Moja kwa moja, Marekani inaendelea na Mazungumzo na Iran huku mashambulizi yakisitishwa - Trump

Hata hivyo, ameonya kuwa iwapo mazungumzo hayo hayatakuwa na mafanikio, Marekani "itarejea kufanya kile tulichokuwa tukifanya" kabla ya kusitishwa kwa mashambulizi.

Muhtasari

Ruka Video uendelee
  • .
  • xx
  • xx
  • xx
  • Lungu
  • xx
  • xx
  • d
  • s
  • a
  • Sonko
  • xx
  • xx
  • xx
  • xx
  • xx
  • Dangote
  • xx
  • Lydia Wanjiku

Moja kwa moja

Na Asha Juma

  1. Twiga Stars yaandika historia kwa kuifunga Afrika Kusini WAFCON 2026

    D

    Chanzo cha picha, CECAFA

    Tanzania imeandika historia kwa kupata ushindi wake wa kwanza kabisa katika Kombe la Mataifa ya Afrika kwa Wanawake (WAFCON) baada ya kuifunga mabingwa wa mwaka 2022, Afrika Kusini, mabao 2 kwa 1 katika mchezo wa ufunguzi wa Kundi B.

    Twiga Stars ilitoa moja ya matokeo ya kushangaza zaidi katika mashindano hayo baada ya kuonyesha mchezo wa nidhamu na ujasiri dhidi ya Banyana Banyana, huku Hasnath Ubamba akifunga bao la ushindi dakika ya 87.

    Diana Msewa aliitanguliza Tanzania mbele dakika ya 37 baada ya Twiga Stars kuanza mchezo kwa kasi na kulisukuma lango la Afrika Kusini mara kwa mara.

    Hata hivyo, Bambanani Mbane aliisawazishia Afrika Kusini katika muda wa nyongeza wa kipindi cha kwanza, na kuifanya timu hizo ziende mapumziko zikiwa sare ya bao 1 kwa 1.

    Kipindi cha pili kilikuwa na ushindani mkubwa huku Afrika Kusini ikitafuta bao la ushindi, lakini Twiga Stars iliendelea kujilinda kwa umakini na kutumia mashambulizi ya kushtukiza.

    Dakika ya 87, Hasnath Ubamba aliyeingia akitokea benchi aliifungia Tanzania bao la ushindi, lililozua shangwe kubwa miongoni mwa wachezaji, benchi la ufundi na mashabiki.

    Ushindi huo ni hatua muhimu kwa soka la wanawake Tanzania. Kabla ya mchezo huo, Twiga Stars ilikuwa imecheza mechi sita za WAFCON bila kushinda, ikipata sare moja na kupoteza tano.

    Matokeo hayo pia yanaongeza matumaini ya Tanzania kutinga hatua ya mtoano kwa mara ya kwanza katika historia ya mashindano hayo.

    Kwa upande wa Afrika Kusini, mabingwa wa mwaka 2022 wameanza vibaya kampeni yao ya kutwaa ubingwa kwa mara nyingine, na sasa watakuwa chini ya shinikizo la kupata matokeo mazuri katika mechi zao zilizosalia za Kundi B ili kujiweka katika nafasi nzuri ya kufuzu hatua inayofuata.

    Kwa Twiga Stars, ushindi huo dhidi ya moja ya timu zenye nguvu zaidi barani Afrika unaweza kuwa chachu ya kujiamini katika harakati za kuandika historia nyingine kwenye WAFCON 2026.

    Wakati huo huo, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, ameipongeza Timu ya Taifa ya Wanawake ya Tanzania, Twiga Stars, kwa kuanza vyema michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika kwa Wanawake (WAFCON) 2026 nchini Morocco.

    “Ninaungana na Watanzania wote kuitakia kila la kheri Twiga Stars inapoendelea kupeperusha bendera ya Taifa letu katika michezo inayofuata. Endeleeni kupambana kwa moyo huo huo, mkionyesha uzalendo, nidhamu na ari ya ushindani inayolitangaza vyema Taifa letu,” amesema Rais Samia Suluhu Hassan.

    Fuatilia hapa:

    d

    Chanzo cha picha, cecafa

  2. Dunia iko katika hatari ya kuongezeka kwa maambukizi ya VVU - UNAIDS

    .

