeni wa Nepal amesema kuwa tetemeko la ardhi liliripotiwa katika mpaka wa Tibet na Nepal muda mfupi kabla ya maporomoko hayo ya ardhi kutokea, akipendekeza kuwa huenda tetemeko hilo ndilo lililosababisha janga hilo.

    Hata hivyo, uchambuzi wa hivi karibuni wa Shirika la Jiolojia la Marekani (USGS) unaonyesha kuwa hakukuwa na tetemeko la ardhi, jambo ambalo limeibua maswali kuhusu chanzo halisi cha maporomoko hayo ya ardhi.

    Kuna uwezekano kuwa maji kutokana na mvua au kuyeyuka kwa barafu huenda yalifanya ardhi au barafu kutokuwa imara, na hivyo kusababisha mfululizo wa matukio hayo.

    Mabadiliko ya tabianchi yamekuwa yakichochea kuyeyuka kwa barafu katika eneo la Hindu Kush Himalaya, lakini wanasayansi wanasema bado ni mapema kubaini mchango wake katika tukio hili.

    Kwa sasa, wanasayansi wanajaribu kurejelea matukio hayo ili kubaini kilichotokea

    Ni watu wangapi wamefariki na kupotea?

    Idadi ya watu waliofariki au kupotea bado inaendelea kuongezeka.

    Polisi nchini Nepal wanasema angalau watu 162 wamefariki. Kati ya waliokufa, miili ya watu 64 ilipatikana katika maeneo ya chini ya mkondo wa maji katika wilaya ya Chitwan, huku miili mingine 26 ikipatikana Nawalparasi Mashariki.

    Idadi ya watu waliopotea kufuatia janga hili katika kaunti ya Gyirong, Tibet, imeongezeka hadi 558.

    Watalii waliopotea wanatoka nchi gani?

    Watalii kutoka sehemu mbalimbali duniani huitembelea Nepal kwa ajili ya kukwea milima yake na maeneo yake matakatifu. Takwimu rasmi zinaonyesha kuwa angalau wageni 291 ni miongoni mwa watu waliopotea, wakiwemo:

    India –142 wa India, Ukraine –53, Malaysia –50, Uingereza –33, Canada –24, Marekani –54 , Australia –34 ,

    Idadi ndogo ya wasafiri kutoka Korea Kusini, Afrika Kusini, Ureno na Uholanzi pia ni miongoni mwa watu waliopotea.

  10. Moto wa nyika wauwa watu 12 Algeria

    Wizara ya Mambo ya Ndani nchini Algeria, imetangaza kuwa watu 12 wamefariki kutokana na moto wa nyika unaoendelea kuteketeza maeneo ya kaskazini-mashariki mwa nchi hiyo.

    Waziri wa Mambo ya Ndani, Serikali za Mitaa na Uchukuzi, Said Saioud, amethibitisha vifo hivyo na kuongezea kuwa watu wengine 54 walipata majeraha ya moto, huku sita kati yao wakiwa katika hali mbaya na wamelazwa katika vyumba vya watu mahututi.

    Mamlaka za Algeria zimeripoti visa 154 vya moto kote nchini humo, huku wakiweza kudhibiti sehemu kubwa ya moto huo.

    Moto wa nyika umetokea wakati mataifa ya Afrika Kaskazini yanaendelea kukumbana na joto kali, haswa Tunisia na Algeria.

    Soma pia:

  11. Marekani na UN zatoa msaada kwa waathiriwa wa mafuriko Nepal

    Marekani imeahidi kutoa msaada wa dola 500,000 ambazo zitatumika kugharamikia makazi ya muda, maji, huduma za usafi na misaada mingine kwa jamii zilizoathiriwa na mafuriko.

    “Marekani inatuma salamu zake za rambirambi kwa familia na jamaa wa waliofariki katika mafuriko makubwa ya ghafla yaliyoikumba wilaya ya Rasuwa nchini Nepal,” Idara ya Mambo ya Kigeni ya Marekani ilisema katika taarifa.

    Takriban raia 54 wa Marekani, wengi wao wakiwa watalii, wameripotiwa kuwa miongoni mwa mamia ya watu waliopotea kufuatia mafuriko na maporomoko ya ardhi.

    Hayo yakijiri, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, António Guterres, amesema “amehuzunishwa na mafuriko hayo makubwa” ambayo yamesababisha vifo vya watu wengi, huku wengine wakiwa hawajulikani walipo nchini Nepal na China.

    “Nasimama pamoja na wote walioathiriwa,” amesema kiongozi huyo.

    Ameongezea kuwa timu za Umoja wa Mataifa na washirika wake zinaandaa kusafirisha vifaa pamoja na kuwapeleka wahudumu wa dharura nchini Nepal ili kuisadia kukabiliana na janga hilo.

    Soma pia:

  12. Tazama namna vijiji vilisombwa na mafuriko Nepal

    Waokoaji wanakabiliwa na changamoto kufika katika maeneo yaliyoathiriwa na mafuriko makubwa ya ghafla na maporomoko ya udongo nchini Nepal, ambayo yamesababisha vifo vya zaidi ya watu 160.

    Mamia ya watalii hawajulikani walipo, wakiwemo zaidi ya 100 kutoka India, 54 kutoka Marekani, 34 kutoka Australia na 33 kutoka Uingereza.

    Maafisa pia wanasema zaidi ya watu 100 kutoka Nepal wenyewe hawajulikani walipo.

