Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Moja kwa moja, Trump asema alitumia ndege ya kijeshi kwa kuhofia Iran

Maafisa waliiambia CBS News, mshirika wa BBC nchini Marekani, kwamba Marekani ilikuwa imegundua tishio la kuaminika kutoka Iran la kulenga ndege hiyo kwa kombora.

Moja kwa moja

Na Mariam Mjahid

  1. Cristiano Ronaldo amuoa Georgina Rodríguez baada ya miaka 10

    Nyota wa soka Cristiano Ronaldo amemuoa mpenzi wake wa muda mrefu, mwanamitindo na mshawishi Georgina Rodríguez, katika hafla ya kiraia nchini Ureno.

    Ronaldo alichapisha picha kwenye akaunti yake ya Instagram ikionyesha mikono miwili, unaodhaniwa kuwa wake ukiwa juu ya wa mke wake, huku wote wakiwa wamevalia pete za ndoa.

    Vyombo vya habari nchini Ureno vimeripoti kuwa wawili hao walifunga ndoa tarehe 11 Agosti katika mji wa pwani wa Cascais, karibu na Lisbon, huku watoto wao watano wakihudhuria.

    Picha hiyo ilipata uungwaji mkono wa mitandaoni milioni tatu ndani ya dakika 30 baada ya kuchapishwa.

    Ronaldo na Rodríguez wamekuwa pamoja kwa miaka 10, baada ya kukutana katika duka la Gucci mjini Madrid, ambako Rodríguez alikuwa akifanya kazi. Wakati huo Ronaldo alikuwa akiichezea Real Madrid.

    Wawili hao walitangaza uchumba wao tarehe 11 Agosti mwaka jana.

    Ronaldo amefunga karibu mabao 1,000 katika maisha yake ya soka, akichezea Sporting Lisbon, Manchester United, Real Madrid, Juventus, Al Nassr ya Saudi Arabia na timu ya taifa ya Ureno.

    Hivi karibuni alishiriki katika Kombe lake la Dunia la sita, rekodi ya ushiriki katika fainali za Kombe la Dunia kwa upande wa wanaume, ambayo anaishikilia pamoja na Lionel Messi wa Argentina.

  2. Mwanamke aliyezikwa na vifusi aokolewa akiwa hai baada ya saa 36

    Kwa mujibu wa Idara ya Zimamoto ya Bogotá, timu za uokoaji zimemtoa mwanamke akiwa hai baada ya kunaswa chini ya vifusi kwa saa 36 katika mji wa Pereira.

    Waziri wa Mambo ya Ndani wa Colombia, Rodrigo Lara, amesema katika ujumbe kwenye mtandao wa X kwamba Daniela Largo Sanchez, mwenye umri wa miaka 32, alipatikana chini ya vifusi vya hoteli.

    Mwanamke huyo alihamishiwa mara moja katika kituo cha afya cha eneo hilo, ambako anaendelea kupatiwa matibabu.

    Kwa mujibu wa Rais Abelardo de la Espriella, waokoaji mjini Pereira bado wanaendelea kuwatafuta zaidi ya watu 40 ambao hawajulikani walipo.

    Idadi ya waliofariki katika tetemeko la ardhi lililoikumba Colombia imefikia watu 181, huku vifo vingi vikiripotiwa katika miji ya Cali na Pereira.

    Tetemeko hilo lenye ukubwa wa 7.4 lilitokea saa 1:34 asubuhi kwa saa za nchini humo Jumatatu, na mitikisiko yake ilihisiwa katika maeneo makubwa ya magharibi mwa Colombia, huku mitetemeko midogo ikiendelea hadi Jumanne.

    Ingawa idadi rasmi ya vifo ni 181, mamlaka za eneo hilo zinasema huenda idadi hiyo ikaongezeka na kuvuka watu 240 kadiri shughuli za uokoaji zinavyoendelea.

    Rais wa Colombia Abelardo de la Espriella ametangaza hali ya dharura nchini humo.

    Akitoa taarifa kuhusu hali ilivyo mjini Pereira, mojawapo ya maeneo yaliyoathirika zaidi, rais amesema watu wapatao 2,600 wamejeruhiwa na takriban watu 200 bado hawajulikani walipo.

