Amri ya kutotoka nje yatangazwa Dar es Salaam

Uharibifu mkubwa umeshuhudiwa kwa vituo vya mabasi ya mwendokasi, vituo vya kupigia kura, mabasi, na maeneo ya biashara.

Moja kwa moja

Yusuph Mazimu na Lizzy Masinga

  1. Mamlaka zichunguze ukatili wa polisi dhidi ya waandamanaji Tanzania - Amnesty International

    g

    Shirika la Amnesty International limezitaka mamlaka za Tanzania kufanya uchunguzi wa haraka, huru na wa kina kuhusu matumizi ya nguvu kupita kiasi na zisizo za lazima yaliyofanywa na polisi dhidi ya waandamanaji siku ya uchaguzi mkuu nchini humo.

    Haya yanajiri baada ya ripoti kuwa watu wawili wameuawa na kadhaa kujeruhiwa.

    Akizungumzia tukio hilo, Mkurugenzi wa Kanda wa Amnesty International kwa Afrika Mashariki na Kusini, Tigere Chagutah, alisema:

    “Taarifa za raia mmoja na askari polisi mmoja wameuawa katika maandamano ya siku ya uchaguzi nchini Tanzania ni za kusikitisha sana. Kuna hatari kubwa ya kuongezeka kwa machafuko tunazihimiza mamlaka za polisi kujizuia na kuepuka kutumia nguvu zisizo za lazima au kupita kiasi dhidi ya waandamanaji.”

    “Mamlaka za Tanzania lazima zifanye uchunguzi wa kina, huru na wa haraka kuhusu matumizi yasiyo halali ya nguvu kupita kiasi dhidi ya waandamanaji, na kuhakikisha kwamba wahusika wote wanawajibishwa ipasavyo.”

    Chagutah pia alionya kwamba usumbufu wa huduma za intaneti uliyoripotiwa nchini kote unaweza kuongeza zaidi hali ya taharuki.

    “Mamlaka zinapaswa kuhakikisha upatikanaji wa taarifa bila vizuizi, mtandaoni na nje ya mtandao. Ni muhimu huduma ya intaneti irejeshwe kikamilifu na vyombo vya habari vya ndani na vya kimataifa viruhusiwe kuripoti kwa uhuru kuhusu uchaguzi. Serikali ina wajibu wa kikatiba kulinda na kuheshimu haki za binadamu za wote kabla, wakati na baada ya uchaguzi,” aliongeza.

    Soma pia:

  2. Shughuli ya kuhesabu kura yaanza visiwani Zanzibar

    Wakaazi wakipiga kura ya uchaguzi mkuu Tanzania
    Maelezo ya picha, Wakaazi wakipiga kura ya uchaguzi mkuu Tanzania

    Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar, Thabit Aidarous, amewahakikishia wananchi wa visiwa hivyo kwamba matokeo rasmi ya uchaguzi yatatangazwa kesho jioni.

    Vituo vya kupigia kura vilifungwa saa kumi jioni, na hadi sasa hakujaripotiwa matatizo yoyote ya mfumo wa kusambaza matokeo kufuatia intaneti kuminywa hadi Tanzania Bara.

    Aidarous amesema kuwa hatua hiyo imetokana na maandalizi mazuri waliyofanya mapema, ikiwemo kutumia mtandao wa ndani (intranet) ambao haujapata hitilafu za kiufundi.

    “Tulijipanga mapema. Tuna mfumo wa intranet ambao haujapata matatizo ya kiufundi,” alisema Aidarous.

    Katika uchaguzi huu, wananchi wa Zanzibar wanapiga kura kumchagua Rais wa Zanzibar, Rais wa Muungano, Wabunge, na Madiwani.

    Laila Rajab amekuwa mgombea pekee wa urais mwanamke visiwani Zanzibar, na wa kwanza katika historia yote ya uchaguzi wa visiwa hivyo. Hatua yake imevunja ukimya wa miaka mingi ulioweka uongozi wa juu mikononi mwa wanaume.

