Moja kwa moja, Hatuko vitani na Saudia na Wahouthi wana masuala yao wenyewe - Iran

Katika mahojiano na shirika la habari la India Today, Rais wa Iran Masoud Pezzekian amesema kuwa nchi yake haiko vitani na Saudia

Muhtasari

  • Ndege za kivita za NATO zaangusha ndege isiyo na rubani iliyoingia katika anga ya Lithuania
  • Marekani yathibitisha kupeleka silaha anga za juu
  • Hatuko vitani na Saudia na Wahouthi wana masuala yao wenyewe - Iran

Moja kwa moja

Abdalla Seif Dzungu

  1. Ndege za kivita za NATO zaangusha ndege isiyo na rubani iliyoingia katika anga ya Lithuania

    .

    Chanzo cha picha, AFP Via Getty

    Marubani wa ndege za kivita za NATO wameidungua ndege isiyo na rubani (drone) iliyoingia katika anga ya Lithuania usiku kucha, Rais wa Lithuania amesema.

    Mamlaka zimesema kuwa ndege hiyo huenda iliingia kusini mwa Lithuania, karibu na jiji la pili kwa ukubwa la Kaunas, ikitokea nchi jirani ya Belarus muda mfupi baada ya saa sita usiku siku ya Jumanne.

    Rais wa Lithuania, Gitanas Nausėda, aliandika katika taarifa kwenye mtandao wa X: "Ndege isiyo na rubani iliyoingia katika anga ya Lithuania imeangamizwa na ndege za kivita za NATO."

    Chanzo cha ndege hiyo bado hakijajulikana, msemaji wa kituo cha kitaifa cha usimamizi wa dharura cha Lithuania alisema.

    Tahadhari kuhusu ndege hiyo zilisikika katika mji mkuu wa Vilnius na maeneo ya jirani mapema siku ya Jumanne.

    Jeshi la Lithuania na marubani wa Italia wanaohudumu katika Operesheni ya NATO ya Ulinzi wa Anga "walionyesha mwitikio wa haraka na wa uwajibikaji" dhidi ya kuingia kwa ndege hiyo, Wizara ya Ulinzi ya Lithuania ilisema.

    Ujumbe wa Nausėda kwenye mitandao ya kijamii uliongeza: "Wakati Urusi ikiongeza uchokozi wake dhidi ya Ukraine, utayari wa namna hii ni muhimu sana kwa eneo letu. Kwa kushirikiana na washirika wetu wa NATO, Lithuania italinda anga yake."

    Moscow haijatoa maoni yoyote kuhusu tukio hilo.

  2. Marekani yathibitisha kupeleka silaha anga za juu

    ..

    Chanzo cha picha, Thomas Traasdahl/Ritzau Scanpix/AFP via Getty Images

    Marekani imethibitisha kuwa imetuma silaha ya angani katika obiti ya Dunia, ikiwa ni mara ya kwanza kukiri kuwa na uwezo kama huo wa mashambulizi.

    Waziri wa Jeshi la Anga la Marekani, Troy Meink, amesema silaha hiyo iliyopo kwenye obiti ilikuwa muhimu ili kulinda vikosi vya Marekani dhidi ya vitendo vya uhasama vya adui.

    Akizungumza katika Kongamano la Anga, Nafasi ya Anga na Mtandao (Air, Space and Cyber ​​Conference) siku ya Jumatatu, Meink alisema Marekani iko tayari kukabiliana na "vitisho vinavyobadilika", lakini hakutoa maelezo zaidi kuhusu uwezo wa silaha hiyo au wakati ilipowekwa kwenye obiti.

    Viongozi wa ngazi ya juu wa kijeshi hapo awali walisema walipanga kuimarisha uwezo wa kijeshi angani, wakitaja mipango ya Urusi na China ya kutengeneza njia za kushambulia na kuvuruga satelaiti za Marekani katika mzozo wa siku zijazo.

    Utawala wa Trump umesema kuwa uwezo wa kijeshi wa angani - na makombora ya kuzuia mashambulizi - ni sehemu muhimu ya mfumo wake wa ulinzi unaopangwa kuitwa "Golden Dome" ili kuilinda Marekani dhidi ya makombora na vitisho vingine vya angani.

    Mkataba wa mwaka 1967 ulipiga marufuku silaha za maangamizi makubwa katika obiti. Tangu wakati huo, mataifa yenye nguvu kubwa ikiwemo Marekani, Urusi, na China yamekuwa yakichunguza uwezo mwingine nje ya mkataba huo, kama vile kulenga satelaiti za wapinzani - ambazo ni muhimu kwa mawasiliano ya kijeshi, ufuatiliaji na urambazaji.

    Mwaka jana, Rais Donald Trump alitoa agizo la kiutendaji likisisitiza jukumu la Jeshi la Anga la Marekani (US Space Force) si tu katika kulinda rasilimali, bali pia kama nguvu ya kushambulia.

    Jeshi la Anga la Marekani - tawi jipya zaidi la jeshi la Marekani katika kipindi cha zaidi ya miaka 70 - lilianzishwa mwaka 2019 kama njia ya kulinda rasilimali za Marekani angani, ikiwa ni pamoja na mamia ya satelaiti zinazotumiwa kwa mawasiliano na ufuatiliaji.

  3. Hatuko vitani na Saudia na Wahouthi wana masuala yao wenyewe - Iran

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Maelezo ya picha, Rais Pezzeksian wa Iran

    Katika mahojiano na shirika la habari la India Today, Rais wa Iran Masoud Pezzekian amesema kuwa nchi yake haiko vitani na Saudai , na kwamba nchi za eneo hilo pia zina "mtazamo potofu" kuhusu mashambulizi ya Iran dhidi ya kambi za kijeshi za Marekani katika eneo hilo.

    Katika mazungumzo hayo, ambayo yalirekodiwa wakati Bw. Pezzekian akiwa nchini India kuhudhuria mkutano wa kilele wa BRICS na kurushwa hewani na mashirika ya habari ya Iran siku ya Jumatatu, Bw. Pezzekian anasema: "Hatuko vitani na Saudi Arabia, na Wahouthi pia wana masuala yao wenyewe. Nchi zote za eneo hilo zinapaswa kukaa pamoja na kuleta amani na usalama katika eneo hilo. Hakuna mantiki wala sababu ya sisi kuwa katika vita na migogoro sisi kwa sisi."

    Rais wa Iran amesisitiza: "Tatizo ni kwamba Marekani imeanzisha kambi katika ardhi ya nchi za Kiarabu. Wanatushambulia kutokea huko. Haiwezekani tukawa tunashambuliwa kutokea huko kila siku. Sisi hatukuwashambulia wao. Tulilenga chanzo cha shambulio dhidi ya nchi yetu. Kwa kawaida, jambo hili limesababisha kiasi fulani cha chuki dhidi ya nchi za eneo hilo."