Matumizi ya mitandao ya kijamii kwa vijana na watoto unamulikwa darubini kali katika kesi ambayo imeanza kusikilizwa huko California Marekani.
Mawakili wa majimbo29 ya Marekani wanaishutumu Kampuni ya Meta kwa kusababisha watoto kutumbukia katika uraibu wa kutumia visivyo mitandao yao ya Facebook na Instagram huku wakiupotosha umma kuhusu hatari zake.
Meta inakanusha madai hayo, lakini imekiri kwamba baadhi ya watumiaji wa mitandao ya kijamii wanakabiliwa na changamoto.
Majimbo hayo ya Marekani yanataka Meta kutozwa mabilioni ya dola. Mahakama pia inaweza kuamuru mabadiliko katika jinsi Facebook na mitandao mingine ya kijamii inavyofanya kazi.
Mahakama imesikia hoja kutoka kwa mawakili wanaowakilisha majimbo hayo kwamba Meta ilikusudia kukiteka kimawazo kizazi cha sasa cha watoto kwenye Facebook na Instagram.
Baraza la majaji huko Oakland, California litatumia wiki sita zijazo kuchunguza madai ya mawakili wakuu kutoka majimbo kadhaa ya Marekani, na mawakili wa kampuni hiyo ya mitandao ya kijamii, ambao kila mmoja alipinga hoja za mwenzake wakati kesi hiyo ikifunguliwa hapo jana Jumanne.
Wakili wa jimbo la California alidai Meta iligundua mamilioni ya watoto wenye umri wa miaka 11 na 12 walikuwa kwenye Instagram na haikuchua hatua za kutosha kuwazuia watoto hao. Hata hivyo, Wakili wa Meta alisema ni takriban watumiaji laki moja tu wa umri huo waliogunduliwa na pia alidai uraibu wa mitandao ya kijamii haupo.
Baada ya wakili wa jimbo la California kusema Meta ilifahamu majukwaa yake yanadhuru afya ya akili ya vijana, upande wa Meta ulisema kampuni hiyo inapuuzwa kutokana na jinsi ilivyochangia vijana wengi zaidi kuwa na wakati mzuri na wanavyonufaika na mitandao hiyo.
Kesi hiyo inatokana na kesi iliyofunguliwa mwaka 2023 na majimbo 29 ya Marekani, yanayodai ukiukwaji mkubwa wa sheria za Serikali kuu na za majimbo kuhusu kulinda faragha za watoto.
Si tu kwamba majimbo hayo yanadai mabilioni ya dola kutoka kwa Meta, pia yanaitaka ifanye mabadiliko kwenye Instagram na Facebook, ikiwa ni pamoja na kukomesha idadi ya "likes" na mfumo wa kusogeza mbele maudhui bila kikomo.