    Aidha, amesema zaidi ya nyumba 1,100 zimeharibiwa kabisa, huku zaidi ya nyumba 8,000 zikiharibiwa kwa viwango tofauti.

    Soma Zaidi Hapa:

  3. Idadi ya visa vya Ebola yafikia 4,449 nchini DRC

    Idadi ya visa vilivyothibitishwa vya Ebola katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC, imeongezeka hadi 4,449, huku watu 2,061 wakifariki, kwa mujibu wa takwimu za serikali zilizotolewa Jumanne usiku.

    Idadi ya waliofariki imeongezeka kwa asilimia 8.7 ndani ya siku mbili, hali inayoonyesha kasi ya kuongezeka kwa mlipuko huo.

    Haya yanajiri baada ya Shirika la Afya Duniani WHO kutangaza kuwa ebola 'inasambaa kwa kiwango cha kutisha'.

    Maambukizi ya sasa yamesababishwa na aina adimu ya virusi vya Ebola inayojulikana kama Bundibugyo, ambayo husababisha vifo kwa takribani robo ya watu wanaoambukizwa.

    Linalotia wasiwasi wanasayansi ni kuwa aina hii ya Ebola haina tiba.

    Maelezo zaidi:

  4. Wasyria washerehekea baada ya aliyekuwa rais Bashar Al Assad kuhukumiwa kifo

    Wakazi wa mji wa Idlib nchini Syria wamekusanyika kusherehekea baada ya mahakama kumhukumu kifo rais wa zamani wa nchi hiyo, Bashar al Assad.

    Picha za mitandaoni zinaonyesha watu wakishangilia katika mitaa ya Idlib, huku baadhi yao wakipanda magari na wengine wakiimba na kusherehekea uamuzi huo wa mahakama.

    Haya yanajiri baada ya Mahakama ya Syria kumhukumu kifo dikteta aliyeondolewa madarakani Bashar al-Assad licha ya kutokuwa mahakamani, baada ya kumpata na hatia kwa makosa ya kivita na uhalifu dhidi ya binadamu wakati wa vita vya wenyewe kwa wenyewe nchini humo.

    Assad alikimbilia Urusi pamoja na familia yake baada ya utawala wake kupinduliwa mwezi Desemba mwaka 2024, jambo lililohitimisha utawala wa familia yake uliodumu kwa miongo mitano.

    Katika kesi hiyo hiyo, mahakama pia ilimhukumu kifo Atef Najib, binamu yake Assad na aliyekuwa mkuu wa usalama wa kisiasa katika jimbo la Deraa kusini mwa Syria.

    Alionekana akiwa ndani ya kizimba mahakamani wakati jaji akisoma hukumu yake. Jimbo la Deraa linachukuliwa kwa kiasi kikubwa kuwa mahali ambapo vuguvugu la uasi dhidi ya utawala wa Assad lilianzia.

    Mnamo Machi 2011, kukamatwa na madai ya kuteswa kwa kundi la vijana walioshtakiwa kwa kuandika maandishi ya kupinga serikali kwenye kuta kulichochea maandamano jijini humo, ambayo yalikabiliwa na ukandamizaji mkali kutoka kwa vikosi vya usalama.

    Hatua hiyo ilichochea maandamano nchi nzima yaliyogeuka kuwa vita vya wenyewe kwa wenyewe vilivyosababisha vifo vya mamia ya maelfu ya watu.

    Serikali ya mpito ya Syria ilianza kuwashtaki maafisa waliohusishwa na utawala wa Assad ambao ulitawala nchi hiyo kwa zaidi ya miaka 50, mapema mwaka huu.

    Najib ni mmoja wa maafisa wa ngazi ya juu kabisa kufikishwa mahakamani.

    Pia Unaweza kusoma:

  5. Trump asema haiamini Iran na sasa Marekani inadhibiti Hormuz kikamilifu

    Rais wa Marekani Donald Trump amesema Jumatano kwamba hana imani na Iran, akisisitiza kuwa Marekani ina udhibiti kamili wa Mlango wa Hormuz.