    Laila ni mgombea wa chama cha NCCR-Mageuzi, moja kati ya vyama 11 vilivyosimamisha wagombea wa urais Zanzibar mwaka huu.

    Pia unaweza kusoma:

  3. Uchaguzi mkuu Tanzania 2025: Muunganisho wa mtandao Tanzania watatizika

    Picha inaonyesha mawimbi ya mitandao ikisuasua

    Chanzo cha picha, NetBlocks/X

    Maelezo ya picha, Picha inaonyesha mawimbi ya mitandao ikisuasua

    Kwa mujibu wa data kutoka kwa shirika la mitandao NetBlocks imethibitisha kukatika kwa huduma za intaneti kote nchini Tanzania siku ya uchaguzi mkuu wa Tanzania unaofanyika Jumatano ya tarehe 29 mwezi Oktoba 2025.

    Tukio hili limejiri wakati raia wa Tanzania wanaposhiriki kuchagua Rais mpya, wabunge, madiwani huku vyama vikuu vya upinzani kama Chadema vikisusia uchaguzi huo wakidai mageuzi ya sheria za uchaguzi.

    Hii imeshatokea mara kadhaa katika nchi mbalimbali na hata Tanzania na haswa wakati wa Uchaguzi wa 2020 mtandao ulifungwa.

    Tanzania, mijadala kuhusu kufungia X imekuwa ikijirudia, hasa baada ya wito wa baadhi ya viongozi mwaka 2024.

    Soma pia:

  4. Habari za hivi punde, Uchaguzi mkuu Tanzania 2025: Amri ya kutotoka nje yatangazwa Dar es Salaam

    Picha ya Inspekta jenerali wa polisi Tanzania Camillus Wambura

    Chanzo cha picha, Camillus Wambura/X

    Maelezo ya picha, Picha ya Inspekta jenerali wa polisi Tanzania Camillus Wambura

    Inspekta Jenerali wa Polisi Tanzania ametangaza amri ya kutotoka nje jijini humo kuanzia leo saa kumi na mbili jioni.

    ''Jeshi la polisi kufuatia hali hiyo inawatangazia wakaazi wote wa jiji la Dar es Salaam kuwa kuanzia leo tarehe 29 Oktoba mwaka 2025 kuanzia saa kumi na mbili jioni wawe majumbani mwao,'' alisema Camillus akitoa tangazo hilo.

    Ni kauli ambayo imekaririwa na Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salam Jumanne Muliro akisema kuwa ni maafisa wa polisi watakaokuwa wakishika doria wabaki mitaani.

    Hayo ni kufuatia matukio ya ghasia yaliyoshuhudiwa katika maeneo kadhaa mjini Dar Es Salam na kwingineko nchini humo ambapo waandamanaji wanaopinga kufanyika kwa uchaguzi wameandamana wakifunga barabara kadhaa na kuchoma moto maeneo kadhaa.

    Soma pia:

  5. Watu kadhaa wajeruhiwa kwenye makabiliano na polisi

    Majeruhi

    Watu kadhaa wamejeruhiwa kwenye maandamano katika baadhi ya miji ya Tanzania huku shughuli ya upigaji kura ukiendelea katika uchaguzi mkuu ambao umekumbwa na mvutano.

    Waandamanaji waliwasha moto barabarani, kuharibu mabasi, na kusababisha uharibifu mkubwa kwenye vituo vya mabasi ya mwendo kasi na miundombinu mingine ya umma.

    Tumechoka... Tunataka Tume huru ya uchaguzi ili Watanzania wamchague kiongozi wanayemtaka, mmoja wa waandamanaji aliiambia BBC.

    Zaidi ya wapiga kura milioni 37 waliosajiliwa kupiga kura katika uchaguzi wa urais na ubunge.

    Vyama 16 vidogo, ambavyo havina umaarufu, vimeruhusiwa kugombea urais dhidi ya Rais Samia, ambaye anawania muhula wa pili.

    Mgombea pekee wa upinzani, Luhaga Mpina wa Chama cha ACT-Wazalendo, alienguliwa kutokana na taratibu za kisheria.

    ,
    ,
  6. Maandamano yasambaa katika baadhi ya maeneo Dar es Salaam

    Waandamanaji

    Maandamano katika jiji la Dar es Salaam yanazidi kusambaa kutoka Kimara na yameingia eneo la Magomeni.

    Mapema asubuhi vikundi vya vijana vilianza kujikusanya katika eneo la Kimara Kibo kabla ya kuingia barabarani kuziba barabara kabla ya kukabiliana na Polisi.

    Maandamano yameshuhudiwa Kimara, Magomeni, Ubungo, Kinondoni, Shekilango na Tandale.

    Uharibifu mkubwa umeshuhudiwa kwa vituo vya mabasi ya mwendokasi, vituo vya kupigia kura, mabasi, na maeneo ya biashara.

    ,

    Awali Mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila alionya kuwa vyombo vya dola viko imara kukabiliana na uvunjifu wa amani.

    Maelezo zaidi:

  7. Uchaguzi Tanzania: Serikali yatoa onyo uvunjifu wa amani

    Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Alfred Chalamila

    Chanzo cha picha, Daily News

    Maelezo ya picha, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Alfred Chalamila

    Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Alfred Chalamila, amesema vyombo vya dola viko imara na tayari kukabiliana na jaribio lolote la uvunjifu wa amani katika jiji hilo, akisisitiza kuwa Serikali haitasita kuchukua hatua kali dhidi ya mtu au kikundi chochote kitakachojaribu kuvuruga utulivu.

    Kauli hiyo imekuja kufuatia taarifa za uwepo wa kundi la vijana waliodaiwa kujaribu kuandamana katika eneo la Kibo, Kimara, kabla ya polisi kuwatawanya.

    “Hata mkiona kuna propaganda za aina yoyote kwenye mitandao kuhusu eneo lolote la Mkoa wa Dar es Salaam, mjue nguvu itakayotumika kudhibiti jambo hilo ni mara saba zaidi ya nguvu iliyotumika kulipanga,” alisema Chalamila.

    Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kupiga kura, Chalamila alisisitiza umuhimu wa kulinda utamaduni wa amani ambao Tanzania imeujenga kwa miaka mingi, na kuwataka wananchi waendelee kuiamini Serikali yao pamoja na vyombo vya usalama.

    “Utamaduni wa taifa letu ni amani. Tukiiharibu amani hii, kwa lugha nyepesi, tutakuwa tumepoteza msingi wa kuwepo kwetu kama taifa. Nimetembea maeneo mbalimbali kuwaambia vijana wajitokeze kutumia haki yao ya msingi ya kupiga kura, lakini wafanye hivyo kwa amani,” alisema.

    Chalamila pia alitoa wito kwa wananchi wa Dar es Salaam kuendelea kushirikiana na Serikali kuhakikisha jiji hilo linaendelea kuwa kitovu cha utulivu, maendeleo na mshikamano wa kitaifa.

    Soma pia:

  8. Rais Samia apiga kura jijini Dodoma

    Rais Samia

    Chanzo cha picha, Ikulu Tanzania

    Mgombea wa Urais kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) Samia Suluhu Hassan akishiriki zoezi la kupiga kura ya kumchagua Rais,Mbunge na Diwani, eneo la Chamwino, jijini Dodoma leo tarehe 29, Oktoba 2025.

    Akiwa kwenye foleni

    Chanzo cha picha, Ikulu Tanzania

    Rais Samia

    Chanzo cha picha, Ikulu Tanzania

  9. Mgombea mwenza kupitia CCM, Balozi Dkt.Nchimbi apiga kura

    Balozi Dkt. Emmanuel John Nchimbi

    Chanzo cha picha, CCM

    Mgombea mwenza wa Urais kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) Balozi Dkt. Emmanuel John Nchimbi akishiriki zoezi la kupiga kura ya kumchagua Rais,Mbunge na Diwani katika mtaa wake, eneo la Kilimani, jijini Dodoma leo tarehe 29, Oktoba 2025.

