Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Moja kwa moja, Iran: Tutasitisha mashambulizi iwapo Marekani haitatushambulia tena

Hatua hiyo imekuja baada ya Marekani kusitisha kwa muda kampeni yake ya mashambulizi ya anga.

Muhtasari

Moja kwa moja

Na Asha Juma

  1. Watu watatu wauawa na wanne kujeruhiwa katika katika tamasha la chakula Marekani

    Watu watatu wameuawa na wengine wanne kujeruhiwa baada ya shambulio la risasi lililotokea katika tamasha la chakula karibu na Space Needle mjini Seattle, Marekani.

    Mkuu Msaidizi wa Polisi wa Seattle, Tyrone Davis, amesema watu watatu wamefariki dunia kutokana na tukio hilo.

    Kwa mujibu wa Davis, waathiriwa wawili walifariki dunia papo hapo eneo la tukio kutokana na majeraha mabaya waliopata, huku mwathiriwa wa tatu aliyekimbizwa katika Hospitali ya Harborview Medical Center naye akifariki dunia baadaye kutokana na majeraha aliyoyapata.

  2. Waziri wa Somalia azuiwa kuingia Kenya

    Waziri wa masuala ya nchi katika Ofisi ya Rais, Abshir Bukhaari, ameripotiwa kuzuiwa kuingia nchini Kenya na baadaye kurejeshwa Mogadishu, kwa mujibu wa taarifa kutoka vyanzo mbalimbali.

    Maafisa wa uhamiaji wa Kenya katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Jomo Kenyatta (JKIA) jijini Nairobi wanadaiwa kumzuia kuingia nchini siku ya Jumapili kutokana na pasipoti ya Kenya aliyokuwa akisafiria.

    Serikali za Somalia na Kenya hazikuwa zimetoa kauli rasmi kuhusu tukio hilo.

    Taarifa hiyo inafuatia tukio jingine lililotokea takribani mwezi mmoja uliopita (Juni 24), lililomhusisha Naibu Waziri Mkuu wa Somalia, Jibril Abdirashid Haji, ambaye pia aliripotiwa kunyimwa kuingia nchini Kenya na kurejeshwa Somalia kutokana na madai kuwa alikuwa na pasipoti ya Kenya iliyopatikana kwa njia ya udanganyifu.

    Naibu Waziri Mkuu huyo aliwasili katika Uwanja wa Ndege wa JKIA kwa ndege ya Shirika la Saacid Airlines kutoka Mogadishu na kuwasilisha pasipoti halali ya kidiplomasia ya Somalia pamoja na visa ya kuingia Kenya.

    Taarifa zinasema maafisa wa uhamiaji walimtilia shaka baada ya kushukiwa kuwa pia alikuwa na pasipoti ya Kenya iliyopatikana kwa njia isiyo halali.

    Vyanzo vinavyofahamu suala hilo viliviambia vyombo vya habari vya ndani kuwa afisa huyo wa Somalia alikiri kuwa na pasipoti ya Kenya, lakini alikataa kuikabidhi, akisema suala hilo linapaswa kushughulikiwa kupitia mchakato wa mahakama.

    Mvutano huo ulisababisha Haji kupelekwa katika eneo la mapumziko la wageni maalumu la uwanja wa ndege wakati uchunguzi ukiendelea, kabla ya baadaye kusindikizwa kupanda ndege ya Shirika la Daallo Airlines iliyokuwa ikielekea Mogadishu, na hivyo kunyimwa rasmi ruhusa ya kuingia nchini Kenya.

    Hadi wakati huo, serikali za Kenya na Somalia hazikuwa zimetoa taarifa rasmi kuhusu tukio hilo.

  3. Wafcon 2026: Wawakilishi wa Afrika Mashariki Kenya wachapwa na Morocco

    Michezo ya kandanda ya mataifa ya Afrika kwa wanawake zimeanza kutimua vumbi jana Jumapili nchini Morocco na kuchezwa michezo miwili ya kukata utepe.

    Katika mchezo wa kwanza Algeria waliwanyuka Senegal 2-0 magoli ya dakika ya 42 na 85 huku wenyeji Morocco wakiwanyanyasa wawakilishi wa Afrika Mashariki Kenya kwa ushindi wa magoli 4-0.

    Magoli matatu yalitiwa kimiani ndani ya dakika 32 za kwanza la nne likafungwa dakika 2 tu baada ya mapunziko.

    Leo kuna michezo miwili. Afrika Kusini itakipiga na wawakilishi wengine wa Afrika Mashariki Tanzania saa mbili usiku kabla ya Ivory Coast kutoana jasho na majirani zao wa Kaskazini, Burkina Faso.

    Pia unaweza kusoma:

  4. Macron aitisha kikao cha dharura huku moto mkubwa wa nyika ukiendelea

    Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron ataongoza kikao cha dharura cha baraza la mawaziri leo Jumatatu huku moto wa nyika ukikaribia mji wa Bordeaux, ulioko kusini-magharibi mwa nchi hiyo.

    Wimbi jingine la joto linatarajiwa kufanya juhudi za kudhibiti moto huo unaoendelea kuenea kuwa vigumu. Moto huo kwa sasa uko umbali wa takribani kilomita 15 (maili 9) kutoka Bordeaux, meya wa mji huo, Thomas Cazenave, alisema. Awali, alisema hakuna mpango wa kuwahamisha wakazi wapatao 850,000 wa mji huo.