    “Nitakuwa mtu wa mwisho kabisa kuamini Iran, wamekuwa wakinidanganya kila mara.”

    Awali, Kamandi Kuu ya Jeshi la Marekani, CENTCOM, ilisema kuwa imeizuia na kuifanya meli iliyokuwa ikielekea katika bandari ya Iran ishindwe kuendelea na safari.

    Katika taarifa iliyochapishwa kwenye mtandao wa X, CENTCOM ilisema meli hiyo iliyokuwa na bendera ya Panama ilikuwa ikijaribu kupita katika Ghuba ya Oman.

    Kwa upande mwingine, katibu mpya wa Baraza Kuu la Usalama wa Taifa la Iran, Mohsen Rezaei, amesema:

    “Mlango wa Hormuz hautafunguliwa hadi Marekani ibadili msimamo wake na ikubali masharti ya Iran.”

    Katika siku mbili zilizopita, Iran na Marekani zimeongeza ukali wa kauli zao kuhusu mzozo huo.

    Katibu wa Baraza Kuu la Usalama wa Taifa la Iran, Mohsen Rezaei, amesema Jumanne kuwa Mlango wa Hormuz utaendelea kufungwa hadi Marekani ikubali masharti ya Iran ya kumaliza vita.

    Masharti hayo ni pamoja na kuachiliwa kwa mali za Iran zilizogandishwa na kusitishwa kwa vita katika maeneo mbalimbali ya Mashariki ya Kati, likiwemo Lebanon na Gaza.

    Kauli hiyo imekuja baada ya Rais Trump Jumatatu kuitaka Iran ilipe fidia kwa watu waliouawa katika vita, mashambulizi na maandamano katika kipindi cha miaka 50 iliyopita.

    Katika kipindi chote cha mzozo huo, kauli za Trump zimekuwa zikibadilika kati ya kutishia kuongeza mashambulizi na kusema kuwa makubaliano yako karibu kufikiwa.

    Katika mahojiano yaliyorushwa Jumatatu usiku, Trump amesema hali ya sintofahamu inaweza kuendelea kwa muda, akisema huenda akaamua “kusubiri na kuona kitakachotokea.”

    Soma Zaidi:

  6. Trump asema alitumia ndege ya kijeshi kwa kuhofia Iran

    Rais wa Marekani Donald Trump amethibitisha kuwa alibadilisha ndege kwa siri alipokuwa akiondoka kwenye mkutano wa NATO nchini Uturuki mwezi uliopita, kutokana na uwezekano wa kuwepo kwa tishio la kiusalama.

    “Nafuata maelekezo ya Usalama wa Taifa na jeshi. Walitaka nipande ndege nyingine, kwa hiyo nalazimika kufanya wanachoniambia,” Trump aliwaambia waandishi wa habari Jumanne.

    Taarifa hiyo imekuja baada ya kuripotiwa kuwa Trump alipanda ndege ya Air Force One tarehe 8 Julai mbele ya kamera za televisheni, kabla ya kuhamishiwa kwenye ndege ya kijeshi kwa msaada wa gari la kubeba chakula.

    Mabadiliko hayo ya ghafla yameibua maswali kuhusu iwapo watu waliokuwa kwenye ndege iliyotumika kama chambo waliwekwa katika hatari. Hata hivyo, Trump amesema Jumanne kuwa ndege ya kijeshi aliyopanda ilikuwa katika “hatari kubwa zaidi”.

    Maafisa wameiambia CBS News, mshirika wa BBC nchini Marekani, kuwa Marekani ilikuwa imegundua tishio la kuaminika kutoka Iran la kurusha kombora kuelekea ndege hiyo.

    Waandishi wa habari na baadhi ya wafanyakazi wa Ikulu ya Marekani waliokuwa ndani ya ndege hiyo hawakujua kuwa Trump alikuwa ameondolewa kwa siri kupitia mpango maalumu wa kupotosha, kutokana na tishio linalodaiwa kutoka Iran.

    Soma Zaidi:

  7. Hujambo na karibu kwa matangazo ya moja kwa moja ya tarehe 12/08/2026.