Shirika la ndege la Uganda lasitisha safari za Kinshasa kwa hofu ya Ebola
Shirika la ndege la Uganda Airlines limetangaza kusitisha kwa muda safari za ndege kwenda na kutoka Kinshasa kufuatia hofu ya mlipuko wa Ebola hivi karibuni katika eneo hilo.
Katika taarifa kwa umma iliyotolewa na usimamizi wa shirika hilo la ndege, kampuni hiyo ilisema uamuzi huo utaanza kutekelezwa kuanzia Mei 23, 2026, hadi watakapotoa taarifa nyingine
Shrika hilo aidha limesema kuwa uamuzi huo umechukuliwa “kama hatua ya tahadhari kwa maslahi ya afya, usalama, na ustawi wa abiria wetu, wahudumu wa ndege, na abiria kwa ujumla.”
Shirika hilo la ndege lilisema kuwa abiria walioathiriwa na kusitishwa kwa safari wanapaswa kuwasiliana na kampuni kupitia njia zake za huduma kwa wateja ili kupata msaada.
“Tunasikitika kwa usumbufu wowote utakaosababishwa na hali hii na tutashkuru kwa uelewa na ushirikiano wa wateja wetu tunaowathamini katika kipindi hiki,” taarifa hiyo ilisema.
Uganda Airlines iliongeza kuwa itaendelea kufuatilia hali hiyo “kwa karibu kwa kushirikiana na mamlaka husika za afya na usafiri wa anga,” na kusema kuwa taarifa zaidi zitatolewa zitakapopatikana.
Mnamo Mei 21, Uganda ilithibitisha visa viwili vya kuambukizwa kutoka nje vya aina ya Bundibugyo ya Ebola vinavyohusishwa na mlipuko unaoendelea katika Jamhuri ya Demokrasi ya Congo (DRC), jambo lililosababisha kuimarishwa kwa ufuatiliaji na hatua za dharura za kukabiliana na ugonjwa huo nchini kote.
Katibu wa kudumu katika Wizara ya Afya ya Uganda, Diana Atwine, alisema kuwa mmoja wa wagonjwa hao amefariki dunia huku mgonjwa wa pili akiendelea kupata nafuu baada ya kupatikana hana maambukizi ya Ebola katika vipimo vilivyofanywa Mei 18 na Mei 20
Atwine alisema mamlaka tayari zimewatambua na kuwaweka watu 127 waliokaribiana na wagonjwa hao chini ya karantini ya taasisi kama sehemu ya juhudi za kudhibiti ugonjwa huo.
Soma zaidi: