Marekani imetangaza ushuru mpya kwa washirika wake
60 wa kibiashara, wanaowakilisha sehemu kubwa ya
bidhaa zinazoingizwa nchini humo, kwa madai kwamba hawajachukua
hatua za kutosha kukomesha ajira za kulazimishwa.
Ushuru huo, unaoanzia asilimia 10 hadi 12.5,
unazihusu nchi na maeneo muhimu ya kiuchumi, ikiwemo Uingereza,
China, Umoja wa Ulaya, Canada, Japan na India.
Unaanza kufanya kazi Ijumaa,
baada ya ushuru wa muda wa asilimia 10 uliowekwa mapema mwaka
huu kumalizika.
Hatua hiyo ni mwendelezo wa mvutano wa vita
vya kibiashara uliochochewa tena na Rais wa Marekani Donald
Trump baada ya kurejea madarakani mwaka jana.
Mapema mwaka huu, Mahakama Kuu ya Marekani iliamua
kuwa ushuru mwingi uliowekwa duniani chini ya mamlaka ya dharura
ulikuwa umeanzishwa kinyume cha sheria.
Tangu uamuzi huo, Trump amekuwa akitafuta njia
nyingine za kutekeleza sera yake kuu ya biashara.
Mwezi uliopita, Ikulu ya Marekani
ilipendekeza ushuru wa asilimia 10 hadi 12.5 kwa bidhaa
kutoka mataifa kadhaa, ikidai hayafanyi juhudi za kutosha
kukabiliana na ajira ya kulazimishwa.
Siku ya Alhamisi, Mwakilishi wa Biashara wa
Marekani, Jamieson Greer, alisema ushuru huo utaanza kutekelezwa
kwa maelekezo ya Rais Trump.
Katika taarifa yake alisema hatua hiyo italenga
kurekebisha ukiukwaji wa haki za binadamu na biashara isiyo ya haki, huku
ikilenga kuboresha ustawi wa wafanyakazi duniani.
Ushuru huo mpya utawahusu washirika 60 wakuu wa biashara wa Marekani, ambao kwa pamoja wanachangia asilimia 99.4 ya bidhaa zote zinazoingizwa nchini humo, kwa mujibu wa mamlaka za Marekani.
Ofisi ya Mwakilishi wa Biashara wa Marekani ilisema kuwa Rais Donald Trump ameifanya marufuku ya uagizaji wa bidhaa zinazozalishwa kwa kutumia ajira ya kulazimishwa kuwa sehemu muhimu ya makubaliano ya biashara ya pande mbili na mataifa mengine.
Kwa mujibu wa ofisi hiyo, hadi sasa washirika 10 wa kibiashara wamekubali kuweka marufuku hiyo katika makubaliano yao na Marekani, huku mataifa mengine yakichukua hatua kama hizo kufuatia uchunguzi uliofanywa katika wiki za hivi karibuni.
Mataifa ambayo yameahidi kutunga na kutekeleza kikamilifu marufuku ya bidhaa zinazotokana na ajira ya kulazimishwa yatatozwa ushuru wa asilimia 10. Nchi ambazo hazijatoa ahadi hiyo zitatozwa ushuru wa juu zaidi wa asilimia 12.5.
Mwakilishi wa Biashara wa Marekani, Jamieson Greer, alisema ameridhishwa na hatua za haraka zilizochukuliwa na baadhi ya washirika wa biashara kupiga marufuku bidhaa zinazozalishwa kwa ajira ya kulazimishwa, na akaeleza kuwa anatarajia kuhakikisha hatua hizo zinatekelezwa ipasavyo.