    Chanzo cha picha, AFP via Getty Images

    Shirika la Umoja wa Mataifa linalopambana na UKIMWI limesema dunia iko katika hatari ya kushuhudia kuongezeka tena kwa janga la maambukizi ya VVU baada ya ufadhili wa kimataifa kupunguzwa kwa karibu asilimia 20 mwaka uliopita.

    Katika ripoti iliyotolewa kuadhimisha ufunguzi wa Mkutano wa Kimataifa wa UKIMWI nchini Brazil, UNAIDS ilisema ufadhili ulipungua hadi takriban dola bilioni saba za Marekani, kiwango cha chini zaidi katika karibu miongo miwili.

    "Ni ripoti inayoonyesha mambo mawili, kwanza ni kuhusu maendeleo ya kisayansi na pili ni onyo kwamba kuondolewa kwa misaada inaleta kukosekana kwa usawa kunakoathiri haki za binadamu. Na kuweka maisha katika miongo kadhaa hatarini," amesema Winifred Byanyima, Mkurugenzi Mtendaji wa UNAIDS.

    Byanyima ameongeza kuwa kwa sasa matwakwa ya kisiasa ndio yanayoamua namna ya kupambana na virusi vya UKIMWI na si masuala ya kisayansi

    "Swali sio tena kama tunaweza kumaliza UKIMWI, bali ni je, tunachagua kumaliza Ukimwi. Harakati za kupambana na ukimwi kwa sasa hazikumbwi na changamoto za kisayansi bali zinakabiliwa na kukosekana kwa usawa kutokana na msukumo wa kisiasa. Kama tunatokomeza ukimwi haitaamuliwa maabara, basi ni matwaka ya kisiasa," amesema Byanyima.

    Marekani ilikuwa ikichangia takriban robo tatu ya ufadhili wa kimataifa wa mapambano dhidi ya VVU kabla ya Rais Trump kurejea madarakani mnamo Januari 2025.

  3. Moto wa nyika: Macron asema Ufaransa inakabiliwa na hali mbaya zaidi tangu Vita vya Pili vya Dunia

    .

    Chanzo cha picha, EPA/Shutterstock

    Rais wa Ufaransa, Emmanuel Macron, ameahidi kutumia kila rasilimali iliyopo kupambana na moto mkubwa wa nyika unaoendelea nchini humo akisema janga hilo ni mbaya zaidi kuwahi kuikumba Ufaransa tangu Vita vya Pili vya Dunia.

    Rais wa Ufaransa, Emmanuel Macron, ameonya kuwa hali itaendelea kuwa ngumu zaidi alipokuwa akitembelea kituo cha operesheni za kuzima moto katika eneo la Gironde, ambalo limeathiriwa vibaya na moto huo uliosababisha mioto mikubwa isiyoweza kudhibitiwa.

    Akizungumza na vikosi vya zimamoto na wahudumu wa dharura, Macron alisema:

    "Tunakabiliwa na hali ngumu zaidi kuwahi kushuhudiwa, hali ambayo haijawahi kutokea tangu Vita vya Pili vya Dunia."

    Aliongeza kuwa msimu wa moto wa nyika, ambao kwa kawaida hufikia kilele mwezi Agosti, bado haujaanza kikamilifu.

    Rais Macron ameonya kuwa viwango vya joto vinatarajiwa kupanda tena, akisisitiza kuwa cha msingi kwa sasa ni kuokoa maisha.

    Wakati huo huo, wazima moto nchini Uhispania wamekuwa wakipambana kudhibiti baadhi ya moto mbaya zaidi wa nyika katika historia ya hivi karibuni ya nchi hiyo huku kukiwa na onyo la wimbi kubwa la joto linaloongezeka ambalo linaweza kuzorotesha zaidi hali hiyo.

    Viwango vya joto katika baadhi ya maeneo ya nchi hiyo vinatarajiwa kuwa ya juu zaidi.

    Waziri Mkuu, Pedro Sanchez, ameonya kuwa ni wakati mgumu kwa nchi yake huku akitoa wito kwa vyama vya kisiasa kuweka kipaumbele katika kuunda mkataba wa kitaifa wa dharura wa kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.

    Soma Zaidi:

  4. Johnson & Johnson yajitolea kulipa hadi $5.5bn kumaliza kesi za poda ya watoto

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Kampuni ya Johnson & Johnson (J&J) imejitolea kulipa hadi dola bilioni 5.5 (pauni bilioni 4.14) ili kumaliza maelfu ya kesi zinazodai poda yake ya watoto pamoja na bidhaa nyingine zenye madini ya talcum husababisha saratani ya ovari au kifuko cha mayai.

    Makubaliano hayo makubwa yanakusudia kumaliza mzozo wa kisheria uliodumu kwa miaka kadhaa na kuendelea kuigharimu kampuni hiyo kubwa ya huduma za afya nchini Marekani.

    J&J imeendelea kusisitiza kuwa bidhaa zake zenye talcum hazisababishi saratani, na tayari imebadilisha viambato vya poda yake ya watoto inayotumiwa na watu wengi.

    Makamu wa Rais wa masuala ya kesi za kisheria wa kampuni hiyo, Erik Haas, alisema Jumatatu kuwa madai hayo "hayana msingi", na kwamba J&J imeamua kufikia makubaliano ili kutatua kabisa suala hilo.

    Kampuni hiyo imesema makubaliano hayo yatahusisha takriban kesi 69,000, ambazo ni sehemu kubwa ya madai yaliyosalia yanayohusiana na bidhaa za talcum. J&J imeeleza kuwa italipa hadi dola bilioni 3 mwaka ujao, na kusitarajiwe malipo mengine kabla ya mwaka 2028.

    J&J pia imesema pendekezo hilo litalazimika kukubaliwa na kampuni za mawakili zinazowawakilisha asilimia 95 ya walalamishi wa kesi za saratani ya ovari katika mahakama za majimbo na za shirikisho, kabla ya makubaliano hayo kukamilika.

    Katika taarifa yake, Haas alisema kampuni ina imani kuwa ingeibuka mshindi endapo kesi hizo zingeendelea mahakamani, kama ilivyofanikiwa katika kesi nyingi ambazo tayari zimeamuliwa.

    Aliongeza kuwa makubaliano hayo yataiwezesha kampuni kuhitimisha suala hilo na kuelekeza nguvu zake katika jukumu lake la kutengeneza dawa na vifaa vya tiba vinavyookoa maisha.

    Soma Zaidi:

  5. Mazungumzo ya vita vya Iran yanaendelea huku mashambulizi yakisitishwa - Trump

    .

    Chanzo cha picha, Reuters

    Rais wa Marekani, Donald Trump, amesema kuwa kuna "mazungumzo ya kirafiki yanayoendelea" kuhusu mzozo wa Iran, baada ya pande zinazopigana kutoshambuliana kwa siku ya tatu mfululizo.

    Akiwa ndani ya ndege ya Air Force One siku ya Jumatatu, Trump alieleza matumaini yake kwamba vita hivyo vinaweza kufikia mwisho. Aliwaambia waandishi wa habari: "Ninaamini kuna uwezekano mkubwa jambo fulani likatokea."

    Alionyesha matumaini kwamba vita vinaweza kumalizika Jumatatu, akiwaambia waandishi wa habari ndani ya ndege ya Air Force One: "Nafikiri kuna fursa nzuri ya kutokea kwa jambo fulani."

    Hata hivyo, alionya kuwa iwapo mazungumzo hayo hayatakuwa na mafanikio, Washington "itarejea kufanya kile tulichokuwa tukifanya" kabla ya kusitishwa kwa mashambulizi.

    Kwa upande wake, Tehran imekanusha kuwa kuna mazungumzo yoyote ya moja kwa moja yanayoendelea.

    Trump alisema aliamua kusitisha mashambulizi ya Marekani dhidi ya Iran siku ya Ijumaa baada ya nchi zinazosaidia kupatanisha pande hizo kumwomba kutoa fursa nyingine kwa mazungumzo.

    Iran pia imesitisha mashambulizi yake.

    Hatua hiyo inafuatia karibu wiki mbili za mashambulizi ya kila siku ya Marekani na ya kulipizana kisasi kati ya pande hizo, hali iliyovuruga kwa kiasi kikubwa makubaliano ya usitishaji mapigano yaliyofikiwa mnamo mwezi Juni.

    Wakati huo, jeshi la Marekani lilisema mashambulizi yake yalilenga kupunguza uwezo wa Iran wa kuhatarisha usafirishaji wa meli za kibiashara katika Mlango Bahari wa Hormuz, ambao ni njia muhimu duniani ya usafirishaji wa mafuta.

    Soma Zaidi Hapa:

  6. Hujambo Msomaji wetu. Karibu katika matangazo yetu mubashara tarehe ni 28/07/2026.