    Eneo hilo ni maarufu kwa watalii wanaofanya matembezi milimani pamoja na mahujaji.

    Wakati shughuli za uokoaji zikiendelea, wataalamu wanaonya kuwa vifusi vilivyoziba mto karibu na eneo la maafa vinaweza kusababisha mafuriko mengine.

    Mamlaka zinaendelea na juhudi za kuwasaka na kuwaokoa watu waliokwama katika maeneo yaliyoathiriwa.

  13. Iran yaishtumu Marekani kwa kujaribu kuzuia mazungumzo yao na Oman

    Jeshi la Iran IRGC, limeishtumu Marekani kwa kile wamekitaja ‘kujaribu kuzuia’ makubaliano kati ya Iran na Oman, kuhusu usimamizi wa Mlango Bahari wa Hormuz.

    Jeshi hilo limesema wamefikia makubaliano na Oman, ya kugawana mapato watakayokusanya katika usimamizi wao wa Pamoja wa Mlango wa Hormuz,ila Marekani inajaribu kuzuia kukamilika kwa makubaliano hayo.

    Tehran na Muscat zimejadili kuanzishwa kwa njia nyingingine ya bahari na mfumo utakaoendesha safari za meli katika Mlango wa Hormuz.

    Aidha, Tehran imeonya kuwa njia hiyo ya bahari haitafunguliwa tena hadi Marekani isitishe vita.

    Mazungumzo kati ya Iran na Oman, yanajiri baada ya Washington kutangaza vikwazo vipya vinavyolenga kuilemaza Iran kiuchumi.

    Soma pia:

  14. Mafuriko Nepal na Tibet yaua zaidi ya 160, mamia ya watalii hawajulikani walipo

    Zaidi ya watu 160 wamefariki nchini Nepal, huku mamia ya watalii wakiwa hawajulikani walipo baada ya mafuriko makubwa ya ghafla na maporomoko ya udongo katika eneo la mpaka kati ya Nepal na Tibet.

    Nchini China, idadi ya watu ambao hawajulikani walipo baada ya maporomoko ya udongo katika kaunti ya Gyirong, Tibet, imefikia 558, kwa mujibu wa shirika la utangazaji la serikali CCTV.

    Kati yao, 260 ni raia wa kigeni. Idadi ya waliofariki imeendelea kuwa watatu.

    Mpaka wa Gyirong ni njia kuu inayotumiwa na watalii na magari kusafiri kati ya China na Nepal.

    Nepal awali ilisema watu 579 hawajulikani walipo, wakiwemo raia 466 wa kigeni. Haijafahamika mara moja iwapo baadhi ya watu hao wamehesabiwa mara mbili katika takwimu za nchi hizo mbili.

    Jeshi la Nepal limetuma wanajeshi 2,000 kushiriki katika shughuli za utafutaji na uokoaji kwa njia ya ardhini na angani katika maeneo yaliyoathiriwa na mafuriko.

    Msemaji wa jeshi, Brigedia Jenerali Rajaram Basnet, ameiambia BBC kuwa wanajeshi hao wamejikita katika maeneo yaliyoathirika zaidi, yakiwemo wilaya za Rasuwa na Nuwakot.

    Jeshi hadi sasa limefanikiwa kuwaokoa watu 97 waliokuwa wamekwama kwenye mafuriko. Watatu kati yao walikuwa wafanyakazi waliokwama katika handaki la mradi wa kuzalisha umeme wa maji wa Trishuli A.

    Polisi na kikosi cha polisi wenye silaha cha Nepal pia vimepeleka maafisa katika maeneo yaliyoathiriwa kusaidia shughuli za utafutaji.

    Awali mamlaka zilidhani kuwa huenda tetemeko la ardhi lilitangulia mafuriko hayo. Hata hivyo, Utafiti wa Jiolojia wa Marekani, USGS, sasa umesema nishati iliyosababisha mtikisiko huo ilitokana na maporomoko ya udongo, badala ya tetemeko la ardhi.

  15. Waziri Mkuu wa Qatar kuzuru Tehran

    Waziri Mkuu wa Qatar anatarajiwa kuzuru Tehran hii leo, katika juhudi za kuanzisha tena mazungumzo ya kidiplomasia, baada ya makubaliano ya kusitisha vita kati ya Iran na Marekani kuvunjika.

    Washington tayari imetangaza kuiwekea Iran vikwazo vya kiuchumi pamoja na washirika wake wa karibu.

    Qatar, ambayo ni jirani wa Iran katika eneo la Ghuba na pia mshirika wa Marekani, imekuwa mpatanishi wa siri kati ya pande hizo mbili zinazozozana, na ilichangia pakubwa katika kufanikisha makubaliano ya kusitisha mapigano yaliyoafikiwa mwezi Juni.

    Ziara ya Waziri Mkuu wa Qatar, Mohammed bin Abdulrahman bin Jassim bin Jaber Al Thani, inafanyika wakati vita kati ya Iran na Marekani vinaingia mwezi wake wa sita huku kukiwa hakuna dalili ya mafanikio yoyote ya kidiplomasia.

    Marekani na Iran bado zinatofautiana kuhusu Mlango Bahari wa Hormuz ambayo ni njia muhimu ya usafirishaji mafuta duniani.

    Soma pia:

  16. Hujambo na karibu katika matangazo yetu ya moja kwa moja Alhamisi ya leo