    Akiwa kwenye foleni
    DKT. Nchimbi

    Chanzo cha picha, CCM

  10. Mgombea Urais UDP: Nikipata, nikishindwa nitapokea

    Mgombea Urais UDP, Saum Rashid

    "Nikishinda kura ya urais nitapokea, nikishindwa nitamuunga mkono na kumpongeza yoyote atakayeshinda," amesema Mgombea urais kupitia chama cha UDP, Saum Rashid mara baada ya kupiga kura.

    Akizungumza, mapema leo baada ya kupiga kura jijini Dar es Salaam , Saumu alisema ametimiza wajibu wake wa kikatiba na kwamba kura zitaamua.

    Alisema kuwa iwapo kura hazitatosha basi atajipanga na uchaguzi mwingine.

    Hatahivyo, Saumu amedai kuridhishwa na utaratibu uliowekwa wa kupiga kura. "Utaratibu uliowekwa na tume ya uchaguzi unaridhisha.

    Mimi sasa nasubiri matokeo, nina imani na tume itatenda haki," alisema mgombea huyo.

    Katika uchaguzi unaoendelea, wagombea uraisi 17 walijitokeza kugombea nafasi hiyo. Kwa mujibu wa Tume Huru ya Uchaguzi, matokeo ya urais yatatangazwa ndani ya saa 72.

    Maelezo zaidi:

  11. Polisi wakabiliana na 'waandamanaji' Dar es Salaam

    s

    Polisi jijini Dar es Salaam wametawanya kundi la vijana waliokuwa wakijaribu kuandamana katika eneo la Kimara Kibo, umbali wa kati ya Ubungo na Kimara, wakati huu wa uchaguzi mkuu unaoendelea nchini.

    Mashuhuda wamesema kundi hilo la vijana lilianza kujikusanya karibu na Kanisa la Ufufuo na Uzima, ambalo lilifungiwa hivi karibuni. Kanisa hilo la Askofu Josephat Gwajima, ambaye alikuwa mbunge wa chama tawala, CCM, kuanzia mwaka 2015 hadi mwaka huu. Gwajima amekuwa akijulikana kwa misimamo yake ya kupinga vitendo vya utekaji na ukiukwaji wa haki za binadamu, hatua ambayo iliwahi kumuweka kwenye mvutano na mamlaka za serikali.

    Maelezo ya video, Polisi wakabiliana na 'waandamanaji' jijini Dar es Salaam

    Hadi kufikia muda huu, polisi wanaendelea kudhibiti hali ya eneo hilo huku magari ya doria yakionekana katika barabara kuu ya Morogoro Road. Hakuna taarifa rasmi za majeruhi wala idadi kamili ya waliokamatwa.

    Maandamano haya ni sehemu ya mwitikio wa mitandaoni wa makundi ya wanaharakati na vijana wakitaka mageuzi zaidi ya kisiasa. Hata hivyo, hadi sasa, maandamano hayo yalikuwa hayajashuhudiwa kwa kiwango kikubwa nchini kote.

    s
  12. Watu milioni 37.6 wanatarajiwa kupiga kura leo

    Wapiga kura

    Watu milioni 37.6 wanatarajiwa kupiga kura katika uchaguzi wa mwaka huu.

    Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC) imesema jumla ya Watanzania milioni 37.6 wameandikishwa kupiga kura kwa ajili ya uchaguzi wa mwaka huu.

    Kati yao, milioni 36.65 wapo Tanzania Bara na takribani 996,000 wapo Zanzibar.

    Takwimu

    Wanawake ni asilimia 50.34 ya wapiga kura wote, sawa na watu milioni 18.95, huku wanaume wakiwa 49.66%. Mwenyekiti wa INEC, Jaji wa Rufani Jacob Mwambegele, amesema kati ya wapiga kura hao, milioni 7.6 ni wapya, ikionesha ongezeko la zaidi ya asilimia 26 kutoka uchaguzi wa mwaka 2020.

    Tume imesema idadi hiyo kubwa ya wapiga kura ni kielelezo cha mwamko wa kisiasa unaoongezeka nchini, hasa miongoni mwa vijana.

  13. Spika wa Bunge la Tanzania apiga kura Mbeya

    Tulia Ackson

    Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mgombea Ubunge Jimbo la Uyole kupitia Chama cha Mapinduzi (CCM), Dkt.Tulia Ackson, leo tarehe 29 Oktoba, 2025 amejitokeza kupiga kura katika kituo cha Shule ya Msingi Tambukareli mkoni Mbeya.

    Tulia
  14. Rais Mwinyi apiga kura Zanzibar

    Dkt Mwinyi

    Rais Dkt. Hussein Mwinyi amepiga kura yake katika kituo cha Kariakoo jimbo la Kwahani.

    Rais Dkt Mwinyi

    Zaidi ya wapiga kura 700,000 waliojiandikisha wanatarajiwa kupiga kura zao katika uchaguzi mkuu ambao hadi sasa umebaki shwari kwa kiasi kikubwa katika visiwa hivyo, ambavyo vina historia ya mashindano ya kisiasa yenye mvutano.

  15. Shughuli za upigaji kura Arusha ni tulivu

    a
    Maelezo ya picha, Mkuu wa mkoa wa Arusha, Amos Makalla

    Mkoa wa Arusha kuna utulivu shughuli za upigaji kura zikiendelea. Kwa mujibu wa mwandishi wetu jijini humo, ametueleza kuwepo kwa utulivu mkubwa, mtu mmoja mmoja wakionekana mtaani.

    Mkuu wa Mkoa huo, Amos Makalla alikuwa miongoni mwa waliojitokeza mepema mara baada ya vituo kvya kura kufunguliwa.

    Mkuu huo wa mkoa alipiga kura katika kituo cha AICC Hospitali.

    s
    Maelezo ya picha, Mkuu wa mkoa wa Arusha, Amos Makalla (kulia) akipanga mstari kwenda kupiga kura kwenye kituo cha AICC Hospitali
    s
    s
    s
  16. Upigaji kura waanza rasmi

    a

    Shughuli za upigaji zimeanza rasmi katika maeneo mengi ya nchi. Katika maeneo ya miji ya Dar es Salaam, Arusha, Kilimanjaro, Mbeya, Zanzibar, Tanga wapiga kura wameonekana wakifika vituoni tangu mapema alfajiri.

    Maafisa wa uchaguzi katika maeneo hayo wanasema vituo vimefunguliwa kwa wakati, na kuhimiza kufuatwa kwa taratibu zote ikiwemo uhakiki wa wapiga kura kwa njia ya kielektroniki (BVR).

    Baadhi ya wapiga kura wameeleza kufurahishwa na maandalizi ya tume na kuhimiza wananchi wenzao kujitokeza kwa wingi kutekeleza haki yao ya kikatiba.

    Awali Tume ya Taifa ya Uchaguzi ya Uchaguzi (INEC) ilitoa wito kwa wapiga kura kutokaa majumbani na kuendelea kujitokeza hadi muda wa kufunga vituo utakapofika saa 10:00 jioni.

  17. Siku ya pili ya upigaji kura Zanzibar

    Visiwani Zanzibar

    Leo ni siku ya pili ya upigaji kura Zanzibar. Jumla ya vituo 1,756 vya kupigia kura kote Unguja na Pemba vimefunguliwa saa 6:00 asubuhi na kufungwa saa 12:00 asubuhi.

    Zaidi ya wapiga kura 700,000 waliojiandikisha wanatarajiwa kupiga kura zao katika uchaguzi mkuu ambao hadi sasa umebaki shwari kwa kiasi kikubwa katika visiwa hivyo, ambavyo vina historia ya mashindano ya kisiasa yenye mvutano.