    Ufaransa imekuwa miongoni mwa maeneo yaliyoathirika zaidi, huku hekta 42,000 zikiathirika na moto kusini-magharibi mwa nchi hiyo. Hilo limeufanya kuwa miongoni mwa moto mkubwa zaidi wa misitu nchini humo tangu Vita vya Pili vya Dunia.

    Kwa jumla, zaidi ya watu wapatao laki mbili na ishirini wamehamishwa katika eneo la kusini-magharibi mwa Ufaransa.

    Kapteni Nicolas Braz, mmoja wa viongozi wa operesheni ya kuzima moto, amesema moto huo ulikuwa na upepo mkali sana ukiambatana na vimbunga vidogo”, na kuongeza kuwa ulikuwa “haueleweki na usioweza kudhibitiwa.

    Wakazi wa Le Porge, mojawapo ya miji ya pwani iliyoathiriwa na moto huo, wameanzisha mtandao wa kujitolea wa kusaidia wazima moto waliochoka. Wanawapikia chakula na kuwapa mahali pa kupumzika kati ya zamu zao.

    Zaidi ya nyumba 150 zimeharibiwa katika mji huo wenye wakazi 3,500.

    Wakaazi wengi wanasema wamehuzunishwa na tukio hilo ulioathiri misitu yake, wanyamapori na watu waliopoteza vitu vingi,” alisema Augonnet.

    “Kwa sasa, tunazingatia kuchukua hatua, hivyo hatuna muda wa kufikiria sana. Nadhani sehemu yenye changamoto itakuja baadaye, wakati wa kuanza tena ujenzi.

    Wakati huo huo nchini Uhispania, moto unaendelea kusambaa, huku zaidi ya watu 90,000 wakihamishwa kutoka maeneo yanayozunguka Madrid na Ávila.

    Takriban hekta 77,000 zimeathiriwa na moto nchini Uhispania, alisema Waziri wa muda wa Ikolojia, Sara Aagesen, siku ya Jumapili.

    Soma Zaidi:

  5. Iran: Tutasitisha mashambulizi iwapo Marekani haitatushambulia tena

    Iran ameliambia shirika la habari la Reuters siku ya Jumapili kuwa itasitisha mashambulizi yake, mradi tu Marekani nayo iendelee kusitisha mashambulizi yake, kulingana na afisa mmoja mwandamiz.

    Hatua hiyo imekuja baada ya Marekani kusitisha kwa muda kampeni yake ya mashambulizi ya anga, kufuatia washauri wa Rais Donald Trump kumweleza kuwa walikuwa wakikabiliwa na wasiwasi kuhusu kupungua kwa akiba ya silaha za Marekani.

    Baada ya usiku 13 mfululizo wa mashambulizi makali ya anga ya Marekani dhidi ya Iran, Wizara ya Ulinzi ya Marekani ilisisitisha operesheni hiyo mwishoni mwa Ijumaa.

    Hakukuwa na mashambulizi yoyote ya Marekani yaliyoripotiwa Jumamosi wala Jumapili.

    Kwa upande wake, Iran, ambayo ilikuwa ikijibu kila usiku wa mashambulizi ya Marekani kwa kushambulia nchi jirani zinazohifadhi kambi za kijeshi za Marekani, pia haijafanya mashambulizi yoyote kwa siku mbili zilizopita hadi sasa.

    Afisa huyo wa Iran, ambaye alizungumza na shirika la habari la Reuters kwa sharti la kutotajwa jina, alisema msimamo wa Tehran unaendelea kuwa "shambulio kwa shambulio." Alieleza kuwa, "Iwapo mashambulizi yatasitishwa, Iran pia itasitisha operesheni zake. Ujumbe huo tayari umefikishwa kwa Marekani."

    Kwa upande mwingine, Balozi wa Marekani katika Umoja wa Mataifa, Mike Waltz, aliviambia kipindi cha Fox News Sunday pamoja na vyombo vingine vya habari vya Marekani kuwa Rais Donald Trump aliamua kusitisha kwa muda mashambulizi ya Marekani ili kutoa nafasi zaidi kwa juhudi za kidiplomasia.

    Akizungumza kuhusu uamuzi wa Rais Donald Trump, Balozi wa Marekani katika Umoja wa Mataifa, Mike Waltz, alisema:

    "Antoa fursa kwa mazungumzo yaendelee; anatoa muda kidogo ili yaweze kusonga mbele."

    Maafisa wa jeshi la Marekani katika siku za karibuni wameonya kuwa mashambulizi ya mabomu yaliyofanywa katika kipindi cha wiki mbili zilizopita, yaliyolenga kuzuia vitisho vya Iran dhidi ya usafirishaji wa meli katika Mlango-Bahari wa Hormuz—njia ya maji ambayo imesababisha mvutano katika vita hivyo—yalikuwa yamekaribia kumaliza maeneo lengwa yaliyokuwa yamechaguliwa mapema kwa ajili ya kushambuliwa, kwa mujibu wa afisa mmoja wa Marekani aliyezungumza kwa sharti la kutotajwa jina.

    Soma Zaidi:

  6. Hujambo na karibu katika matangazo yetu mubashara, tarehe ni 27/07/2026