    Wapiga kura

    Mchuano mkuu ni kati ya mgombea wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dkt. Hussein Mwinyi, na mgombea wa ACT-Wazalendo, Othman Masoud Othman.

    Dkt. Mwinyi anatarajiwa kupiga kura yake katika kituo cha kupigia kura cha Kariakoo saa 2:00 asubuhi, huku Othman Masoud akipiga kura katika kituo cha kupigia kura cha Mpendaye.

    Matokeo yanatarajiwa kutangazwa ndani ya saa 24.

    Rais aliye madarakani Hussein Ali Mwinyi anaangazia rekodi ya kuvutia ya maendeleo ya miundombinu, ikiwa ni pamoja na majengo ya shule ya hali ya juu, vituo vya afya vya kisasa, na mtandao wa kilomita mia kadhaa za barabara katika visiwa hivyo.

    Kwa upande mwingine, upinzani umejikita katika ahadi za kutokomeza ufisadi, ambao unadai umekuwa mkubwa sana chini ya utawala wa sasa unapotekeleza miradi yake ya miundombinu iliyotangazwa sana.

    ACT Wazalendo pia imeapa kushinikiza uhuru zaidi kwa Zanzibar, ikisema kwamba maendeleo ya visiwa hivyo yamezuiwa na hitaji la kutafuta idhini kutoka kwa serikali ya bara kuhusu maamuzi mengi muhimu.

    Uhakiki
  18. Vituo vya kupigia kura kufunguliwa saa moja asubuhi

    s
    Maelezo ya picha, Maafisa wa Uchaguzi katika Kituo cha Viwandani, WEO, namba moja jijini Dodoma

    Kwa mujibu wa Tume yta Taifa ya Uchaguzi, Vituo vya kupigia kura vinafunguliwa saa moja kamili asubuhi.

    Katika maeneo Mbalimbali ya nchi, kumeonekana maandalizi yakiendelea kwa maafisa wa uchaguzi kuandaa mazingira ya kupigia kura.

    Na katika baadhi ya maeneo tayari watu wanaonekana kusogea vituoni tayari kwa ajili ya kupiga kura. Picha chini ni Maafisa wa Uchaguzi katika Kituo cha Viwandani, WEO, namba moja jijini Dodoma wakiendelea na maandalizi ya mwisho.

    a
    A
    Msimamizi
    Uchaguzi
  19. Watanzania wanapiga kura leo

    S

    Watanzania wanapiga kura leo katika Uchaguzi Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ambapo Rais Samia Suluhu Hassan wa chama tawala Chama Cha Mapinduzi (CCM) anatazamiwa kutetea nafasi yake kwa muhula mwingine wa miaka mitano.

    Ni uchaguzi wa saba tangu kurejeshwa kwa mfumo wa vyama vingi mwaka 1992, na unafanyika wakati vyama vikuu vya upinzani vikiwa na misimamo tofauti kuhusu ushiriki wao katika mchakato huu.

    Chama kikuu cha upinzani, CHADEMA, hakishiriki uchaguzi huo kikishinikiza mabadiliko ya mfumo wa uchaguzi, wakidai unakipendelea chama tawala.

    Wakati huo huo, chama cha ACT-Wazalendo hakina mgombea urais baada ya Luhaga Mpina kuenguliwa na Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC) kwa kutokidhi matakwa ya kikanuni.

    Kwa mujibu wa INEC, vituo vya kupigia kura vinafunguliwa saa 1:00 asubuhi na vitafungwa saa 10:00 jioni kabla ya kuanza kwa zoezi la kuhesabu kura mara moja baada ya upigaji kura kukamilika.

    Hapo jana, wakaazi wa visiwa vya Zanzibar walipiga kura ya mapema kwa makundi maalum ikiwemo askari, maafisa wa tume na wahudumu wa afya. Tume imesema maandalizi yote yamekamilika na imewataka wapiga kura kufika vituoni mapema ili kuepuka msongamano.

  20. Habari na karibu katika matangazo yetu ya moja kwa moja kuhusu Uchaguzi Mkuu wa Tanzania